Mara nyingi sana

5:45:00 PM Unknown 0 Comments


MARA NYINGI SANA
(Saba mara sabini)
Wanaofuatilia huduma ya Uinjilisti watakuwa wanamfahamu au kumsikia ndugu Jimmy Swaggart, yeye hupenda kujiita brother Swaggart, ni mwinjilisti mwenye alama ya aina yake na mwenye kutembea mwendo mrefu kwa miaka kadhaa katika huduma aliyopewa. Ameonja kuanguka na kusimama na hapa anatoa funzo: “Msalaba wa Yesu kila siku unatenda kazi kamwe haushindwi, ni mimi na wewe tunaoweza kushindwa. Sisemi kama ikitokea ukianguka (maana utaanguka kweli) kama hautaacha kumwamini Yesu hata katika anguko lako, Yeye Bwana Yesu hatakuacha na mwishowe atakusimamisha maana hujaacha kumwamini hata katika kuanguka kwako.”
Kwa tafsiri yangu Jimmy anasema, kuanguka kupo, ndio maana haoni sababu ya kusema ikitokea ukianguka maana anajua itatokea. Katika huduma yake ameanguka na kusimama, anajua machungu ya kuanguka, anasisitiza tusikate tamaa maana msalaba wa Yesu unauweza wa kuokoa nyakati zote. Asubuhi moja nikiwa katika Studio za Ileje Fm radio msikilizaji aliniuliza kama, Mungu anaweza kusamehe dhambi kubwa. Nilimjibu, “Ndiyo anaweza, mara nyingi tu.” Si tu kwamba Mungu anasamehe bali anasamehe mara nyingi. Many times!
Baadaye nilimpa mfano tuliopewa na paroko kanisani kwetu, nanukuu: “mtu mmoja alimuuliza padre mmoja akisema, ‘padri nimemuua bosi wangu, Je! naweza kusamehewa? Padri akamjibu akasema, ‘unaweza kusamehewa bila shaka’ yule bwana akaendelea akasema, ‘wakati nikimuua bosi wangu dereva wake aliniona, ili kufuta ushahidi nikamuua na dereva je, naweza kusamehewa? Akamjibu ndiyo bila shaka. Akamwambia, ‘Padri niwie radhi kwani, nilipokuwa nikimuua dereva mke wa bosi aliniona ikabidi nimchinje na yeye pia. Vipi na hilo nalo Mungu anaweza kusamehe? Padri akajibu ndiyo bila shaka.’”
Usikate tamaa  Mungu anaweza kukusamehe haijalishi umefanya nini. Somo kuu la mfano hapo juu ni hili; Si kwamba Mungu anaweza kusamehe tu, bali anaweza kusamehe mara nyingi zaidi.
Mungu ni upendo. Maandiko yanasema upendo husitiri dhambi nyingi. Usipokata tamaa Mungu hatakuacha, na hata ukikata tamaa yeye ataendelea kukutafuta maana wokovu wako ni muhimu. Si sisi tuliomtuma mjumbe aende mbinguni kumshusha Yesu ili aje atuokoe bali ni Mungu aliyemtuma Yesu ashuke kutuletea wokovu.
Kila mtu anaweza kusamehe lakini si kila mtu anaweza kusamehe mara nyingi. Tabia kuu ya kimungu (great godly character) haiko katika kusamehe tu, bali iko katika kusamahe mara nyingi zaidi. Hata wapagani kuna nyakati husamehe, lakini hawawezi kufanya hivyo zaidi ya mara saba. Mitume walidhani, unaweza kusamehe mara saba tu, na kumbe ni zaidi ya hapo.
Msamaha unaponya mahusiano, unaponya ndoa, unaponya kanisa na nchi kwa ujumla. Asiye mfuasi wa msamaha ni mfuasi wa vita. Kuna wengine husema jino kwa jino, hili linawezekana ikiwa tu aliyekukosea ni mdogo. Ikiwa unapenda kulipiza kisasi badala ya kusamehe napenda kukuuliza, Je, utafanya nini ikiwa aliyekukosea anazo nguvu kuliko wewe? Je, utafanya nini ikiwa aliyekukosea ni mkuu sana? Naamini utamwachia Bwana maana, kisasi ni juu yake. Kama hatuwezi kusamehe hatuwezi kumwachia Mungu, kwani tutaona kama vile Mungu hawezi kumwadhibu vizuri mhusika.  Jifunze kusamehe mara nyingi zaidi, tamka msamaha sirini na hadharani pia, wewe uliyesamehewa makosa yako unawezaje kushindwa kusamehe wengine? Mathayo 6:14-15
Leo ninakuachia kazi ya nyumbani (home work) ifuatayo, piga simu, tuma meseji ya kusamehe na kama aliyekukosea yuko karibu mwambia nimekusamehe.
BARIKIWA

0 comments :