Si kwa kazi wala si kwa matendo mema

2:28:00 PM Unknown 0 Comments



SI KWA KAZI WALA SI KWA MATENDO MEMA
Tumeokolewa bure

Biblia inanena wazi wazi kwamba, tumeokolewa kwa Neema kwa njia ya imani katika Yesu Kristo. Hakuna kazi inayoweza kutosha kumwokoa mwanadamu isipokuwa kazi ya msalaba tu, ni ile ambayo Kristo aliitenda. Kazi ya msalaba ni kazi timilifu hatuwezi kuchangia kitu. Iliyo kamili haihitaji kusaidiwa, Yesu alishasema imekwisha. Hakuna namna unavyoweza kuikamilisha iliyo kamili badala yake unapaswa kuamini tu. Kwa maana mmeokolewa kwa neema, kwa njia ya imani; ambayo hiyo haikutokana na nafsi zenu, ni kipawa cha Mungu; wala si kwa matendo, mtu awaye yote asije akajisifu.” Waefeso 2:8-9
“Utii wetu katika sheria za nchi unatufanya tuwe raia wema katika nchi na si raia wa Mbinguni. Tunaweza kupata uraia wa mbinguni tu kwa njia ya Imani katika Kristo Yesu.”

Matendo mema hayaokoi bali humthibitisha mwamini. Ni lazima tujue ukweli huu, raia mwema si raia wa mbinguni. Katika mataifa mbalimbali kuna raia wema, wanalipa kodi kwa wakati, hawavunji sheria, wananidhamu na wanaishi vizuri na jamii zao. Pamoja na wema wote na uzalendo wao, bado watakwenda motoni kama hawatamkubali Yesu kuwa BWANA na mwokozi. Utii wetu katika sheria za nchi unatufanya tuwe raia wema katika nchi na si raia wa Mbinguni. Tunaweza kupata uraia wa mbinguni tu kwa njia ya Imani katika Kristo Yesu.
Wako ambao kila siku huenda kuwatazama wagonjwa, wako ambao huenda gerezani kuwatazama wafungwa na wengine wengi huwalisha masikini. Matendo haya yote humthibitisha mwamini lakini kamwe hayataweza kuokoa. Biblia inasema, Bali wote waliompokea aliwapa uwezo wa kufanyika watoto wa Mungu, ndio wale waliaminio jina lake;” Yohana 1:12
Biblia inasema “bali wote waliompokea Yesu Kristo” haisemi wanaokwenda kanisani, haisemi wanaokwenda gerezani, haisemi wanaowalisha masikini, haisemi wenye nidhamu. Je, umempokea? Kumpokea ndio dili. Matendo yetu mema yataleta maana kama tayari tumekwisha kumpokea Kristo ndani yetu. Swala ni moja tu, Umempokea? Anakaa kwako? Ni rafiki yako? Je, wewe ni mtoto wa Mungu?
Hakuna msafi, hakuna mwenye haki yake, hakuna mwenye matendo yenye kuweza kuokoa. Si fulani tu ndiye mwenye dhambi hata wewe uu mdhambi na unamuhitaji YESU. Sote tu wagonjwa na tunamhitaji tabibu. Mungu alinena kwa kinywa cha nabii Isaya: “Kwa maana sisi sote tumekuwa kama mtu aliye mchafu, na matendo yetu yote ya haki yamekuwa kama nguo iliyotiwa unajisi; ” Isaya 64: 6a
“Inawezekana mtu ana matendo mazuri, inawezekana mtu ni mtaratibu inawezekana ni mfanyakazi katika shirika la kutoa misaada wa wahitaji, lakini pasipo kumpokea Yesu ataishia Jehenamu ya moto”

Watu wengi wanadhani wanaanza kuwa wenye dhambi pale wanapozini, wanapoiba au wanapowaza mabaya. Lakini mawazo yao si ya kweli sana. Mwanadamu kwa mara ya kwanza hawi mwenye dhambi kwa sababu ya uongo, mawazo mabaya au uchawi, bali ni kwa sababu Adamu wa kwanza alitenda dhambi [Warumi 3:23]. Hapa hata kabla hujatenda baya lolote unakuwa mwenye dhambi kwa sababu ya dhambi ya Adamu.  Ndivyo ilivyo, ndio maana ikanenwa kuwa, sote tumetenda dhambi. “Kwa sababu kama kwa kuasi kwake mtu mmoja watu wengi waliingizwa katika hali ya wenye dhambi, kadhalika kwa kutii kwake mmoja watu wengi wameingizwa katika hali ya wenye haki.”Warumi 5:19
Hali hiyo ya kuzaliwa wadhambi haiondoki mpaka pale mtu atakapompokea Yesu, hali hiyo ya dhambi haitamwacha mtu mpaka pale atakapobatizwa katika Kristo Yesu. Inawezekana mtu ana matendo mazuri, inawezekana mtu ni mtaratibu inawezekana ni mfanyakazi katika shirika la kutoa misaada wa wahitaji, lakini pasipo kumpokea Yesu ataishia Jehenamu ya moto. Wokovu ni zawadi, hauwezi kununua kwa matendo yako wala kwa fedha. “Lakini Petro akamwambia, Fedha yako (jitihada/bidii) na ipotelee mbali pamoja nawe, kwa kuwa umedhania ya kuwa karama ya Mungu yapatikana kwa mali.” Matendo 8:20
Rafiki yangu tangu kale hata sasa Yesu humwokoa mtu anayeliamini neno lake, anayekubali kwamba, hajampokea lakini anamuhitaji. Ikiwa unamuhitaji Yesu Kristo aje kwako kama BWANA na mwokozi sema sala hii kwa imani. “BWANA YESU KARIBU MOYONI MWANGU, MIMI NI MWENYE DHAMBI. TAFADHALI BWANA NIREHEMU NA UNIOKOE HIMA. AMEN”
Kwa sala hiyo fupi amekupokea na amekuja kwako, tafadhali mshukuru kwani ungeliweza kufa pasipo kufikiwa na ujumbe huu, kwa hakika hii ndio siku aliyoifanya BWANA nasi tunaifurahia na kuishangilia. Tuliokolewa na tuseme, fadhili zake ni za milele. Haleluyah! Glory Haleluyah.