Moto wa milele upo

2:14:00 PM Unknown 0 Comments



MOTO WA MILELE UPO
(Neno liko kama lilivyo wala si zito)

Ben Carson ni mwanataaluma mstaafu, mwandishi na mwanasiasa ninayempa heshima kubwa. Lakini kuna eneo moja tunatofautiana sana ki-msimamo na ndugu Ben Carson. Ben haamini katika moto wa milele licha ya kwamba, neno la Mungu linasema kuna moto wa milele, linasisitiza waziwazi jehanamu ya moto ipo.

Ben anajenga hoja kwamba, “Mungu hawezi kumhukumu mtu aliyefanya makosa kwa miaka sitini (60) adhabu ya milele labda adhabu ya miaka sitini (60)”. Ben anaona ni afadhali mtu akikosa kwa mwaka mmoja akae Jehanamu kwa mwaka mmoja, ni mawazo yake. Mawazo ya mwanadamu yeyote kama Ben si ya kusikilizwa ikiwa tu yanakinzana na neno la Mungu. Neno litasimama imara hata kama wanasiasa wote watalipinga hata kama ulimwengu wote utalikataa. Alichosema Yesu kitabaki pale pale, neno lake halibadiliki kamwe. Yeye mwenyewe amesema, “Mimi ni Mungu, Sina kigeugeu”

Jehanamu ilikuja kama dharura, katika uumbaji hatusikii Mungu akiumba Jehanamu. Mwandishi wa kitabu cha Mwanzo, Musa haoneshi kama hapo mwanzo jehanamu iliumbwa. Mungu hakuumba watu au Malaika ili awaangamize, wote aliwaumba kwa utukufu wake. Lusifa alipokosa ndipo Jehanamu ilipoundwa kwa ajili yake na si kwa ajili ya wanadamu.  Jehanamu ni kwa ajili ya shetani ambaye ni muasi, wanadamu wakienda huko wanakwenda mahali ambapo si pao.

Yesu alisema, “Nakwenda kuwaandalia makao”. Makao ya wandamu ni mbinguni mahali alipo Yesu. Ukiangalia mateso yaliyoko Jehanamu utagundua si eneo ambalo Mungu anataka watu wake waende. Kumbuka alipoweka bustani nzuri ya Eden, ikiwa na mito, miti mizuri, ndege, samaki na wanyama wazuri ndipo alipowaweka Adamu na Eva. Je, alipoweka moto mkali, sehemu yenye kiu kali, sehemu ya mateso na dhiki kuu alimkusudia nani? Bila shaka alimkusudia shetani na malaika zake. Ufunuo 20:10 “Na yule Ibilisi, mwenye kuwadanganya, akatupwa katika ziwa la moto na kiberiti, alimo yule mnyama na yule nabii wa uongo. Nao watateswa mchana na usiku hata milele na milele.

Watu wengi hawaamini katika uwepo wa moto wa milele na kama wangeliamini basi wangelibadilika. Lakini ukweli ni kwamba, moto wa milele upo. Watu wataungua usiku na mchana, watu watalia na kusaga meno. Wataona kiu bila ya kupewa maji, wataishi motoni milele, yaani bila mwisho. Na iwapo mtu ye yote hakuonekana ameandikwa katika kitabu cha uzima, alitupwa katika lile ziwa la moto. Ufunuo 20:15

Siku moja nikiwa ofisini dada mmoja alinieleza kwamba, anampenda Mungu lakini hawezi kuacha dhambi. Kwa kuwa napenda kuhubiri nikaamua kurefusha maongezi huku nikimweleza jinsi jehanamu palivyokuwa pabaya. Ni kweli pasipo neema ya Kristo na msalaba wake hatuwezi shinda dhambi, lakini ni lazima tujue sana kuhusu matokeo ya kudumu ya dhambi (eternal repercussions).

Nilimweleza kwa hekima, Ok! Unaona ugumu kuacha dhambi vipi umejiandaaje kuikabili jehanamu ya moto. Kila tunapotenda dhambi kwa lugha nyingine tunasema, tuko tayari kwa jehanamu, tuko tayari kwa jehanamu ya moto. Binafsi ninaogopa ni heri nitubu na kugeuka.

KInachowafanya watu wapende jehanamu na kumkataa Mungu ni uhuru. Wanataka wafanye kile miili yao inapenda, wavae kili miili yao inajisikia, waishi wanavyotaka, na waseme wawezavyo. Hawataki kujitia chini ya mamlaka ya Mungu na Kristo wake.

Waefeso 5:5 “Maana neno hili mnalijua hakika, ya kwamba hakuna mwasherati wala mchafu wala mwenye tamaa, ndiye mwabudu sanamu, aliye na urithi katika ufalme wa Kristo na Mungu.” Hawafanyi kwa bahati mbaya, Biblia inasema wanajua. Uhuru wowote unaoturuhusu kulidharau neno la Mungu ni utumwa. Sheria za nchi zinazopingana na neno la uzima ni pingu ya milele kwa raia wa nchi husika. Chagua moja leo mbinguni au Jehanamu? 

Tubu ufalme umekufikia leo. Kama uko tayari kugeuka sema pamoja na mimi: “Bwana Yesu wewe ni mwenye haki na mimi ni mdhambi. Unirehemu Bwana na uyafute makosa yangu yote. Uniumbie na moyo safi kwa maana, sina moyo safi. Nipe na Roho wako Bwana aniongoze tena. Amina”

0 comments :