Mbona umeacha

12:28:00 PM Unknown 0 Comments

 
MBONA UMEACHA?
(Hakikisha unaanza tena)
Ulianza kusali vipi mbona umeacha? Ulianza biashara vipi mbona umeishia njiani? Ulianza kusoma kozi ile vipi mbona umekwama? Kwa nini umeacha kufanya mazoezi? Tatizo liko wapi? Hauoni kwamba, huu ni muda sahihi kwako kurejea kwa kishindo.
Katika siasa kuna neno maarufu liitwalo, “bouncebackability” ambalo linaelezea uwezo wa mwanasiasa kuinuka tena. Anaweza kuonekana ameishiwa sera au ameanguka kabisa, na ghafla anasimama na kushinda kwa kishindo. Ufufuko wa Yesu nao ulikuwa na sura hiyo. Kwa siku mbili na zaidi alizokuwa kaburini wengi walidhani ameshindwa kabisa, hata mitume wake walikata tamaa, siku ya tatu alifufuka na kutoka mzima.
Hii ni wiki yetu ya kusimama tena na kurejea katika nafasi zetu kwa kishindo.  Ni wiki ya kumwomba BWANA, afufue kazi zake ndani yetu. Inawezekana wewe ni mhubiri mfu, ni kiongozi mfu, ni mkristo mfu au ni mhandisi mfu. Lakini ni saa yako na yangu kumwambia, “EE BWANA FUFUA KAZI ZAKO NDANI YANGU”
Ni muhimu kumaliza ile kazi tuliyoianza, ni muhimu zaidi kuanza tena kutokea pale tulipoishia. Mwanariadha mmoja wa Tanzania akiwa katika mashindano ya Olimpiki aliendelea kukimbia na kumaliza mbio hizo ndefu licha ya kuumia. Napenda maneno ambayo mtangazaji alimpamba mwanariadha huyo aliyekuwa majeruhi alisema: “Sikutumwa na Nchi yangu kutoka mamilioni ya maili ili kuanza mbio, bali nimetumwa kumaliza mbio.”
Ni kweli kabisa hatukuitwa kuanza bali kumaliza, hatukuitwa kuwa washiriki tu wa maisha bali tumeitwa kuishi kama washindi. Je, Nguvu yetu inatoka wapi? Nguvu yetu si tu ile itokanayo na chakula tunachokula yaani, protini, vitamin, maji na vyakula vya nguvu. Nguvu yetu ni zaidi ya chakula tulacho, nguvu yetu yatoka kwa Bwana Mungu aliyeziumba mbingu na nchi. Kwa Yeye (Yesu Kristo) tunayaweza mambo yote na tunahakika tutamaliza.
Kwa kuwa bado tuko hai basi kila kitu kinawezekana. Napenda mchezo wa mieleka, somo kubwa katika mchezo huu ni kwamba, kuwekwa chini si kushindwa na kupigwa sana si kupoteza mchezo. Mara nyingi katika mchezo huu hata aliyechoka huweza kuibuka mshindi. Ni siku yako leo, toka kaburini, anza tena, maliza kazi yako, Mungu Baba na afufue kazi yake ndani yako katika jina la Yesu Kristo. Amen

0 comments :