Yanayo Ondoa Furaha Yetu

2:35:00 PM Unknown 0 Comments

 

YANAYO ONDOA FURAHA YETU
Yako mambo mengi yanayotuondolea furaha na kutujaza mioyo yetu huzuni kuu.  Kuyajua mambo hayo ni ufunguo kuelekea furaha ya kweli. Mambo hayo ni pamoja na dhambi. Dhambi hufanya tujisikie vibaya, toba ya kweli huturejeshea furaha hiyo. Kama tunataka nyakati za kubarizi katika uwepo wa Mungu ni lazima tutubu; Mungu ameahidi kwa kinywa cha mtume Petro kwamba tukitubu tutapata burudiko la moyo.
 Tubuni basi, mrejee, ili dhambi zenu zifutwe, zipate kuja nyakati za kuburudishwa kwa kuwako kwake Bwana;” Matendo ya Mitando 3:19  Ahadi gani nzuri kama hii? Ningekuwa na kalamu ningeandika pembeni ya mstari huu, “I can’t miss this promise”. Burudani itarajea baada ya toba, uchungu na mgandamizo wa mawazo vitatoweka tukitubu. Yanayoondoa furaha yetu ni mengi, lakini toba ni mlango wa pekee wa kurejesha furaha.
Fyodor Dostoevsky ni Mrusi aliyeacha alama ya aina yake, maneno yake yamejaa mafunzo. Katika moja ya kauli zake anasema, “The greatest happiness is to know the source of unhappiness” kwa tafsiri isiyo rasmi, “Furaha kuu ni kujua chanzo cha mambo yanayotuhuzunisha”. Ukishajua nini chanzo cha huzuni yako basi huna budi kujitahidi kukifunga chanzo hicho.
Wakati mwingine tunagubikwa na huzuni kwa sababu ya kuficha siri ambazo zinatuumiza sisi wenyewe, hakikisha unatumia hekima kutoka katika kitanzi hicho. Wakati mwingine ni uhusiano usio afya; nao pia si wa kuulea sana.
Ni kweli kabisa, hatuwezi kukwepa maumivu ya kukosa uadilifu au huzuni ya udhalimu. Ni ama uingie gharama ya kuwa mwadilifu na mwaminifu au uingie gharama ya kuwa dhalimu na asiyeaminika. Kukimbia dhambi ni gharama, lakini kutenda dhambi na kukaa nayo ni gharama kubwa zaidi.
Watu wengi wenye dhambi hawapendi kusali. Ninapata funzo kubwa katika Luka 18:13 ninaposoma kwamba mwenye dhambi alikwenda kusali na Mungu akajibu sala yake. Ni jambo zuri mno kwamba, Mungu huwasikiliza hata wadhambi. Ikiwa Mungu huwasikiliza hata waovu basi tunataraji kuona dunia nzima ikisali.
Tatizo si dhambi, tatizo ni kutokwenda kusali; tatizo ni kutokumwendea Mungu. Wenye makosa wengi hawapendi kusali na ni ujanja wa shetani kwani anajua wakisali Mungu atawasikia na kuwasamehe. Twendeni tukasali, twendeni tukaombe toba. Wito wa toba si wito kwa watu binafsi tu, bali ni wito kwa makanisa, taasisi za kiraia, mashirika, mataifa na dunia nzima, sote tunahitaji kutubu.
Inawezekana umekosea, unahuzuni na unaogopa kusali tafadhali leo naomba tusali pamoja. Nalifurahi Yesu aliposema mtoza ushuru mwenye dhambi alikwenda kusali [Luka 18:10na 13]. Oh! akatoka amesamehewa na amejibiwa. Mpendwa usikate tamaa amua kusali leo. Nikualike useme maneno haya kwa imani kama mwanzo wa sala yako leo: “ BWANA YESU WEWE UMEWAKUBALI WAKOSAJI NA MIMI UNANIKUBALI. NAOMBA UNIREHEMU KWA DHAMBI ZANGU ZOTE AMBAZO NIMETENDA. NINA KIRI WEWE NI BWANA NA NINAAMINI MUNGU ALIKUFUFUA KUTOKA KWA WAFU” AMINA.


0 comments :