Napendekeza usikope

5:47:00 PM Unknown 0 Comments


 
NAPENDEKEZA USIKOPE
(Makala ya Kwanza) 
Kukopa katika benki (taasisi za fedha) ili kujikomboa kiuchumi ni sawa na kujificha chini ya transifoma ya umeme wakati mvua kali yenye kuambatana na radi ikinyesha. Benki nyingi hazikopi hovyo na zikilazimika kukopa hufanya hivyo ili kuwakopesha wengine. Wanakopa ili kukopesha na kuwekeza. Je, ni watu wangapi ambao wana mikopo benki; walichukua mikopo hiyo ili kukopesha wengine au ili kuwekeza kwa lengo la kupata riba? Mpaka tumejitazama na kuhamia katika nafasi ya benki hatuwezi kupata matokeo mazuri kama benki zipatavyo faida katika mikopo yake. Kwa kweli nalazimika kukumbuka na kujaribu kutafsiri maneno ya mshairi huyu: “Benki ni mahali wanapokupatia mwavuli wakati hali ya hewa ni tulivu na kukutaka urejeshe mara tu mvua itakapo anza kunyesha” Robert Frost
Inawezekana ujumbe wangu ukaleta ukakasi masikioni mwako na ganzi katika meno yako, ndiyo! Sote tumelelewa na kukua huku; nchi, wazazi, walezi pamoja na jamaa zetu wakikopa na hivyo makala hii inakabiliwa na upinzani mzito kutoka katika Historia. Sijui kama unajua, mtoto akizaliwa jela hupaita nyumbani badala ya gerezani. Tuliozaliwa katika mazingira yenye changamoto lazima tufikiri kwa upya namna ya kutoka katika ombwe la mikopo. Namna ya kuvunja kawaida isiyofaa.  Kawaida nzuri au utamaduni mzuri waweza kuwa sheria lakini si busara kuacha kawaida mbaya kuwa kama sheria.
Kuna watu wanakopa kwa sababu hawataki kupunguza matumizi yasiyo ya lazima. Kuna matumizi mengi tunayafanya na hayana tija ndani ya dakika tano zijazo. Ni matumizi ambayo hutupatia furaha wakati tunapoyafanya na baada ya hapo kilio. Mwenye hekima mmoja anasema, “Ikitokea bahati mbaya mchimba shimo akajikuta ndani ya shimo jambo la kwanza analopaswa kufanya ni kuacha kuchimba shimo hilo ili asijichimbie kwenda kina kirefu zaidi”. IKiwa uko katika madeni na mikopo isiyokwisha jambo la kwanza la msingi ni kuamua kuacha kukopa. Ninapendekeza usikope katika benki na taasisi nyingine zenye kutoza riba kubwa.
Mikopo inadumaza akili, inakutaka uwe mteja wa benki kila siku tena haikupi nafasi ya kufikiri kama benki. Badala ya kuwaza  kukopesha watu wengine, milele utakuwa ukiwaza kukopa. Wakati wewe unawaza ukope shilingi ngapi, benki wanawaza wakutoze riba kiasi gani. Umewahi kuwaza kwamba kusingekuwa na mikopo ungeishi vipi? Ni kweli kwamba, hakuna namna nyingine ya  kuishi isipokuwa kwa kukopa tu? Naamini jawabu ni hapana.
Jambo la kwanza kabla ya kufanya uamuzi wa kukopa si kuitazama shida yako bali ni kuangalia masharti ya mkopo husika. Je, unauwezo kiasi gani wa kuyasoma na kuyadadavua masharti ya mkopo? Kesi ya meno hupelekwa kwa daktari wa meno, mambo ya nyota kwa mamajusi iweje mambo yahusuyo pesa yaende bila idhini wala ushauri wa mtaalamu yeyote?  Ni vizuri wataalamu wakupe ushauri kuhusu mkopo wako, na wataalamu hao wawe ni nje ya benki. Kesi ya nyani usimpelekee tumbili.
Kila tunapokopa kwa lugha nyingine tunatangaza kwamba sisi si wabarikiwa. Je, unalijua na hili? Tunapokopa tunamaanisha tumepungukiwa ilhali ahadi inasema hatuta pungukiwa: Msiwe na tabia ya kupenda fedha; mwe radhi na vitu mlivyo navyo; kwa kuwa yeye mwenyewe amesema, Sitakupungukia kabisa, wala sitakuacha kabisa.” Waebrania 13:5
Tafakari halafu Chukua hatua, usikope hovyo. Wiki ijayo nitaendelea kujenga hoja ili tujue ubaya wa mikopo hii ni kulingana na utafiti nilioufanya kwa kuwahoji na kutazama mwenendo wa jamii ya sasa. Hadi wiki ijayo, Shalomu!!!
Kwa maswali au maoni  kuhusu hili tuandikie katika email na blog yetu.

0 comments :