Swali lililowapoteza wengi

5:28:00 PM Unknown 0 Comments

 
SWALI LILILOWAPOTEZA WENGI
(Nitakula nini, Nitavaa nini)
Kujiuliza kwamba, utakula nini na utavaa nini ni swali ambalo limewapoteza wengi, wengi kwa kujiuliza swali hilo wameachana na wito wao. Wengine wamepoteza wito wao kwa kujiuliza kuhusu wazazi wao na jamaa zao, watakula nini na watavaa nini.
Naamini wazi ni kwa sababu hiyo Yesu alitutaka tusijiulize swali hilo. Aliwataka wanao mwamini waachane na swali hilo. Alitumia mfano wa maua ya kondeni na ndege wa angani ambao hawapandi wala hawavuni lakini wanaishi, alisema sisi ni bora zaidi mbele zake kuliko ndege wa angani. Akawaambia wanafunzi wake, Kwa sababu hiyo nawaambia, Msisumbukie maisha yenu, mtakula nini; wala miili yenu, mtavaa nini.” Luka 12:22
Yesu anasema hatuwezi kutumikia mabwana wawili, hatuwezi kutumikia Mungu na mali. Unapoitwa ni lazima uchague kimoja. Wengi wanapoitwa katika uinjilishaji wanakataa kwa sababu biashara zao zitakufa. Wengi wanaoitwa katika wito wa ukombozi wa nchi zao au wa roho za watu wanakataa kwa kuwa jambo hilo litaumiza wanaowategemea kwa chakula na mavazi.
Rai yangu kwako leo ni kwamba, unaposikia kuitwa na Mungu kufanya kazi fulani usijiulize swali ambalo Yesu ametukataza. Wengi wamejikuta wanaogopa kupigania haki kwa sababu tu itaathiri kipato chao au chakula chao. Wito wako ndio kitambulisho chako, kukataa wito ni kujikataa. Wengi wanajulikana kwa majina ya wito wao: mwalimu, mwinjilisti, mchungaji, kiongozi, waimbaji, wasanii na wabunifu.
Wito unaleta faida kwa watu wengi zaidi kuliko sisi na familia zetu, mamilioni ya wana wa Israeli walitegemea utii wa Musa, Mamilioni ya watu wa Afrika kusini walitegemea utii wa hayati mzee Nelson Madiba Mandela.Tunapoishi kwa ajili ya Mungu tunaishi kwa ajili ya watu wengi ambao kwa hakika hata si ndugu zetu wa damu.  Pastor Chris Oyakhilome anasema, “It is the spiritual family that means so much to God, It is not for your biological family” yaani, “Ni familia yako ya kiroho ndiyo yenye mashiko zaidi mbele za Mungu, wala si kwa ajili ya ndugu zako wa damu”
Ingawaje kwa asili Musa alikuwa Mwebrania lakini kimwili alikuwa ni mwana wa binti Farao, alijulikana kama mtu anayetokea katika familia ya kitajiri. Angeliweza kukubali kuishi kwa ajili ya familia ya Farao. Lakini familia ya kiroho ya Musa ilihusisha watumwa, watu wasio na kitu, watu wanaoteswa utumwani. Musa aliitwa kwa ajili ya watu wasio na kwao, uwe na hakika wito wako utakuletea familia na utapaswa kuteseka kwa ajili ya familia hiyo.
Bwana anapokuita na kukutuma kwa ajili ya jambo fulani uwe na hakika hatakupungukia kwa chochote. Alipowaita na kuwatuma mitume wake hawakuwa na kitu lakini pamoja na hayo hawakupungukiwa na kitu. Usijiulize kuhusu nguo na mavazi ya ndugu zako, usijiulize kuhusu chakula chakula chako, mara zote walioitwa walilazimika kuacha mifugo yao (kondoo), wengine biashara zao(uvuvi) na ndugu zao (wazazi).Katika hawa wanafunzi wote pamoja na kuacha kila kitu bado hawakupungukiwa chochote, na Yesu anawauliza mitume wake swali la kuwajenga: “Akawauliza, Je! Hapo nilipowatuma hamna mfuko, wala mkoba, wala viatu, mlipungukiwa na kitu? Wakasema, La!” Luka 22:35
Wanafunzi walijibu, ”lah!” wakiwa na maana kwamba hawakupungukiwa na kitu. Katika maisha yetu tumemwona Bwana na sasa tunakika naye hata jangwani tunajua hatutakosa maji, hata usiku tunajua hatutaogopa, hata hatarini tunahakika tutatoka salama. Kuna maneno mawili tu ndiyo twaweza kumjibu BWANA pale tunaposikia kuitwa, nayo ni, “ndiyo BWANA.”

0 comments :