Kwa kila ambaye....... II

10:11:00 AM Unknown 0 Comments

KWA KILA AMBAYE HAJAOA AU KUOLEWA - II
(Amua kuwa na familia ya aina hii)
Tunapoandika kwa kila ambaye hajaoa na kuolewa sisi pia ni wahusika. Tunapokufundisha tunajifunza pia, na nyakati nyingine tunayasema yale ambayo BWANA ametupa sirini ili kutusaidia. Mengine ni uzoefu wetu unaotokana na miongo kadhaa ambayo Bwana ametukirimia hapa Duniani, yamkini pia ni mafunzo kutoka katika  kukosea kwetu au kutoka kwa  wale ambao tumepata nafasi ya kuwafuatilia. Msanii mmoja anasema, “wasio na watoto ndiyo wanajua kulea vizuri” anamaanisha ndio wanazungumza sana wakidhani ni rahisi wasijue kinachowapata wazazi katika kulea na kukuza watoto. Katika makala hii ninaandika nikiwa na tahadhari hiyo kichwani.

Ili kuepuka majuto na sintofahamu kila ambaye hajaoa na kuolewa azingatie mambo yafuatayo:

Mungu ndiye atoe jawabu: Hili ni gumu ila ni la kweli na hivyo hatuna budi kulisema. Maandiko yanaonesha wazi wazi, “BWANA ndiye akataye nena” pengine imenenwa, ‘’jawabu la ulimi latoka kwake” yote yakimaanisha kwamba, BWANA MUNGU ndiye mwenye maamuzi ya mwisho na ndiye mwenye sauti ya mwisho. Yesu alipotaka kuepuka kikombe cha mateso aliomba, alitaka iwe ni mapenzi ya Mungu kukiepuka na hata alipokipokea bado ilikuwa ni mapenzi ya Mungu. Mwenye hekima mmoja anasema, “You cannot say, ‘Your will’ without saying ‘not my will’” Ni kweli hatuwezi kusema tumemwachia Mungu aamue ilhali sisi wenyewe bado tumeshikilia msimamo wetu. Kinachonifanya nimwombe Mungu si tu ni kwa sababu nampenda bali ni kwa sababu sijimiliki, Yeye ni muumba wangu na mimi ni mali yake. Yeye ni mfinyanzi na mimi ni chombo chake. Si urembo, urefu na utanishati ndio uwe kivutio chetu, la hasha! Chaguo la Mungu ndiyo chaguo letu. Epuka kumnyima Mungu kuwa mwamuzi wako katika jambo la msingi namna hii. Derek Prince anakiri kila ilipokuja suala la kuoa mara zote (mbili kufuatia kifo cha mke wa kwanza) alimtegemea Mungu pasipo kuweka ujuzi wake. Nimefuatilia hekima ya wengi waliotutangulia, akiwamo Sunday Adelaja, Billy Graham na Derek Prince kwa ujumla wanashauri watu waoe chaguo la Mungu. Waachane na watu waliowachora kichwani (chaguo la fikra) badala yake wapokee zawadi toka kwa Bwana.

Jizatiti katika Viwango vya kimungu (Committed to God’s standard): Ndoa ni ya kimungu, ni wazo lililotoka moyoni mwa Mungu wala si akilini mwa Adamu. Ziko ndoa za kihindi, za kiafrika, za mkeka, za serikali na nyingine nyingi. Lakini ndoa hizi kama hazikuwekwa katika viwango vya kimungu ambavyo ni vya kibiblia si tu kwamba huwa hazina mashiko bali huwa hazikamilishi kazi. Kusudi la ndoa ni kazi, anayetoa kazi hiyo ni Mungu. Ndiye anajuaye wanaofaa kwa ufanisi bora wa jukumu hilo. Viwango vya kimungu ni pamoja na kuwa na mke mmoja tu (msaidizi na si wasaidizi), kuwa na watoto waadilifu, kukamilishana, kuwa na usafi na utakatifu. Mungu hakutaka kuleta Dunia ya watu bilioni saba kwa siku moja bali alitaka kwa kupitia familia moja (ya Adamu na Eva) wapatikane watu wote zaidi ya bilioni saba. Nadhani nia kubwa ni kupata ubora ule ule wa utakatifu, uchaji na uadilifu. Rafiki yangu aliandika: “Quality is never an accident, it is planned”

Achana na ndoto: Kuna rafiki zangu wa kike ambao walikuwa na ndoto na maono kwamba, tutaoana na sasa hivi wameshaolewa na watu wengine kabisa; tena kwa ndoa takatifu, na mimi naziheshimu. Kuna wengine nilipata maono na wao wakapata njozi lakini sasa wako na watu wengine na mimi nawaita shemeji. Ndoto ni hatari! Ndoto ni njia isiyoaminika. Zamani nabii akiota ndoto na kuisema au akitabiri na isitimie basi aliuawa. Kama ndoto za ndoa zingekuwa hivyo basi wengi wangepigwa na kuchinjwa kama manabii wa uongo mfano wa manabii wa baali walivyochinjwa na Eliya. Naamini ukikaa katika neno la Mungu utakuwa salama, achana na ndoto. Ndoto zinapoteza wengi kuliko wanaonufaika. Ndoto za injili na kazi hazina shida lakini za harusi na ndoa zinamatatizo, si kigezo halali cha kumkubali mtu.

Omba bila kukoma: Wanaosema hili si la kuombea hawana tofauti na wanaosema hakuna Mungu. Binafsi najua Mungu atanijibu na kunipa haja ya ninachostahili katika Kristo. Si tu kwamba najua atanijibu, bali ninajua tena kwa hakika. Omba kwa bidii kiasi kwamba hata Mungu akijibu usiweze kujua amekujibu maombi uliyaomba lini bali uwe unajua tu, amekujibu. Nampenda Hudson Taylor mmisionari mwenye alama anasema, “kila alichonacho ni matokeo ya maombi”. Hata mshahara wake ulipochelewa hakuthubutu kumwambia kiongozi wake, bali aliingia kwenye maombi alitaka mshahara wake uwe ni jibu liliotokana na maombi. Ni furaha namna gani kuwa na familia ambayo baba, mama na watoto wote ni matokea ya maombi? Nimeshuhudia watoto katika nyumba ya dada yangu ambao  ni matokeo ya maombi, na ni furaha kuona matunda ya maombi katika ulimwengu wa nyama. Pray, pray, pray

Tukutane wiki ijayo, usikose makala yako. Shallom…

0 comments :