Laiti kila mwenye dhambi angalitambua hili

9:44:00 PM Unknown 0 Comments

LAITI KILA MWENYE DHAMBI ANGELITAMBUA HILI!
[Wana ujumbe nusu na hivyo hauleti maana kamili]
Kila mwenye dhambi anajua fika kwamba yeye ni mwenye dhambi.  Kujua kwamba tuna dhambi haitoshi, lazima tujue kwamba, Mungu yuko tayari kutusamehe. Kujua kwamba, unadhambi kunaleta uchungu lakini kujua kwamba, Mungu yuko tayari kusamehe kunaleta amani ikiwa utalifanyia kazi wazo hilo. Kama kila mdhambi angelijua hilo angeliomba toba mapema.
Mungu hafanyi maandalizi ili ajiweke tayari kusamehe bali yuko tayari hata sasa kusamehe. Laiti kama kila mwenye dhambi angelijua hili, wengi wangetubu, shida yao wana ujumbe nusu, wanajua wazi ni wenye dhambi, bali hawajui  kama Mungu yuko tayari kusamehe.
Yohana 8:1-8 inaeleza, nyakati zile Mafarisayo walipomkamata [mfumania] yule mwanamke katika zinaa walimpeleka mbele za Yesu wakiwa na wazo la kumpiga kwa mawe mpaka kufa kama ilivyokuwa katika sheria ya Musa. Lakini Yesu aliposema, “asiye na dhambi na awe wa kwanza kumtupia jiwe”, biblia inasema, wote waliokuwa pale kuanzia watoto wadogo mpaka wazee walishtakiwa mioyoni mwao, ikiwa na maana mioyoni mwao walishuhudiwa kwamba, wao pia ni wenye dhambi. Hakuna mwenye dhambi asiyejua kwamba yeye ni mwenye dhambi. {Yohana 8:7-8}
John Newton mtunzi wa wimbo maarufu duniani, ‘amazing grace’ anasema, “nijualo mimi ni hili, mimi ni mwenye dhambi mkuu, na Yesu Kristo ni Mwokozi mkuu”. Anajua yeye ni mwenye dhambi na anaifahamu na tiba pia.  Hakuna mwenye dhambi asiyejijua wala asiyeijua hukumu yake. Imeandikwa:  Maana neno hili mnalijua hakika, ya kwamba hakuna mwasherati wala mchafu wala mwenye tamaa, ndiye mwabudu sanamu, aliye na urithi katika ufalme wa Kristo na Mungu.” Waefeso 5:5
Paulo anasema, neno hilo tunalijua hakika, tunafanya tunachokijua, tunajua madhara yake na hasara zake tunazijua pia. Je, ni nani hajui kama Mungu anachukia wizi, udhalimu, uchafu na ubaya wote? Bila shaka sote tunajua.
Yesu aliposema asiye na dhambi na awe wa kwanza kumtupia mwanamke huyu jiwe, biblia inasema wote walisutwa nafsini mwao yaani, hakusalia hata mmoja asiyekuwa na dhambi wala ambaye hakujua kwamba anadhambi. Kumbe kila mwenye dhambi anajua anazo lakini hataki kuzipeleke kwa Yesu, maana hata hawa baada ya kushtakiwa mioyoni mwao hawakumwendea Yesu, badala yake waliondoka zao wakamwacha Yesu na yule mwanamke.
Ni muda muafaka sasa tumejua kwamba tunadhambi na tunachukua uamuzi wa busara wa kuzipeleka mbele za BWANA badala kukimbia au kuendelea kukaa nazo kama walivyofanya wayahudi hawa. Mungu yuko tayari kusamehe muda wote ungalipo hai, Mungu ni wa rehema na ni mwenye huruma nyingi; hatamdharau mtu mwenye dhambi atubuye, wala hawezi kumwacha aliyeumizwa katika ukosaji. Napenda kukualika leo mwendee kwa kusema maneno haya: “Ee BWANA uniwie radhi mimi mwenye dhambi, nimejua makosa yangu na nimejua wokovu wako. Unioshe kwa damu yako na unioneshe na wokovu wako leo. Amina”
Aksante kwa kuja na kushiriki katika msimu wa nne [4] wa weekend of purpose, makala zijazo tutakujuza  mafundisho yatokanayo na weekend of purpose kwa uchache.

0 comments :