Linda sifa yako nzuri

4:27:00 PM Unknown 0 Comments

 
LINDA SIFA YAKO NZURI
(Mwenendo wangu ni mzuri kuliko uzuri wa huyu dada)
Manukato au marashi husifika kwa kutoa harufu nzuri sana, hata hivyo harufu hiyo haiwezi kwenda mbali ukilinganisha na sifa njema. Sifa njema huenea kijiji kizima, manukato hayana uwezo huo. Sifa njema huenda mbali sana mahali ambapo manukato hayafiki. Nelson Mandela, nani asiye mjua? Yesu Kristo Mfalme, nani aisiyemjua? Askofu Desmond Tutu, nani asiyemjua? Vipi kuhusu sifa za mama Teresa? Sifa za hawa wote zimeenea mno.
Imenenwa katika Mhubiri 7:1a “Heri sifa njema kuliko manukato mazuri” ikiwa na maana, heri mwenendo bora na halisi kuliko mwenendo mbaya na feki. Ikimaanisha heri kuwa na mwenendo mmoja wa kweli kuliko kuwa mnafiki. Heri kuonesha tabia yako ya ndani kuliko kuificha. Manukato au marashi hutoa harufu ambayo kwa asili si ya mtu. Hata kama mtu hujaoga manukato yanauwezo wa kufanya anukie vizuri. Manukato yanaficha uchafu wala hayauondoi. Manaukato yanakusanya uovu na kuupa harufu ya wema.
Jina jema ni jumla ya matendo yako, jina jema ni kitambulisho chako. Marhama au manukato [perfume] hufanya tunukie vizuri hata kama moyoni mwetu tumeoza kwa sababu ya dhambi. Maandiko yanatutaka tuchague jina jema. Ninafananisha jina jema na utakatifu wa ndani na manukato ni harufu inayoficha ile dhambi ikaayo ndani ya mtu.
Siku moja tulikuwa mahali fulani na kulikuwa na dada mrembo kweli kweli. Na wengi walimtolea macho, na rafiki zangu walitamani na mimi nitoe macho. Kwa kweli alikuwa dada mlimbwende lakini haina maana yoyote kama kila tunapokutana na mrembo tunashindwa kujitawala. Kushindwa kujizuia ni dalili ya watu wa siku za mwisho. “…Wasiojizuia…” 2Timotheo 3:3
Rafiki zangu walitaka nichangamkie fursa ya yule dada wakiniambia, “pastor vipi” yaani, “mchungaji vipi” na mimi nikawajibu kizungu, “my character is beautiful than the beauty of this lady” yaani, “mwenendo wangu ni mzuri kuliko uzuri wa huyu dada”. Mara nyingine tumepotea kwa sababu tumekwenda haraka bila ya kujali muda mwingi ambao tumetumia katika kujenga haiba, tabia na wasifu wetu.
Dada mmoja aliniambia kwa masikitiko jinsi sifa yake ilivyoharibiwa haraka na kaka waliyeingia naye kwenye uhusiano. Aliandika kwa huzuni, “ameharibu sifa yangu yote”. Huenda ni sifa ambayo aliijenga kwa muda mrefu ya mwenendo bora. Imeharibiwa katika mwendo wa sekunde tu!
Katika karne hii waaminifu na wenye mwenendo bora wamekuwa bidhaa adimu. Watu hawaamini kama utakatifu unawezekana tena. Hawawezi kukubali kama utawaambia wewe si mlevi wala si mwasherati. Rafiki yangu hupenda kusema, “simba akisema hali nyasi hajidai ndivyo alivyo”.  Leo hii tabia nzuri zimekuwa adimu, dunia haimini kama Simba hali nyasi, inachojua ni kwamba kila mtu ni mwovu tu.
Kuna jambo linashangaza kidogo, wakati mji mzima wa Ninawi ukiokoka, mji mzima wa Sodoma na Gomara uliangamia. Yaani wakati mkoa fulani wote unaokoka mkoa mwingine wote unaangamia. Kanuni ni hii, ni vigumu kumpata mtakatifu katikati ya waovu, na ni vigumu kumpata mtu mwovu katikati ya watakatifu. Miji hupambana kuhakikisha ama ni uovu tu unaoshamiri au utakatifu tu ndio unashamiri. Kwa asilimia hamsini mtu ni mazingira yake. Pastor Sunday Adeleja anasema, “Mazingira yanatutengeneza kwa takribani asilimia 50”  sisi pia ni matokeo ya mazingira yetu.
Kazi ya wahubiri ni kufanya mazingira ya mbinguni yaje duniani, ambayo ni amani, utakatifu na uaminifu. Dunia ni kama msitu mkubwa ambao wanyama wote hula nyasi. Sasa wanyama walao nyasi hawataki kuamini kwamba wapo wasiokula nyasi, simba hali nyasi. Ndivyo walivyo watakatifu katikati ya ulimwengu ambao BWANA mwenyewe amesema ni wa mbwa mwitu. Chukua muda huu kutafakari tabia, mwenendo na haiba yako na kisha amua kubadilika na kuulinda mwenendo wako mzuri. Mpaka wiki ijayo Shallomu…

0 comments :