Tazama zaidi ya uonanyo

11:14:00 AM Unknown 0 Comments


TAZAMA ZAIDI YA UONAVYO

Watu wanapokutana na ukinzani/changamoto  katika jambo, mambo mawili huweza kutokea; kukosa nguvu na  ujasiri wa kuendelea mbele hadi kupata mpenyo,  au kukosa  uvumili na hivyo kutafuta njia mbadala hata kama si salama ili kufikia tamanio lake. Mtu wa namna hii huona changamoto kama mwisho au kikwazo cha kufikia mafanikio yake. Mfalme Sauli alipokutana na Goliath, yeye na Israeli yote isipokuwa Daudi walikosa nguvu na ujasiri wa kuendelea mbele [1Sam 17:11]; wakati Ibrahimu alipokutana na changamoto ya kupata mtoto, aliingia kwa mfanyakazi wake kama njia mbadala ili kufikia matamanio yake, na gharama yake ilikuwa kubwa. 

Robert H. Schuller, mwandishi wa kitabu cha “Tough times never last but tough people do”, anasema “Tofauti ya mtu anayeshinda na mtu anaishindwa katika changamoto [hiyo hiyo] wanayokutana nayo wote wawili au mazingira hayo hayo, ni namna ambavyo watu hao wamechagua kulitazama jambo hilo [Tafasiri ya mwandishi]”. Hivyo kumbe, namna ambavyo mtu anatazama au kuchagua kuona jambo au changamoto iliyopo mbele yake ndio huamua hatima ya mtu huyo katika jambo hilo; yaani kushinda au kushindwa kwake. [The ability to see beyond the situation is the key to overcome the challenge/crisis].

Musa alipokuta na vikwazo katika kuwakomboa wana wa Israeli kutoka katika utumwa wa Misri; hakuona kama tatizo la kumrudisha nyumba, bali aliona nafasi kwa yeye kuona Nguvu na Udhihirisho wa Mungu katika maisha yake na wana wa Israeli. Ndio maana kila alipokutana na tatizo au changamoto alikimbilia mbele za Mungu, kwa kuwa alijua ilikuwa ni fursa kwake ya kuona Ukuu wa Mungu; na kupitia ugumu wa Farao, Mungu atukuzwe na watu wote wapate kujua kuwa Mungu Anaishi.  Leo hii anajulikana kama mshindi [Kutoka 9:11, 29].

Wakati kila mtu anamuona Goliath kama tatizo katika Israeli, Daudi alimuona Goliath kama fursa ya kudhiirisha Ukuu na uweza wa Mungu; na ili dunia wapate kujua yuko Mungu katika Israeli. Lakini pia kwake, aliona kama fursa kwa yeye kuoa mtoto wa Mfalme bila kutoa mahari na mwanzo wa kuishi maisha bora, pia fursa kwa yeye pamoja na familia yake kuishi huru [1Sam 17:25, 46-47]. Leo hii anajulikana kama mshindi.

Mama Teresa wa Calcutta, mshindi wa tuzo ya amani ya Nobel alipoona maskini na watu wasio na msaada kule India; hakuona kama tatizo la kumkatisha tamaa, bali aliona fursa ya kumtumikia Mungu kwa kugusa maisha ya watu. Leo hii anajulikana kama mshindi.

Nimewahi kusikia habari za mama mmoja ambaye alikuwa amempa Yesu maisha yake; na alikuwa anafanyakazi katika kampuni fulani, lakini baada ya muda aliachishwa kazi; akaenda kwa mchungaji wake analia, mchugaji wake akamuuliza kwanini alikuwa analia!!!? Akamuuliza, “Je una kitu gani ambacho unaweza kufanya?” Yule mama akamjibu kuwa anaweza kutengeneza keki tu. Baada ya mazungumzo na mchungaji wake; akamuambia aende akatengeneze keki kisha apelekee pale alipoachishwa na kuwagawia wafanyakazi wenzie bure kama sehemu ya kuagana nao; mara ya kwanza hilo wazo halikuingia akilini mwa yule mama lakini akafanya kama alivyoambia na mchungaji wake. Alipomaliza, wakati anarudi nyumbani, watu mbalimbali pale ofisini wakamtafuta na kumuuliza kama anaweza kuwatengenezea keki kwa “oda” maalumu, kwa kuwa keki zake ni nzuri. Baada ya muda kidogo yule mama alikuwa na ofisi yake, akanunua mashine kubwa zaidi na kuajiri watu wengine katika ofisi yake.

Mara kadhaa tumesikia watu wakisema, “Tatizo sio tatizo bali tatizo ni namna ambavyo mtu analitazama tatizo”; ukitafakari usemi huu utagundua kuna ukweli ndani yake. Kumbe, hatua ya kwanza kwa mtu ili aweze kuvuka katika changamoto fulani, ni kuangalia namna ambavyo analitazama jambo hilo vinginevyo mtu anaweza kufanya kosa kama la Ibrahimu au kukubali kuwa dhaifu mbele ya changamoto kama mfalme Sauli na wana Israeli . Wiki ijayo tutangalia mambo kadhaa ya kumsaidia mtu aweze kuona zaidi ya anachoona ili kupata matokeo bora zaidi….

See you at the Top

0 comments :