Kuanzia viongozi .......

9:15:00 AM Unknown 0 Comments

KUANZIA VIONGOZI HADI WAFUASI WAO
(Sote tunamuhitaji Yesu)
Sote tunamuhitaji Yesu kuanzia viongozi wa dini kama Papa Francis mpaka Viongozi wa siasa kama Barack Obama sote kwa ujumla tunamuhitaji mwokozi. Hakuna wokovu kwa mtu awaye yote ila kwa Yesu Kristo tu. Nukuu za Alexender The Great ni simulizi zenye mafunzo tele. Kuna nyakati alinukuliwa akisema, “Nitakapokufa nataka jeneza langu libebwe na madaktari bingwa, waweke mikono yao juu ya jeneza langu ili watu wajue wazi kwamba kuna nyakati, hata madaktari wazuri hawataweza kuokoa maisha.”
Madaktari bingwa wanaposhindwa wanamfanya mwanadamu akumbuke kwamba, hakuna uzima kwa mtu awaye yote isipokuwa kwa Yesu Kristo. Bill Graham anasema, “Hata wanasayansi wasiomjua Mungu wala kumkiri wakishaugua saratani (cancer) huanza kukiri na kusema Mungu nisaidie”. Biblia inamfananisha mwandamu na ua ambalo leo lipo na kesho halipo tena. Hakuna la kudumu ndani ya mwanadamu.
Nje ya Yesu Kristo mwanadamu ni kama kivuli punde hayupo tena. Mwandamu anapata uzima ndani ya Kristo na si uzima tu unaokomeshwa na kifo bali uzima ulio juu ya kifo. Kifo hakiwezi kukomesha maisha ya mtu amwaminiye Kristo Yesu. Iko wazi katika 1Kor 15:55-56 Yesu Kristo alishinda kifo kwa ajili yetu hata ikaandikwa, Ku wapi, Ewe mauti, kushinda kwako? U wapi, Ewe mauti, uchungu wako? 56 Uchungu wa mauti ni dhambi, na nguvu za dhambi ni torati.
Mauti imeshindwa, mauti imechoka na uzima wa Yesu Kristo umetawala tena. Mauti ilipata nguvu kupitia dhambi naye Yesu Kristo alipokwisha kutusamehe dhambi zetu basi aliivunja ile nguvu ya mauti. Ndio maana watu wengi waliokuwa karibu na kufa alipowaambia wamesamehewa dhambi waliponywa, maana nguvu ya mauti ni dhambi, dhambi ikiondolewa mauti hukosa nguvu. Wamwaminio hawaogopi kifo.
Je, unahisi kufa? Je, unaogopa kifo? Nguvu ya uhai inakuja kupitia msamaha. Wale wenye hakika kwamba, Mungu amewasamehe dhambi zao kamwe hawaogopi kifo. Biblia inasema, “anaraha aliyesamehewa dhambi”, kwa lugha nyingine anafuraha aliyesamehewa dhambi. Waliosamehewa dhambi wamebarikiwa tena biblia inasema wanayo heri. Zaburi 32:1-2
Yesu aliishinda mauti kwa kupitia kuishinda dhambi. Na hakuna mwandamu awaye yote aliyeishinda dhambi na kuiharibu pale msalabani isipokuwa Yesu Kristo peke yake. Madaktari, walimu, viongozi wa siasa, viongozi wa dini hawakuweza na hawataweza ni Yesu peke yake. Mhimili (mzizi) wa kifo ni dhambi, unapotubu unafukuza mauti na hofu zake.
Tumaini la uhai na uzima wetu ni Kristo peke yake. Kama tungelikuwa na uzima Yesu asingelikuja. Kama tungelikuwa wema asingekuja pia. Kwa hiyo amekuja kwa sababu tulikuwa wafu kwa dhambi, watupu kwa uovu wetu na wachafu kwa matendo yetu.
Mwimbaji mmoja anasema, “All I need is you” ni kweli tunamuhitaji Yesu peke yake. Tunamuhitaji kila saa na kila wakati. Ni vema tusogelee mahali anapokaa. Twende kitini pake kwa toba. Imeandikwa, “Basi na tukikaribie kiti cha neema kwa ujasiri, ili tupewe rehema, na kupata neema ya kutusaidia wakati wa mahitaji. ” Waebrania 4:16
Yesu anapatikana katika kiti cha rehema na biblia inasema, “wakati wa mahitaji”. Je! ni wakati gani huo tunaohitaji neema na rehema? Ni kila saa na kila dakika. Mara kadhaa asubuhi nimekuwa nikipiga magoti na kuomba neema ya siku husika, kwa kuwa najua ninahitaji neema kila siku. Najua namuhitaji Yesu kwa uhai wangu.
Siku ukitenda dhambi unahitaji neema, na siku usipotenda dhambi unahitaji neema pia. Na kama tunahitaji neema kila siku na kila saa basi moja kwa moja tunamuhitaji Yesu kila siku na kila saa. Yeye ndiye mtoaji wa neema hizo. Pata muda wa kuomba sote tunahitaji neema...tukutane wiki ijayo mpendwa. Barikiwa

0 comments :