Weka imani yako .......

9:36:00 AM Unknown 0 Comments

 
WEKA IMANI YAKO KATIKA KAZI TIMILIFU YA YESU KRISTO
Kwa maana yeye aliyeingia katika raha yake amestarehe mwenyewe katika kazi yake, kama vile Mungu alivyostarehe katika kazi zake…” Waebrania 4: 10
Kazi yote aliyofanya Kristo hapa duniani haikuwa kwa ajili yake mwenyewe, ilikuwa ni kwa ajili ya mimi na wewe. Alikufa ili sisi tupate kuwa hai, alichukua magonjwa yetu ili sisi tupate kufurahia afya na uzima wake katika maisha yetu. Amechukua huzuni, mahangaiko, masikitiko na mizigo yote katika maisha ili sisi tupate amani na kustarehe kwa kazi yake. Kazi zote alizifanya kwa ajili yetu ili sisi tupate kustarehe katika Yeye. Ikiwa Kristo amekufa msalabani kwa ajili ya dhambi zetu, sisi hatuwezi kufa tena; bali tutastarehe katika kazi yake.
Njia pekee ya sisi kuona na kufurahi matokeo ya utimilifu wa kazi ya Mungu katika maisha yetu ni imani, Tunapoamini juu ya kazi yake katika eneo fulani la maisha yetu ndipo hapo matokeo ya kazi hiyo hudhihirika. Ikiwa kuna jambo unahisi limekuwa mzigo kwako[burden] na kukuelemea katika maisha yako au familia, kazi zako au shughuli zako; mwaka huu unapoanza weka imani yako katika kazi timilifu ya Yesu Kristo na katika Ahadi ya Neno lake. Kumbuka, Tunaitwa katika raha ya Kristo kwa njia ya imani yetu katika kazi yake timilifu.  
Njoni kwangu, ninyi nyote msumbukao na wenye kulemewa na mizigo, nami nitawapumzisha” Mathayo 11:28
Unapoanza mwaka mpya, wito wetu kwako ni kwamba, jifunze kuweka imani yako katika kazi timilifu ya Yesu Kristo ili upate kuona Ukuu wa Mungu ukifunuliwa katika maisha yako ndani mwaka huu. Ikiwa amesema atafanya jambo fulani katika maisha yako, huna sababu ya kumsaidia kufanya kwa kuwa hofu au mahangaiko nafsini mwako; kazi yako ni moja tu kuingia katika raha yake na kustarehe huku ukijua kuwa Yeye anawajibika na maisha yako [Kutoka 14:14].
Maana Yeye alisema, ikiwa; Na Yeye aliamuru, ikasimama” Zaburi 33:9
Tunapoweka imani katika kazi yake na ahadi yake, tunauhakika ya kwamba kila kitu kipo katika mikono salama; hivyo hofu, mashaka, kuelemewa katika nafsi na mahangaiko hutoweka. Unapoanza mwaka huu, amua kwa dhati kuweka imani yako katika kazi timilifu na Ahadi yake, haijalishi mwaka jana hali ilikuwaje; kwa kuwa Bwana anafanya jambo jipya. Mazingira ya mwaka jana, yasikukwamishe kumuamini Mungu  katika mwaka huu mpya. Kumbuka jambo hili, Mungu anapotoa ahadi; kwake jambo hilo limeshakamilika. Na tunapoamini ahadi hiyo, haiwi tu upendeleo bali inakuwa haki yako kisheria [legal right].
Lakini akiiona ahadi ya Mungu hakusita kwa kutokuamini, bali alitiwa mguvu kwa imani, akimtukuza Mungu; huku akijua hakika ya kuwa Mungu aweza kufanya [kudhihirisha] yale aliyoahidi. Kwa hiyo ilihesabiwa kwake kuwa ni haki” Warumi4: 20-21 [Msisitizo umeongezwa]
Kazi ya Yesu Kristo haikulenga tu katika kuleta utimilifu wa roho ya mtu [anayeamini], lakini pia ililenga kuleta utimilifu wa nafsi, mwili na jamii yake; ili kurejesha hadhi ya Kimungu katika maisha ya mtu huyo na mazingira yake. Hivyo, unayohaki ya kumuamini Mungu ili Kazi zake, Ukuu wake na Uweza wake uweze kuwa dhahiri [kufunuliwa] katika maisha yako, familia, watoto, mipango, biashara, kazi, jamii au Taifa…nk. [Luka 4:18-19]
Ni nani aliyesadiki habari tuliyoileta? Na mkono wa Bwana amefunuliwa nani?” Isaya 53:1 
Katika mwaka huu mpya 2016, Mwenyezi Mungu akufadhili na kukuangazia Nuru ya uso wake.
Heri ya Mwaka Mpya 2016

0 comments :