Ongeza ufanisi ......

11:27:00 AM Unknown 0 Comments



ONGEZA UFANISI WAKO KUPITIA VIPAUMBELE
Uwezo wa mwanadamu unakikomo chake katika kila afanyalo. Ndio maana kuweka vipaumbele ni jambo la msingi. Nguvu za mwanadamu ni kidogo, hawezi kufanya vizuri kila kitu kwa wakati mmoja. Hawezi kuwekeza katika kila mradi. Hawezi kumfikia kila mtu. Kwa kuwa pesa tulizonazo ni kidogo, muda nao hautoshi na watu tulionao wanamajukumu mengi ndio maana tunahitaji kuweka vipaumbele.
Ni muhimu kuwa na kipaumbele katika wito na Kusudi tuliloitiwa na Mungu. Usain Bolt mkimbiaji kutoka Jamaika ni mmoja wa watu waliofanikiwa sana kwa sababu ya kujua kusudi na hivyo kuweka vipaumbele. Badala la kuwekeza katika mpira wa miguu na riadha baba yake alimtaka adumu katika riadha tu, yaani, achague moja. Alimsisitiza: “Usain my son you belong to the running tracks”
“Muda ni bidhaa pekee inayochacha haraka kupita mboga yoyote ile unayoifahamu. Muda ukipoa (ukipita) hakuna kuchemsha kama mboga, ni rasimali isiyorejesheka.”
Ni muhimu kuwa na vipaumbele katika mawasiliano, katika kazi, katika fedha na katika muda. Vipaumbele huamua kwa nani na kwa ukubwa gani rasilimali zako zitatumika. Kila alichonacho mwanadamu hakitoshi mpaka pale anapoamua kuwa na vipaumbele. Watu wote wana saa 24 lakini si wote wanatumia saa 24. Wengi wanatazama saa 24 zikienda, au wanawatazama wenzao jinsi wanavyotumia saa 24 za siku. Kila unapotazama filamu, unaposikiliza vituo vya redio lazima ujue, unamtazama mwenzako akifanya wakati wewe unapoteza muda. Muda ni bidhaa pekee inayochacha haraka kupita mboga yoyote ile unayoifahamu. Muda ukipoa (ukipita) hakuna kuchemsha kama mboga, ni rasimali isiyorejesheka. You cannot restore (recycle) time once wasted.
Kwa leo tunazungumzia sana pesa, ni muhimu tukajua vipaumbele vyetu vinavyohusiana na pesa kwa mujibu wa biblia. Mwana mpotevu alipochukua pesa hakuwa na vipaumbele, ila anasa tu. Biblia inasema, “akatapanya mali kwa maisha ya anasa.” Angeweza kutumia pesa zake kufungua makanisa, pia anagaweza kuziwekeza katika miradi ili ziongezeke, bali yeye akajitafutia makahaba akatapanya. Wengine wanatafuta pesa, wengine wanazo na hawajui kutumia.
Vifuatavyo ni vipaumbele vya pesa kibiblia:
Moja, Pesa ni kwa ajili ya chakula. Kila unaponunua chakula au unapowapa watu chakula unafanya matumizi mazuri, “Imenenwa wapeni watu chakula.” Mungu akitupa pesa anajua ametupatia kifurushi chenye chakula cha roho na mwili, maji, elimu, teknolojia, maarifa, uzima na msaada. Pesa na matolea lazima yapelekee uwepo wa neno la Mungu la kutosha katika makanisa na katika mikutano. Imenenwa, “Leteni zaka kamili ghalani ili chakula cha kutosha (neno la Mungu) kiwemo katika nyumba yangu, asema BWANA.” Nabii Isaya naye alinena kwa habari ya pesa na wapi itumiwe. Alitaka iende kwenye chakula kinachoshibisha. Mambo ya anasa huleta kiu zaidi (addiction) badala ya utoshelevu. Ndio maana si vizuri kununua pombe, sigara au kuwekeza katika zinaa. Kwani kutoa fedha kwa ajili ya kitu ambacho si chakula? Na mapato yenu kwa kitu kisichoshibisha?... ”Isaya 55:2a
“Tutoapo fungu la kumi la pesa au mazao, ni fungu la kumi la nguvu zetu zilizotumika kuzalisha kiwango hicho cha pesa. Mungu ndiye atupaye nguvu”
Pili, Pesa ni kwa ajili ya kumwabudu Mungu. Huwezi kuabudu pasipo sadaka. Imeandikwa, “Mheshimu BWANA kwa mali yako, Na kwa malimbuko ya mazao yako yote.” Mithali 3:9. Nilipokuwa mdogo nilipewa pesa ili nikatoe sadaka, wengi wetu tunapenda mtindo huu usio na baraka sana. Daudi alikataa vitu vya bure, alisema hawezi kwenda kutoa vya kupewa na akaamua kulipia gharama. Tutoapo fungu la kumi la pesa au mazao, ni fungu la kumi la nguvu zetu zilizotumika kuzalisha kiwango hicho cha pesa. Mungu ndiye atupaye nguvu. We need money for worship.
Tatu, Pesa ni kwa ajili ya kununua maarifa. Naam, kwa mapato yako yote jipatie ufahamu,” Mithali 4:7b. Ni kazi bure kuwa na pesa na ujinga. Kuwekeza katika elimu na maarifa ya kiroho ni jambo la msingi. Kama hununui vitabu, husomi vitabu; tena wala huwekezi katika elimu, kwa kweli bado hujaanza kuishi. Kama pesa haikuletei akili basi inakuletea ujinga, na hapa lazima uwe upande mmoja. Ama ujinga au maarifa. Kwa mjinga ni rahisi kutumia pesa kujiua, biblia inasema, “Kufanikiwa kwao wapumbavu (wasio na maarifa) kutawaangamiza.” Mithali 1:32b
Nne, Pesa ni kwa ajili ya kusaidia wengine. Huwezi kutoa usichokuwa nacho, kama hatuna pesa hata kama ni wakarimu tutaonekana wachoyo. BWANA Yesu alisema, “Ni heri zaidi kutoa kuliko kupokea.” Na hapa kuna pande mbili mtoaji na mpokeaji, Yesu amesema unaheri upande wa mtoaji kuliko ule wa mpokeaji. Mara zote mpokeaji ndiyo huamini amebarikiwa, anaweza hata kufanya maombi ya kushukuru. Lakini Yesu anasema mtoaji hubarikiwa zaidi, ukiweza kutoa unathibisha kwamba umebarikiwa. Rafiki unapenda kuwa upande gani? Nadhani sote tunapaswa kuwa upande wenye heri ambao ni wa kutoa au wa mtoaji. Basi na tutafute pesa kwa njia halali ili tuweze kutoa. “Usimwambie jirani yako, Nenda, urudi halafu, na kesho nitakupa; Nawe unacho kitu kile karibu nawe.”Mithali 3:28
“Mungu alijua akitupa akili hatutapungukiwa na chochote hata kama haturuki kwa mbawa. Tumia akili, acha ndege waruke mpaka shambani bali wewe ruka mpaka miaka 10 au 20 ijayo kupitia uwekezaji.”
Tano, Pesa ni kwa ajili ya uwekezaji. Kuwekeza katika hisa, katika kilimo, ardhi na biashara ni jambo la msingi na la muhimu. Katika biblia tunasikia kwa habari ya kabaila ambaye kwa lugha ya leo anaitwa, mwekezaji. Mwekezaji ni mtu anayetumia pesa leo ili imtumikie kesho. Anataka baada ya kitambo apate pesa bila kufanya kazi. Uwekezaji katika miradi ya muda mrefu ni uwezo wa kuona mahitaji ya kesho tukiwa leo. Uwekezaji huleta mategemeo na matumaini yenye uhakika kwamba, pesa itaingia (we expect cash to inflow). Ni tofauti na ndege ambao nao wana mfumo wao waliopewa na Mungu. Ndege hawana mashamba lakini wana mabawa ambayo huwarusha na kuwaingiza shambani, mwanadamu ana-akili ambayo ni zaidi ya mabawa. Mungu alijua akitupa akili hatutapungukiwa na chochote hata kama haturuki kwa mbawa. Tumia akili, acha ndege waruke mpaka shambani bali wewe ruka mpaka miaka 10 au 20 ijayo kupitia uwekezaji.  “Invest don’t plan spend and squander”
Kimsingi kila pesa yako inapotumika katika mambo haya matano haufanyi anasa. Nje ya haya inaweza kuwa anasa, japo si rahisi kukuandikia kila kitu. Huwezi kuwa mchoyo kama huna cha kutoa, ukiwa nacho na usipotoa ndipo huitwa mchoyo. Pesa si tu kwamba itafafanua vipaumbele vyako, bali pia itaifunua tabia yako ili ionekane dhahiri. Pesa ni, “amplifier” hukuza tabia ili ionekane wazi kwa watu. Mkarimu akiwa na pesa ataonekana sana, mchoyo akipata pesa ataonekana pia. Kule mtaani wanasema, “pata pesa tuijue tabia yako, kosa pesa tuijue tabia ya mkeo”
Tabia yawezwa kuchagizwa na pesa lakini bado msingi wa tabia njema ni Roho Mtakatifu. Tangu kale hata sasa Roho Mtakatifu amekuwa msingi wa matokeo mazuri ya kitabia ya wale wamwaminio Kristo. Tabia ni tunda, hukomaa na kuiva kwa kadiri watu wanavyodumu katika Kristo Yesu. Usikate tamaa, hakuna tunda linalo komaa kwa siku moja, yote hupitia mchakato wa kitambo kirefu. Naamini baada ya miaka kadhaa mwenendo wako utakuwa wa kumpendeza Mungu.  Hata Ibrahimu hakubadilika kwa siku moja, ilipita miaka kabla ya kuenenda kwa ukamilifu. “Lakini tunda la Roho ni upendo, furaha, amani, uvumilivu, utu wema, fadhili, uaminifu, upole, kiasi; juu ya mambo kama hayo hakuna sheria.” Wagalatia 5:22