Siachi

11:13:00 PM Unknown 0 Comments

 
SIACHI
(Dhambi ni kutelekeza kipaji chako)
“If you can’t walk then crawl. But whatever you do you have to keep moving Forward'” Martin Luther King Jr.
Katika siku za karibuni tumeshuhudia migomo ya watu wenye taaluma na vipaji mbalimbali. Kumekuwa na migomo ya walimu, madereva, madaktari na watu wa kada na tasnia nyingine tofauti tofauti. Migomo hii hulenga kuifanya jamii na serikali itambue mahitaji ya makundi haya kipekee, hususani tafsiri ya uwiano wa mchango wao kwa jamii na mishahara wanayolipwa.
Katika migomo yote, mgomo wa madaktari hutikisa zaidi, madhara yake ni dhahiri machoni pa wote. Watu hupoteza maisha, wagonjwa huteseka na ndugu zao hupoteza matumaini. Kama ilivyo kwa madaktari, yako madhara kwa kila mwenye kipaji ambaye ataacha kukitumia. Waathirika ni wale ambao Mungu alitaka wanufaike kwa kipaji chako. Ni wazi hakuna mto unaokunywa maji yake wenyewe. Yako madhara kama viongozi watajiuzulu bila msingi, yako madhara kama wahubiri watasimama na kuacha kuhubiri. Yesu alisema, atazamaye nyuma hafai kwa ufalme wake.
Dereva mwenye hekima akikimbia nafasi yake atafanya madereva walevi wapate ajira na kisha kuua watu kwa ajali isiyo na sababu. Kwa sababu ya wenye hekima kuogopa siasa, nchi zimeongozwa na mabaradhuli. Mchungaji akiacha kuombea kondoo shetani anawatafuna. Kuacha wajibu wetu ni dhambi, Samweli akasema, siachi…… 1Sam 12:23
Wizi, uzinzi, ulevi na uasherati si dhambi kubwa ukilinganisha na mhandisi kuacha kazi aliyoitiwa na Mungu. Dhambi kubwa ni mwimbaji wa kusifu na kuabudi kuacha huduma yake, mhubiri kuacha kuhubiri, kiongozi kuacha kuongoza.
Wewe kama ni ndege jielekeze katika kuruka na si kuogelea. Ni kwa faida yako, ukitaka kujua madhara ya kutokutumia kipaji chako jifunze katika vipaji ambavyo madhara yake yako nje kama vile udaktari au udereva, ambapo kosa moja hugharimu pumzi za watu.
Paulo alisema, “Ole wangu nisipo ihubiri injili”. Usipofanyia kazi kipaji ulichopewa na Mungu unafanya dunia iwe kama kibogoyo, maana pengo lako halitazibika. Uzuri wa dunia ni pamoja na mchango wa kipaji chako.
Jaribu kufikiri familia yenu bila ya wewe, kanisa lenu bila ya wewe, kazini kwako bila ya wewe kuwepo  kama hakuna pengo lolote katika kutokuwepo kwako ujue wazi hautumii kipaji chako. Imagine the World without Jesus Christ!
Mimi siachi kuhubiri, siachi kuimba, siachi siasa safi, siachi ufundi, siachi sanaa, siachi nasema siacha ubunifu wangu. Usiache karama yako ya maombi (1Sam 12:23); usiache biashara yako wala usidharau mwanzo wako mdogo, wala usipuuze wazo lako la ushindi. Kuendelea mbele inapaswa kuwa kama wimbo wako. Mungu Baba na akuimarishe katika kipaji na wito wako ulioitiwa, ukawe hodari; kama jua lisivyo acha kuangaza na wewe kwa kupitia kipaji chako ukaangaze milele kwa jina la Yesu Kristo. Amen
Kileleni ndipo tunapopatikana.

0 comments :

Unataka kufanikiwa katika nini - III

7:15:00 PM Unknown 0 Comments

 
UNATAKA KUFANIKIWA KATIKA NINI - III
 “Success is predictable, so is the failure”
Unatumiaje muda wako wa ziada?
Moja ya jambo kuu linalotofautisha kati ya mtu aliyefanikiwa na watu wengine, ni namna wanavyotumia muda wao wa ziada. Mwenye hekima mmoja amewahi kusema, namna unavyotumia muda wako leo ndio uamua hatima yako ya kesho. Nioneshe unavyotumia muda wako wa siku, nikueleze hatima yako. Wote tuna masaa 24, wote tunamahitaji ya msingi yanayohitaji muda mfano. Kulala, kula, kusoma (darasani kwa mwanafunzi), kufanya kazi n.k, lakini swali langu la msingi kwako ni je unatumaije muda wako wa ziada?
Muda ni kitu cha ajabu sana, ukichagua kuutumia vizuri au kutoutumia kabisa, bado muda utapita. Ukiamua kulala siku nzima, muda hautasimama, chochote utakachoamua kufanya bado muda utapita; ukiamua kukaa tu bila kufanya chochote bado muda utapita; hata ukiamua kuvunja saa bado muda utapita. Hivyo ni muhimu kuzingatia namna tunavyotumia muda wetu. Kumbuka hauwezi kuhifadhi muda kwa ajili ya matumizi ya baadae.
Leo nitagusia aina mbili za watu linapokuja swala la muda; kuna watu wanaopoteza muda na kuna watu wanaowekeza muda. Hivyo kila muda unaopita katika maisha yako, unakuwa umewekezwa au umepotezwa. Kitu kinachoamua kama umepoteza au umewekeza muda wako ni namna unavyoutumia muda huo. Katika mahojiano yake na jarida maarufu la nchini Marekani, Dr. David Oyedepo aliulizwa, unatumiaje muda wako wa ziada, akajibu “I use my time to read and think” yaani natumia muda wangu kusoma na kutafakari (personal development). Wewe na mimi tunatumiaje muda wa ziada?
Mfano; Ukisafiri umbali mrefu unafanya nini, unalala muda wote mpaka unafika? Unaangalia filamu na muziki wanaokuwekea mpaka unafika?!!!! Kwanini usibebe kitabu uwe unasoma wakati wengine wamelala? Kwanini usiweke mafundisho ya sauti kwenye simu yako ukiwa na spika za masikioni (earphones) wakati wengine wanasikiliza bolingo? Nina uhakika mpaka unafika mwisho wa safari yako utakuwa umemaliza sura mbili hadi nne za kitabu; na hapo tunasema umewekeza muda wako.
Au ukiwa kwenye foleni za mjini na umepata kiti cha kukaa, unafanya nini? Unalalamika kuhusu foleni mpaka unafika? Unachati mpaka unafika? Unalala? Au unatumia muda huo kujifunza ili uwe bora zaidi katika eneo unalotaka ufanikiwe? Embu tufikiri pamoja, mtu anayekaa kwenye foleni saa moja au mawili au zaidi kwa siku na kuishia kulalamikia foleni na serikali au kuchati, na mtu mwingine anatumia muda huo kujifunza (kitabu au mafundisho ya sauti kwenye CD kwa gari binafsi) namna ya kuwekeza katika biashara au ujasilimali au uwekezaji jambo lolote hata familia, huduma au kazini; unafikiri baada ya mwezi mmoja watu hawa watakuwa sawa kifikra? Baada ya miezi sita watakuwa sawa kimaisha? Au ukiwa nyumbani unatumiaje muda wako?  Kumbuka: Nioneshe unavyotumia muda wako, nikuoneshe hatima yako…. Wito wangu kwako leo ni kwamba, Anza kuangalia namna unavyotumia muda wako; tumia muda wako kuwekeza katika kuongeza ubora kwako binafsi (personal development) au kuongeza ubora katika eneo unalotaka kuona mabadiliko na mafanikio.
There’s a place at the top

0 comments :

Je hamkusoma?

2:24:00 PM Unknown 0 Comments

 
JE, HAMKUSOMA?
(Mathayo 19:4-6)
Matatizo mengi katika maisha ya mwanadamu ni matokeo ya semina alizokataa kwenda na vitabu alivyokataa kusoma. Askofu David Oyadepo anasema, “Kabla hujaoa au kuolewa jitahidi angalau (at least) usome vitabu (50) hamsini kuhusu mambo ya mahusiano na ndoa”. Ni wachungaji wachache wako tayari kuusema ukweli huu mchungu, matatizo ya ndoa ni matatizo ya maarifa.
Kuna nyakati mchungaji wetu mkuu yaani, Yesu Kristo alihojiwa kuhusu matatizo ya ndoa, naye bila kumumunya maneno alisema, ni matatizo ya kutokusoma. Aliwajibu akawaambia, “….Hamkusoma ya kwamba….” Mathayo 19:4
Wangesoma wangejua. Atakachofanya shetani si kukuzuia usiolewe, bali atakuzuia usisome. Mafundisho ya wiki mbili, mwezi mmoja au mwaka mmoja hayawezi kusaidia, ni lazima usome. Talaka, ugomvi, watoto wa mtaani na jamii zisizo na maadili zote zinasababishwa na jambo moja, ukosefu wa maarifa. Nikiwa chuo kikuu mzumbe nilimweleza rafiki mmoja, kama hauko tayari kusoma hauko tayari kuishi.
Sasa unaweza ukaelewa kwa nini watu wana wake wengi, sasa unaweza ukaelewa kwa nini watu wana waume wengi, sasa unaweza ukaelewa kwa nini makanisa ya leo yameanza kuongeza muda wa mafundisho. Ni kwa sababu ya ukosefu wa maarifa, hawakusoma!
Hakuna familia bila msamaha, hakuna ustawi kama familia itakuwa kipaumbele cha pili. Kuna ndoa za kibudha, ziko za ki-mila, na ziko za kiserikali. Kila hiyo inakanuni na taratibu zake, lakini ni zile zinazofungwa kwa mtazamo wa falsafa ya Yesu Kristo ndizo zitakazo weza kuleta maana kwa dunia hii. Ni familia hizo ndizo zitaleta ufalme, watoto watakao mtisha shetani badala ya kumwogopa, watoto watakao tumia ustadi na akili zao kwa maendeleo ya kudumu ya jamii zao. Si tu kwamba umezaa mtoto bali umemzalia nani, Mungu au shetani, mbingu au Jehanamu?
Bila ya mama, ni bila ya upendo; na bila ya baba, ni bila ya ulinzi, vyote havikuachi salama. Nimewasikiliza wachungaji zaidi ya 8 katika jambo hilo wote wanasema mambo haya kwa pamoja; 1. Uzuri au utanashati unadanganya bali chagua mtu amchaye BWANA, 2. Usioe kabla hujajua makusudi ya kuumbwa kwako, 3. Kazi kwanza ndoa baadaye yaani, usiolewe na mtu asiyejituma kufanya kazi hata ndogo ndogo, 4. Usioe nje ya kanisa, zamani watu walirudi kwao sasa hivi ni kanisani yaani, mtu aliyemwamini Kristo na kuokoka, 5. Usiwe na haraka, “don’t rush”, 6. Usipuuze ushauri wa jamii kuhusa ushuhuda wa huyo mtu, 7. Fuata sifa ulizojiwekea na si umbo na muonekano, review your checklist, 8. Oa chagua la Mungu na si chagua lako.
Nilisikia kwa Benny Hinn na Sunday Adelaja wakisema, “Mary God’s choice and not your choice” yaani “uungane na mtu ambaye Mungu amekuchagulia na si ambaye wewe umemchagua”. Hii hupelekea mtu kuomba sana na kusoma sana. Katika maombi Mungu atakuongoza, na katika neno Mungu atakuangazia, kwa kuwa neno ni taa. Taa ikiangaza ni rahisi kuona na kuwa na hakika na salama.
Kwa muhtasari, soma kabla ya kuingia katika uhusiano, lijue kusudi la kuumbwa kwako kabla ya kuingia kwenye uhusiano. Unaweza pia kuagiza kitabu cha, “Si kwa tamaa, bali kwa upendo” ni kizuri na kinapatikana kwa namba zetu. Barikiwa….

0 comments :

Namna bora ya kutumia ....

2:15:00 PM Unknown 0 Comments

NAMNA BORA YA KUTUMIA KIPAJI CHAKO.
(Appropriate your gift)
Kila kitu kizuri tunajua kinatoka kwa BWANA, Mungu anatenda kazi katika kuwaza na kufikiri kwetu. Ni Mungu atupaye mawazo. Wengi wamezoea kumshirikisha Mungu katika hatua ya utekelezaji, hawajazoea kumshirikisha Mungu katika msingi wa mawazo yao, ambayo ndio hatua ya awali kabisa. Daudi aliomba akisema, “Mawazo ya moyo wangu yapate kibali mbele zako” alitaka Mungu ahusike na mawazo yake.
Vipaji vyetu na taaluma zetu si tunda la akili zetu (it is not our brain child) ni zawadi kutoka juu. Kila kitu kizuri ni zawadi kutoka juu. ...kila kitolewacho kilicho kamili, hutoka juu, hushuka kwa Baba wa mianga.” Yakobo 1:17
Je! Una kipaji? Wewe ni mwanaridha, mtunga mashairi, fundi sanifu, mcheza mpira au mpigaji wa vyombo vya muziki. Vyote hivyo ni vipaji au karama kutoka kwa Mungu tunazopaswa kuzitumia kwa manufaa ya watu wote.
Je, wewe ni mtaalamu? Wewe ni mtawala (manager), wewe ni askari wa barabani, wewe ni mhasibu, wewe ni mgavi au mwalimu, zote ni fani ambazo zinapaswa kutumika kwa maslahi ya watu wote (For common good) wala si kwa maslahi yako binafsi. Ameonya msanii mmoja akisisema, “una mashavu makubwa paka pori, lakini umeshiba vya anasa”.
Hakuna mto unaokunywa maji yake wenyewe, hakuna jua linalojiangaza lenyewe vivyo hivyo hupaswi, kuiba au kujinuifaisha wewe tu. Ukiwa mhasibu kusanya na kuwasilisha ili baadaye kilichopatikana kiwafae watu wote. Ukiwa mchezaji wa timu usicheze ili tu kuonekana peke yako, cheza ili timu yote ifanikiwe na kushinda kama timu.
Mungu ametupa vipaji, karama kama nyezo za kuwatumikia wenzetu ili Mungu atukuzwe. Tunatakiwa kuwa waaminifu na watu wasio na ubinafsi (selfless) ili karama na uwezo tuliopewa na Mungu umnufaishe kila mtu. Uwezo wa Nelson Mandela umenufaisha wengi huko Afrika ya Kusini. Uwezo wa Yesu Kristo umeleta wokovu na kuhesabiwa haki kwa kila kiumbe.
Baba mbinafsi hula kitimoto na kuku choma mtaani na kuacha mihogo nyumbani, lakini baba mwaminifu yeye hupeleka kitoweo nyumbani akale pamoja na watoto na mke wake. Ni kwa namna hii karama zetu zinapaswa kutumika kumfaidia kila mmoja wetu katika familia ya Mungu. Ukiwa mwaminifu kwa kuyalinda mapato na maslahi ya ofisi yako basi kwa njia hiyo utakuwa umemsaidia kila atakayelipwa mshahara halali na ofisi hiyo.
Ukiwa na kipaji basi safari zinakuhusu, kila siku ni lazima uwaendee wale wanaotakiwa kunufaika kwa kupitia kipaji chako. Daktari aende kwa wagonjwa, mwalimu aende kwa wanafunzi, mfanyabiashara asipange bei yenye kumwonea mteja kwa lengo la kupata faida kubwa.
Kila siku Yesu alikuwa safarini akiwaendea wale alioitwa kwa ajili yao, alikwenda Samaria, Galilaya na katika miji na vitongoji vingi kuwaendea wanaomuhusu. Mwanadamu ni kiumbe wa safari na mizunguko, si rahisi kufika juu katika kilele cha mafanikio yako ikiwa utatulia sehemu moja. Mabadiliko ya kijiografia na maeneo yanabaraka zake. Ibrahimu, Yakobo, Musa na Yusufu wote walikuwa ni watu wa safari, walitii sauti ya Mungu, walihakikisha wanapatikana katika eneo wanalotakiwa kwa wakati. Walikuwa ni watu kwa ajili ya watu, kwa Ibrahimu sote tumepokea Baraka. Mimi na wewe tu baraka, kwa ajili ya mataifa kama ilivyokuwa kwa baba yetu Ibrahimu.
We are the blessings!!!


0 comments :

Unataka kufanikiwa katika nini - II?

9:30:00 AM Unknown 0 Comments

UNATAKA KUFANIKIWA KATIKA NINI - II?
“Success is predictable, so is the failure”
Kiwango cha mafanikio ya mtu katike eneo lolote hutegemea kiwango chake cha maarifa sahihi, ufahamu na utendaji kazi wa kanuni zinazoleta mafanikio katika eneo hilo. Toleo la kwanza katika mfululizo huu tuliangalia kanuni/ mambo mawili; Na leo nataka tuangalie mambo mengine mawili:
a.    Je, unaona au unaliona (ndani yako) jambo hilo unalotaka kufanikiwa au kufanikisha (Do you see it)?
Mpaka umeliona jambo hilo waziwazi ndani yako, hautaweza kulimiliki/ kulifanya kuwa dhahiri. Kwa kadri unavyoona ndivyo unavyoongeza eneo la umiliki wako yaani uwezekano wa kulifanikisha jambo hilo au kufanikiwa katika eneo hilo. “Maana nchi hii yote uionayo, nitakupa wewe na uzao wako hata milele”. Kipimo cha Ibrahimu hakikuwa kwa Mungu aliyeahidi, kilikuwa katika uwezo wa macho yake kuona. Mungu hakumuwekea mipaka; mipaka iliwekwa na macho yake. “Inua macho yako ukatazame kutoka hapo ulipo”. (Mwanzo 13:14-15, 17)
Ukitazama kutoka hapo ulipo (ambapo unachotamani na kutaka kufanikisha kipo kama wazo tu kwenye maandishi/mchoro) unaiona hiyo nchi? Je unajua ya kuwa unajua ya kuwa unaweza kufanikiwa au kufanikisha jambo hilo uliloliandika? Kuandika ni jambo moja, na kujua ndani yako kuwa unaweza (confidence) kufanikiwa/kufanikisha ni jambo lingine. Kumbuka, tunapewa au tunapata kile tunachokiona. Habakuki aliambia, “Ukaifanye kuwa wazi sana…” Mpaka macho yako yameona (wazi wazi) kwanza, hautaweza kumiliki kikamilifu. Kwa kadri unavyoona vizuri ndivyo unavyoweza kutembea kwa kasi kufikia mafanikio yako (The more clearer you can see it, the greater the speed of delivery).
Warren Baffett, anasema kabla hajawa tajiri aliona (he saw it clearly) atakuwa tajiri, wala hakuwa na shaka hata dakika moja. “I always knew I was going to be rich. I don’t think I ever doubted it for a minute.” –(“Siku zote nilijua kuwa, nitakuwa tajiri. Sidhani kama nimewahi kuwa na mashaka juu ya hilo (ndani yangu) hata kwa dakika moja”: Tafasiri isiyo rasmi). Mwanadada Emma Wenani anasema, “Deep down, I always knew I would be successful” (“Ndani kabisa ya moyo wangu, nilikuwa najua nitafanikiwa”: Tafasiri isiyo rasmi). Ndani ya moyo wako unaona nini? Unachoona ni muhimu sana, kwa sababu kinaweza kukukwamisha au kukufanikisha.
b.   Tafuta maarifa, elimu na ufahamu wa ‘kutosha kuanza’ jambo hilo/ kuhusu eneo
Kabla ya kuanza jambo lolote lenye maana, ni muhimu kuwekeza katika kupata maarifa sahihi na ufahamu wa kutosha kukusaidia kuanza. Kiwango chako cha mafanikio katika eneo lolote hutegemea kiwango chako cha maarifa na ufahamu uliona nao kuhusu eneo/jambo hilo; iwe kiroho, kimwili, kifedha au kiuchumi, familia, huduma, mradi, uwekezaji n.k. Unapopata maarifa sahihi ya kukuwezesha kuanza matokeo huwa dhahiri. Mfano. Usianze mahusiano, au ndoa, biashara, kilimo, mradi au uwekezaji wowote ule kama huna maaarifa sahihi na ufahamu wa kukusaidia kuanza vyema; Don’t start blindly. Hili litakuepusha na  msongo wa mawazo (stresses and depressions) pamoja na gharama nyingine nyingi sana kama vile muda, fedha n.k. Ukianza bila kuwa na maarifa na ufahamu wa kutosha uwe na uhakika jambo hilo halifiki mbali au litakugharimu sana. Kumbuka, Mpaka akili imetoka jasho, hautaweza kuona wepesi (Until your brain sweat; you won’t experience swiftness).
Japo kujifunza ni jambo endelevu, lakini ni muhimu kuhakikisha kabla ya kuanza jambo lolote unapata maarifa yaliyo sahihi yatakayokusaidia kuanza vyema. Unataka kuona wepesi katika ndoa, uhusiano, huduma, biashara, kilimo, mradi au uwekezaji wowote ule? “Yale uliyoyaona kwa macho, usitoke nje kwa haraka ili kuyashindania; usije ukakosa kujua la kutenda hatimaye...” (Mithali 25:7c-8)
There’s a place for you at the top!

0 comments :