Mfumo wa zawadi

10:23:00 AM Unknown 0 Comments

 
MFUMO WA ZAWADI.
(Nitapata nini? Mathayo 19:27)
Mwanadamu anafanya kazi kwa mfumo wa zawadi (Reward system). Wana raha sana wanaotumia mfumo huu ambao Mungu pia huutumia. Unapopanga malengo yako usisahau kujipa zawadi. Usisubiri watu watambue juhudi zako, wewe pia jitambue na jipongeze. Ikiwa nitafikia lengo fulani nitasafiri wakati wa majira ya joto kwenda mapumziko. Nikifanya kazi kwa bidii na kuzalisha vya kutosha nitakwenda kutembea hifadhi za taifa.
Mfumo huu ni mzuri hata kwa mahusiano ya wazazi na watoto. Ukimaliza kazi ya nyumbani nitakuruhusu utazame sinema, ukimaliza chakula nitakupeleka zuu (zoo) ukatazame wanyama. Mfumo huu unachagiza kutimia kwa malengo. Unamfanya mtu apende utendaji wake.
Wataalamu wengi wa sayansi na saikolojia wanaamini wazi kwamba, kuna furaha na nguvu mpya anayoipata mtu akiwa atapata motisha, atapandishwa cheo, atapongezwa au kufarijiwa kwa kazi yake njema. Si rahisi mtu kufanyakazi kwa bidii na ufanisi ikiwa anajua hatapata chochote kama taji, kutambuliwa na kukubalika, kupandishwa ngazi au kupewa fedha. Usiweke malengo bila zawadi, usijitaabishe bila ya kujiahidi furaha.
Akili ya mwanadamu hufikiri kwa picha, anapofanya kazi picha ya motisha au zawadi tarajiwa huwa akilini mwake. Kufanya kazi bila kujua utakacho pata huleta uchovu. Inatia moyo kufanya kazi ambayo matokeo yake ni dhahiri. Wanadamu wanapenda kujua watakachopata, Petro alimuuliza Yesu, “Ndipo Petro akajibu, akamwambia, Tazama, sisi tumeacha vyote tukakufuata; tutapata nini basi?” Mathayo 19:27
Wakati mwingine si rahisi kuwalipa watu kwa fedha lakini tunaweza kutambua mchango wao na kuukubali. Na si wakati wote mtu anastahili kupata malipo chanya wakati mwingine anapaswa kupewa adhabu. Kanani kwa watii na Misri kwa wasiotii. Usijipongeze kwa kurudi nyuma, usile kwa anasa siku ambayo biashara yako haijazalisha faida. Jipongeze pale tu unapoona unastahili, wakati mwingine jipe adhabu ili utimize lengo. Haifai kuvuna tusipopanda. Reward for compliance and punishment for failure.
Baada ya kazi ngumu ni vema kujipa pumziko kama zawadi, ni vizuri kubarizi kando ya mito na bahari ili kuipa akili uwezo wa kuunganika na asili ya dunia. Mungu hutoa kazi na motisha, ni ajabu sisi tunasahau. Alipoamuru kutii alisema tutakula mema ya nchi, alipoamuru utoaji aliahidi Baraka hata pasipokuwepo nyumba yenye ukubwa wa kuchukua Baraka hizo.
Nikiwa Tabora mwaka 2013 na 2014 nilijifunza jambo la msingi kutoka kwa Michael Mambo, rafiki yangu huyu anayemiliki shule alikuwa akitoa kiasi fulani cha pesa katikakati ya mwezi (mid Month) kiasi hiki kilikuwa kikitoa motisha kubwa kwa walimu kwani hakikuwa sehemu ya mshahara wala hakikuwa sehemu ya mkataba bali ilikuwa ni motisha tu kwa watumishi. Wengi walijisikia kuhuishwa na kupata nguvu ya kazi baada ya kupata kiasi hiki. (Mid month package)
Jiahidi zawadi, itakupa hari na hamasa ya kutimiza malengo yako uliyoyaandika. Endelea kubakia kileleni.
Waunganishe rafiki zako katika mpango huu kwa kututumia email zao au kwa kuwaomba watembelee blog yetu na kujiunga. www.lifeminusregret.blogspot.com

0 comments :