Yesu ni mwalimu mwema

12:19:00 PM Unknown 0 Comments

 
YESU NI MWALIMU MWEMA.
Tuyatii Maagizo Yake
Kijana mmoja tajiri alimwendea Yesu na kumwita, “mwalimu mwema” naye Yesu akitaka sana kumtukuza Baba wa Mbinguni akasema, “aliye mwema ni mmoja”. Kwa kawaida mtu anapokusifu au anapokupa heshima yako huonesha utii kwa nafasi yako. Katika dunia ya leo tunawasomi wanaoitwa daktari bigwa, Profesa, wako wahandisi hata marubani.
Kuwasifia wataalamu hawa pasipo kutekeleza wanachosema ni sawa na kufukuza upepo, ni kuwavisha kilemba cha ukoka. Kumwita mtu Daktari bingwa hakuleti maana ikiwa akikikushauri jambo lihusulo afya utakataa . Ni heri asiyemwita kwa cheo lakini akafuata maelekezo yake. Vivyo hivyo haileti maana tumwitapo Yesu mwalimu ilhali hatufuati asemalo. Ukimjua Yesu kama mwalimu mwema lazima ukubali kufanya asemalo hata kama kwa akili za kawaida linaonekana ni la ki-puuzi au ni la kuaibisha.
“Ukimjua Yesu kama mwalimu mwema lazima ukubali kufanya asemalo hata kama kwa akili za kawaida linaonekana ni la ki-puuzi au ni la kuaibisha”
“Na tazama, mtu mmoja akamwendea akamwambia, Mwalimu, nitende jambo gani jema, ili nipate uzima wa milele? Akamwambia Kwani kuniuliza habari ya wema? Aliye mwema ni mmoja. Lakini ukitaka kuingia katika uzima, zishike amri. Akamwambia, Zipi? Yesu akasema, Ni hizi, Usiue, Usizini, Usiibe, Usishuhudie uongo, Waheshimu baba yako na mama yako, na, Mpende jirani yako kama nafsi yako. Yule kijana akamwambia, Haya yote nimeyashika; nimepungukiwa na nini tena?  Yesu akamwambia, Ukitaka kuwa mkamilifu, enenda ukauze ulivyo navyo, uwape maskini, nawe utakuwa na hazina mbinguni; kisha njoo unifuate. Yule kijana alipolisikia neno lile, akaenda zake kwa huzuni; kwa sababu alikuwa na mali nyingi.” Mathayo 19:17-22
Licha ya kumwita Yesu mwalimu mwema yaani, “Good Master” lakini kijana hakukubali ushauri wa Yesu. Alipoambiwa auze kila kitu na kuwapa masikini hakukubali. Anajua Yesu ni mwalimu mwema, anajua Yesu ni mtaalamu wa roho, mwili na nafisi za  wanadamu lakini hataki kumtii anachosema. Alijua Yesu ni kila kitu lakini hakutaka kumsikia. Wako wengi wanamwita Yesu Bwana, wengine wanasema, “nakupenda Yesu” lakini hawataki kutii neno lake. Yeye mwenyewe anasema, “mkinipenda mtalishika neno langu”
Naamani Yule Jemedari anafanana na huyu kijana tajiri. Yeye alipokwenda kwa Elisha nabii hakutaka kujichovya mtoni mara saba. Alitaka Elisha amwekee mkono. Mara nyingi tunapokwenda mbele za Mungu tunakosea, tunakwenda kumwagiza badala ya kwenda kumsikiliza. Mungu anaweza asiseme na wewe kwa njozi, wala kwa nabii wala kwa dalili. Lakini kupitia neno lake (Biblia) anasema nasi kila siku. Kila tunaposoma maandiko tunasikia sauti ya Mungu. Biblia ni redio yake, isome na usikilize. Naamani hakutaka kusikia maagizo ya nabii bali alitaka nabii ndiye afuate mawazo na maagizo yake. Lakini Naamani akakasirika, akaondoka, akasema, Tazama, nalidhania, Bila shaka atatoka kwangu, na kusimama, na kuomba kwa jina la Bwana, Mungu wake, na kupitisha mkono wake mahali penye ugonjwa, na kuniponya mimi mwenye ukoma.”2 Wafalme 5:11
Jambo zuri ni kwamba, kijana tajiri alimuuliza Yesu swali ambalo kila mwenye akili timamu anapaswa kujiuliza. Mtu mzima hapaswi kujiuliza maswali ya kisiasi tu, bali anapaswa kujiuliza maswali yahusuyo umilele wake na watoto wake. Kijana akamuuliza Yesu, “nifanye nini ili nirithi uzima wa milele?”. Hakuuliza kwa habari ya Simba na Yanga, wala hakuuliza kwa habari ya CHADEMA na CCM, hakugusa habari za kuoa na kuolewa wala hakuhoji kwa habari ya Manchester United na Arsenal bali alihoji kuhusu uzima wa milele. Kwa hili ninampongeza. Kila mwenye hekima ni lazima ajue atakuwa wapi baada ya kifo. Swali hili linapaswa kutawala akili ya kila mwanadamu. Uzima wa milele! Uzima wa milele! Uzima wa milele!
“Si vibaya kumiliki pesa, lakini ni hatari kama pesa zitatumiliki sisi hata tushindwe kumpa Mungu nafasi ya kwanza””
Yesu akimjibu Yule kijana alimwambia akitaka uzima wa milele azishike amri, wewe na mimi pia tukitaka uzima wa milele ni muhimu tuzishike amri zake Mungu. Si vibaya kumiliki pesa, lakini ni hatari kama pesa zitatumiliki sisi hata tushindwe kumpa Mungu nafasi ya kwanza. Yule kijana aliiona ni heri akose ukamilifu lakini abakie na pesa. Aliona bora akose furaha lakini abakie na pesa. Aliondoka kwa huzuni, watu wengi wana pesa lakini hawana furaha ya kweli, mali zao zimewatenga na ukamilifu.
Uzima wa milele unapatika kwa kumwamini BWANA YESU. Tena kila aliaminiye jina lake anao uzima wa milele. Ukimwamini leo na kuisikia sauti yake utaokoka. Usimwite BWANA kama hutaki kufanya aliyokuamuru yaani, kushika amri zake. 
Siku ya mwisho Yesu atawaita mashahidi wawili, ataliita neno lake na kupima utii wetu kwa neno lake. Agano jipya ni shahidi wa pili na Agano la kale ni shahidi kwanza. Mashahidi hawa wawili watapima utendaji wetu wa neno. Nami nitawaruhusu mashahidi wangu wawili,”Ufunuo 11:3a

0 comments :