Uvivu na Uuaji

2:30:00 PM Unknown 0 Comments

UVIVU NA UUAJI.
Maneno haya mawili si rahisi kuyatenganisha, ni kama chanda na pete. Uvivu una hasara kubwa sana na matokea yake ni uuaji. Utaua karama yako au kipaji chako, utaua mtaji na pengine utapoteza yale ambayo wengine waliyasumbukia kwa muda mrefu na walikupatia wewe uyaendeleze.
Uvivu haufanyi tu ukose yale unayoyatamani kuyapata bali unakupokonya hata lile dogo ulilonalo tayari. Muuzaji hodari atachukua wateja wa yule dhaifu na mvivu katika biashara. Kile usichokitunza huondoka na hii ni kanuni wazi. Kile usichokilinda kitaibwa hii haipingiki, ndio maana ikananenwa shika sana ulichonacho.
Nyakati za mfalme Sulemani katika maandiko, yuko mama aliyemlalia mtoto wake na kumuua kisha kugombea mtoto wa mwenzake. Alilala wakati wanawake wenzake hupumzika tu maana wanajua mtoto ni muhimu kwao kwa saa 24. Ni uzembe wa hali ya juu kusinzia hadi kuua mtoto uliyemsumbukia kwa muda mrefu (1Wafalme3:19). Inawezekana wewe na mimi tukiendelea kulala kuna vitu vitakufa. Rafiki yangu mmoja aliwahi kuniambia, “Alphonce, vijana hatulali tunapumzika tu” Ukipenda usingizi utaua ndoto zako na hatma yako.
Siku nyingine nikajifunza kuachana na neno sana. Nakushauri pia uondoe neno “sana” katika misamiati yako. Nimechoka sana, nimesoma sana, nimetembea sana ni sentensi zenye kuhalalishi na kutoa udhuru wa kutofanya kitu kinachotakiwa au cha ziada. Hii ni dalili ya uvivu, neno sana lazima liondoke. Aliyechoka sana atatamani kulala sana lakini aliyechoka atatamani kupumzika na kurejea tena ulingoni. “So avoid using the word ‘very’ because it’s lazy
Mwingine anaweza kuwaza, Uvivu ni nini? Ni ile hali ya kughairisha mambo. Nitafanya jioni, nitafanya kesho na hatimaye nitafanya mwakani. Uvivu pia ni hali ya kushindwa kuzingatia jambo moja, ni kuitawanya akili katika mambo mengi ambayo pengine si ya msingi. Uvivu pia ni ule uoga unakuja wakati wa kupanga mipango mikubwa na migumu na hivyo mtu kwa kujihurumia anajipangia mipango midogo na ya kawaida sana. Mvivu anakubali huondoka mapema hata kama kazi haijaisha, kamwe hapambani mpaka mwisho.  Kwa hiyo uvivu ni ile hali ya kuishia njiani.
Inawezekana umepoteza fursa nyingi na sasa huna cha kushika. Lile neno shika sana ulichonacho halina tena nguvu kwako maana huna cha kushika. Usiogope, Yesu Kristo aliye ufufuo na uzima na kweli anaouwezo wa kufufua yaliyokufa. Yeye alimwita Lazaro aliyekufa na akatoka mzima. Kwake huyu Mungu mwenye nguvu, na Mfalme wa ajabu twaweza kuomba, Ee Bwana fufua kazi zako ndani yetu.
Amka sasa uangaze….


0 comments :