Malezi ni mkataba mrefu

12:50:00 PM Unknown 0 Comments

 
MALEZI NI MKATABA MREFU.
(Ni zaidi ya miaka 18)
Mwanadamu ni kiumbe anayekaa katika utegemezi kwa muda kuliko watoto wa viumbe wengine. Viumbe wengine hulea watoto wao kwa miezi sita au mwaka mmoja na kisha huwaacha wakaendelee na maisha yao.
Ndege hukaa na makinda yao kwa miezi mitatu, wako wanyama wengine hukaa na watoto wao kwa kipindi ambacho ni chini ya mwaka mmoja. Lakini sivyo ilivyo kwa binadamu. Malezi ya mtoto ili mtu awe mtu kamili yanachukua zaidi ya miaka 18. Fikra za kupata mtoto lazima ziende mbele angalau kwa miongo miwili (miaka 20). Mtoto wa binadamu anakaa nyumbani kwa zaidi ya miaka 18 akiwa bado ni tegemezi. Wako wenye miaka zaidi ya 30 na wanalishwa na kutunzwa na wazazi wao. Malezi ni zaidi ya chakula na dawa. Ni kuadabisha na kufundisha utu wema. Mith 21:6
Mkataba wa kupata mtoto hautakiwi kuwa wa usiku mmoja, mkataba wa kupata mtoto unapaswa kuwa mkataba unahusishwa elimu, utu, makuzi, na hatma ya mtoto kwa mioungo isiyopungua miwili. Uamuzi wa kupata mtoto ni lazima uwe ni mkataba wa milele, au uwe mkataba wa zaidi ya miaka 18. Wenye utayari wa kupata mtoto lazima wawe na utayari wa malezi ya pamoja kwa zaidi ya miaka kumi na nane. Kifo ndio sababu rasmi sana ya kibiblia ya kumfanya mtu alelewe na mzazi mmoja, japo kijamii ziko sababu nyingi.
Pamoja na changamoto zote za malezi, mzazi mmoja au wawili bado kulea ni kuzuri kunampa mzazi au mlezi nafasi ya kukijenga kizazi kinachofuata. Katika ujenzi wa Taifa, familia ni sehemu ya kwanza na ya msingi.  Shule ya familia inatajwa kuwafanikisha wengi kuliko vyuo vikuu.
Shule ya familia ikikosewa inaweza kuwafelisha wengi kuliko wanaofeli katika madaraja mbali mbali ya elimu. Familia isipowajenga watoto kwamba matatizo yapo, basi watakapo kutana nayo watakata tamaa. Familia isipoamini katika uwepo na uhusiano na Mungu, basi watoto wataabudu vitu ambavyo kwa asili si Mungu.
Watoto wasiojengwa katika ibada wanaweza wasimwabudu shetani badala yake wakaabudu kazi, fedha, sinema na michezo. Rafiki yangu alipenda ibada kiasi kwamba alikuwa hakumbuki ni lini hakuudhuria ibada kanisani, lakini tunao vijana wengi ambao hawakumbuki ni lini walikwenda kanisani. Makosa haya ni ya mfumo wa malezi.  
Malezi ni jambo la pamoja mzazi hatoshi peke yake wala hapaswi kufikiri kwamba anatosha. Ndio maana Mungu amwetuwekea kanisa. Kanisa ni jumuiya ya waaminio ambapo ndani yake kuna walimu, wainjilisti, wachungaji, mitume, manabii na watu wenye matendo ya miujiza. Mtoto ni wa Mungu kwanza, wa wazazi na baadaye wa jamii yote.
Hitler kabla ya kuwa muaji alikuwa mtoto, Iddi Amini wa Uganda kabla ya kuwa dikteta alikuwa mtoto. Mtoto ni kama karatasi nyeupe isiyo na kitu chochote, mwandishi wa awali ni Mungu na baadaye wazazi wanapata nafasi ya kuandika upendo au ugaidi, amani au chuki, uvumilivu au kisasi.  Mithali 21:6

0 comments :