Umuhimu wa kutambua kusudi - III

3:02:00 PM Unknown 0 Comments

 
UMUHIMU WA KUTAMBUA KUSUDI III
Moyo wa mtu hufikiri njia yake; Bali Bwana huziongoza hatua zake” Mithali 16:9
Katika biblia tafasiri ya kiingereza [NIV] mithali 16:9 inasema, “Moyo wa mtu hupanga mipango yake ili kufikia malengo yake, lakini Bwana huongoza hatua zake” (Tafsiri ya mwandishi). Hii inatupa kufahamu kuwa jukumu la kupanga mipango ili kufikia malengo fulani katika maisha yetu ni jukumu la mtu binafsi. Mpaka tumekuwa na mipango dhabiti katika kufikia  malengo tuliyonayo, Mungu hataongoza hatua zetu ili kufikia malengo hayo.
Akielezea umuhimu wa kuwa na mipango, na jinsi ambavyo Mungu huongoza hatua zetu ili kufikia malengo, kutimia kwa ndoto/maono, katika maisha ya mtu; mwenyehekima mmoja amewahi kusema, “Ni vigumu kuongoza meli iliyosimama”. Mtu mwenye malengo au ndoto/maono katika maisha yake lakini hana mipango dhabiti ya kufikia jambo hilo, ni kama meli iliyosimama; hakuna namna nahodha ataweza kuiongoza meli hiyo; na hivyo hakuna namna meli hiyo itaweza kufika mwisho wa safari yake.
Jambo moja muhimu napenda ukumbuke; Kabla ya mipango hutangulia malengo. Malengo ni mambo unayotaka kuyafikia katika kipindi cha muda fulani; Mipango ni hatua na njia za kupita ili kufikia malengo hayo. Watu wengi wanashindwa kufanikiwa, si kwa sababu hawana uwezo wa kufanikiwa; ila ni kwa sababu hawajui wanataka kufanikiwa katika jambo gani hasa [specific targets]. Mtu asiye na malengo ni sawa na msafiri anaye safari kwenda mahali kusipojulikana. Mpaka umekuwa na malengo mahususi, hauwezi kuwa na mipango dhabiti ya kukutoa hapo ulipo.
Nakumbuka wakati ninaanza mwaka 2015, mojawapo ya malengo niliyokuwa nayo ni kuhakikisha ninasoma angalau kitabu kimoja kipya kila mwezi; na nikaweka mipango/mikakati ya kufikia lengo hilo. Mpaka mwaka unaisha nimefanikiwa kutimiza na kuvuka lengo hilo la kusoma angalau kitabu kipya kila mwezi; hii ni mbali na machapisho mbalimbali ninayosoma; ambapo kwa ujumla imeongeza maarifa, ufahamu, hekima na kupanua uelewa wangu juu ya mambo kadhaa.
Kumbuka jambo hili; Ili kuishi maisha yenye ufanisi, ni muhimu kwa malengo yako kuendana na ndoto zako au maono au kusudi la Mungu juu maisha yako.  Kama mojawapo ya  malengo yako katika mwaka huu ni kuongeza au kukuza uhusiano wako na Mungu, au kujijengea tabia na mwenendo fulani wa kimaisha au kurudi shule au kusoma hadi kufikia ngazi fulani, kuanzisha biashara/jambo fulani au kuboresha mahusiano yako katika eneo fulani; weka mipango ya kufikia lengo hilo.
Mipango ni kama malighafi za kutengenezea bidhaa [malengo], tunapoanza mwaka huu mpya amua kupanga mipango na kuiweka mipango hiyo mbele za Mungu; na mwisho wa yote utapata bidhaa kamili yaani kufikia malengo/ndoto na maono uliyonayo ndani yako kwa mwaka huu [Mithali 16:3].
Unapokuwa na malengo pamoja na mipango dhabiti; inakuwezesha kuweka vipaumbele vyako vizuri juu ya matumizi yako ya fedha, rasilimali ulizonazo, muda wako na aina ya watu unaotaka kutumia nao muda wako; kama mtu hakusaidii kufikia malengo yako ni vizuri ukapunguza matumizi ya muda wako kwake.
Kumbuka; watu wanaosafiri kwenda mahali kusikojulikana hupenda kusafiri pamoja na watu wengine; watu wasiotaka kufikia malengo yoyote katika maisha yao, hupenda kila mtu afanye kama wao.

0 comments :