Je unalijua hili?

11:38:00 AM Unknown 0 Comments

 
JE UNALIJUA HILI?
Ili kufanikiwa katika jambo lolote; liwe kubwa au dogo, inahitajika nidhamu; pia ili kutunza mafaniko ya jambo hilo ulilolipata kwa sababu ya nidhamu uliyokuwa nayo wakati unaanza, unahitaji nidhamu pia. Hakuna mafanikio ya kweli yasiyohitaji nidhamu dhabiti.  Nioneshe mtu aliyefanikiwa; nikuoneshe mtu mwenye nidhamu katika njia yake. Ni nidhamu ndiyo inayoleta mafanikio; Ni nidhamu ndiyo itakayotunza mafanikio hayo.

Mchezaji wa mpira wa kikapu kwa jina Michael Jordan, alikuwa akiamka alfajiri na mapema na kwenda uwanjani peke yake, ili kufanya mazoezi. Wakati vijana wa umri wake wamelala, yeye alifanya mazoezi.  Alijua kuwa hawezi kuwa bora katika kikapu “basketball” endapo atafanya mazoezi kwa kiwango na kiasi cha muda ule ule sawa na watu wengine. Nidhamu yake ilikuwa ya hali ya juu. Kwa sababu ya nidhamu hii, jina lake linatajwa katika kila kona, kama shujaa wa mpira wa kikapu ulimwenguni. Watu wengi hutamani kuwa na mafanikio kama yake; lakini hawako tayari kulipa gharama ya kuwa na nidhamu aliyokuwa nayo. Nioneshe mtu mwenye nidhamu, nikuoneshe hatima yake.

Watu wakuu hawakufikia kilele cha cheo kwa sababu walikimbia (hawakuwa na uwezo kuliko wengine); bali wakati wenzao walipolala wao walipanda juu” (kitabu cha uongozi wa Kikristo, Oswald Sanders, msisitizo umeongezwa)

Kama ungejua mambo uliyoyapoteza katika maisha kwa sababu ya usingizi [uliopitiliza], ungeshangazwa sana” (Pastor Chris Oyakhilome, msisitizo umeongezwa)

Nidhamu ni uwezo na nia ya kujitawala na kujiongoza; kuamua kujiwekea mipaka, kujinyima, kujikatalia na kujizuilia mambo yanayoonekana kuwa mazuri sasa ili kupata yaliyo bora zaidi kesho. Ni muhimu kujiwekea viwango (standards) vya maisha na kuvisimamia, lazima kujijengea uwezo wa kuwa na msimamo ulio dhabiti; na kusimamia maamuzi yako ili kufikia mfanikio ya malengo uliyojiwekea.

Je unajua gharama ya kutokuwa na nidhamu [discipline /self-control]? Gharama ya kutokuwa na nidhamu ni kuharibu maono na ndoto zako. Hata kama tutakuwa na malengo, pamoja na mipango mizuri, hasa katika mwanzo huu wa mwaka; kama hatutachagua kujenga nidhamu dhabiti; ni sawa na mtu anayekimbia haraka ili kuwahi mahali asipopajua.

Njia ya mkato inatajwa kuwa chanzo cha ukosefu wa adabu na nidhamu. Badala ya mazoezi watu wanatumia dawa za kuongeza nguvu michezoni kama njia ya mkato. Badala ya kusoma watu wanaiba vyeti kama njia ya mkato. Badala ya subira watu wanaingia katika tabia chafu kama njia ya mkato. Ni kweli, easy way is the source of all immoral behavior! 
Kumbuka; kusoma Neno la Mungu kunahitaji nidhamu, Kuweka akiba kunahitaji nidhamu, kuamka mapema kunahitaji nidhamu, mahusiano bora yanahitaji nidhamu, matumizi bora ya muda yanahitaji nidhamu, kusoma kunahitaji nidhamu; ili kufikia malengo na mipango yako uliojiwekea unahitaji nidhamu pia…kwa kifupi, hakuna jambo lenye kufaa  ambalo nyuma yake hakuna nidhamu iliyojengeka ili kufanikisha jambo hilo.


0 comments :

Yanayo Ondoa Furaha Yetu

2:35:00 PM Unknown 0 Comments

 

YANAYO ONDOA FURAHA YETU
Yako mambo mengi yanayotuondolea furaha na kutujaza mioyo yetu huzuni kuu.  Kuyajua mambo hayo ni ufunguo kuelekea furaha ya kweli. Mambo hayo ni pamoja na dhambi. Dhambi hufanya tujisikie vibaya, toba ya kweli huturejeshea furaha hiyo. Kama tunataka nyakati za kubarizi katika uwepo wa Mungu ni lazima tutubu; Mungu ameahidi kwa kinywa cha mtume Petro kwamba tukitubu tutapata burudiko la moyo.
 Tubuni basi, mrejee, ili dhambi zenu zifutwe, zipate kuja nyakati za kuburudishwa kwa kuwako kwake Bwana;” Matendo ya Mitando 3:19  Ahadi gani nzuri kama hii? Ningekuwa na kalamu ningeandika pembeni ya mstari huu, “I can’t miss this promise”. Burudani itarajea baada ya toba, uchungu na mgandamizo wa mawazo vitatoweka tukitubu. Yanayoondoa furaha yetu ni mengi, lakini toba ni mlango wa pekee wa kurejesha furaha.
Fyodor Dostoevsky ni Mrusi aliyeacha alama ya aina yake, maneno yake yamejaa mafunzo. Katika moja ya kauli zake anasema, “The greatest happiness is to know the source of unhappiness” kwa tafsiri isiyo rasmi, “Furaha kuu ni kujua chanzo cha mambo yanayotuhuzunisha”. Ukishajua nini chanzo cha huzuni yako basi huna budi kujitahidi kukifunga chanzo hicho.
Wakati mwingine tunagubikwa na huzuni kwa sababu ya kuficha siri ambazo zinatuumiza sisi wenyewe, hakikisha unatumia hekima kutoka katika kitanzi hicho. Wakati mwingine ni uhusiano usio afya; nao pia si wa kuulea sana.
Ni kweli kabisa, hatuwezi kukwepa maumivu ya kukosa uadilifu au huzuni ya udhalimu. Ni ama uingie gharama ya kuwa mwadilifu na mwaminifu au uingie gharama ya kuwa dhalimu na asiyeaminika. Kukimbia dhambi ni gharama, lakini kutenda dhambi na kukaa nayo ni gharama kubwa zaidi.
Watu wengi wenye dhambi hawapendi kusali. Ninapata funzo kubwa katika Luka 18:13 ninaposoma kwamba mwenye dhambi alikwenda kusali na Mungu akajibu sala yake. Ni jambo zuri mno kwamba, Mungu huwasikiliza hata wadhambi. Ikiwa Mungu huwasikiliza hata waovu basi tunataraji kuona dunia nzima ikisali.
Tatizo si dhambi, tatizo ni kutokwenda kusali; tatizo ni kutokumwendea Mungu. Wenye makosa wengi hawapendi kusali na ni ujanja wa shetani kwani anajua wakisali Mungu atawasikia na kuwasamehe. Twendeni tukasali, twendeni tukaombe toba. Wito wa toba si wito kwa watu binafsi tu, bali ni wito kwa makanisa, taasisi za kiraia, mashirika, mataifa na dunia nzima, sote tunahitaji kutubu.
Inawezekana umekosea, unahuzuni na unaogopa kusali tafadhali leo naomba tusali pamoja. Nalifurahi Yesu aliposema mtoza ushuru mwenye dhambi alikwenda kusali [Luka 18:10na 13]. Oh! akatoka amesamehewa na amejibiwa. Mpendwa usikate tamaa amua kusali leo. Nikualike useme maneno haya kwa imani kama mwanzo wa sala yako leo: “ BWANA YESU WEWE UMEWAKUBALI WAKOSAJI NA MIMI UNANIKUBALI. NAOMBA UNIREHEMU KWA DHAMBI ZANGU ZOTE AMBAZO NIMETENDA. NINA KIRI WEWE NI BWANA NA NINAAMINI MUNGU ALIKUFUFUA KUTOKA KWA WAFU” AMINA.


0 comments :

Usikasirike Unapohuzunishwa

12:26:00 PM Unknown 0 Comments

 
USIKASIRIKE UNAPOHUZUNISHWA
(ASUBUHI NI FURAHA)
Mara nyingi katika mazingira yetu ya kazi au katika mahusiano yetu na wenzetu ni rahisi kuhuzunishwa. Wakati mwingine tunahuzunishwa kwa sababu mfumo wetu wa vipaumbele na thamani [Priority and Value systems] umetofautiana kutoka mtu mmoja hadi mwingine. Lile ambalo ni kipaumbele kwako linaweza lisiwe la thamani/kipaumbele kwa mtu mwingine, hata hivyo bado kila mtu atapaswa kuheshimu vipaumbele vya mwingine.

Pamoja na hayo, watu ni muhimu kwetu, hatuwezi kuwa kamili kama hatutakubali kuishi maisha ya jumuiya kwa namna moja au nyingine. Watu ni muhimu kwetu; Unaweza kukaa bila mke au mume lakini si kukaa bila ya jamii au bila ya ushirika na watu kwa namna moja au nyingine. Ukijua umuhimu wao hata wakikuudhi utatafuta kuwa na amani nao. [1 Wakorintho 12:25]

Wakati mwingine jambo zuri linalotarajiwa linapozidi kuchelewa, mtu huweza kuhuzunika na kuugua moyo. Ni vema tukumbuke kuwa, Mungu ni Mungu wa nyakati zote na kamwe hafungwi na muda. Wewe una hofu inayoletwa na muda lakini Mungu anakuhofia wewe kwa kuwa uwathamani machoni pake. Mungu ni wa milele, kwahiyo muda si kikwazo kwake.

Mtoto aliyechelewa kwenda shule anaweza akavuka barabara pasipo kuchukua tahadhari ya kutosha. Kwa mtoto muda ni muhimu; kwa mzazi wake mtoto ni muhimu. Mungu anajua umuhimu wako, japokuwa wewe unaangalia sana muda wako. Kumbuka; Mungu hajishughulishi na jambo lolote ambalo halijakamilika katika mtazamo wa neno lake [He is not God of Premature issues]. Kwetu sisi tunaweza kuona kwamba jambo hilo limeiva; lakini kwa Mungu laweza kuwa bado kabisa. Kutii neno lake na muda wake, ni vema kuliko kujali wakati wetu.

Wana wa Israeli walikaa utumwani Misri zaidi ya miaka 400. Inawezekana wako walioanza kuhuzunishwa na mateso waliyoyapata tangu siku ile walipoanza kutendewa vibaya. Lakini Mungu hakutoa hukumu kwa Farao na Wamisri kwa haraka. Mateso yalipozidi ndipo Mungu alimpomtafuta Musa ili kuwaokoa watu wake, kwa udhihirisho wa Nguvu kuu na ushuhuda mkuu.

Huwa natiwa moyo na maneno ya Henry Ward Beecher [1813-1887] anasema, “Our best successes often come after our greatest disappointments” yaani, “Mara nyingi, Mafanikio yetu makubwa hutokea baada ya kuhuzunishwa sana”. Israeli walipolia na kuhuzunishwa juu ya watesi wao ndipo BWANA aliposikia na kuwajilia kwa mkono wa Musa.

Mzaburi naye amewahi kusema, “Huenda kilio [huzuni] huja kukaa usiku [mmoja], Lakini asubuhi huwa furaha.”Zaburi 30:5 [Msisistizo umeongezwa]; akiwa na maana kwamba, picha pekee tunayoipata pale tuonapo giza limetanda sana ni kwamba asubuhi imekaribia. Hakuna muujiza kama hakuna changamoto; mambo kuonekana hayako sawa, bila ya magonjwa, kifo, kuachwa, kufukuzwa kazi na kuanguka; si tu kwamba hakuna muujiza bali ni wazi kusingelikuwepo hata na muujiza mmoja

Njia yetu inaweza kuwa si nyepesi; hata hivyo hatutakata tamaa katika kutenda mema. Endelea kupendeza, endelea kuvumilia, endelea kung’aa, endelea kuwa mtanashati kwa nje na hata kwa mapambo ya moyoni kwa maana asubuhi yako ii karibu.

Napenda ukweli huu toka kwa Mhubiri T.D Jakes, “Enjoy the journey not destination” akimaanisha, “Furahia safari yako na si hatima ya safari yako”. Furahia changamoto zako; zifanye changamoto zako kuwa ngazi ya kufikia mafanikio yako; changamoto ziwe chachu ya kujifunza zaidi, kumsogelea Mungu zaidi katika sala, na kukujengea mwenendo bora zaidi [character]; na endelea kufurahi katika Bwana.

Mpaka wiki Ijayo, Shalomu, amani!!!!

0 comments :

Umuhimu wa kutambua kusudi - III

3:02:00 PM Unknown 0 Comments

 
UMUHIMU WA KUTAMBUA KUSUDI III
Moyo wa mtu hufikiri njia yake; Bali Bwana huziongoza hatua zake” Mithali 16:9
Katika biblia tafasiri ya kiingereza [NIV] mithali 16:9 inasema, “Moyo wa mtu hupanga mipango yake ili kufikia malengo yake, lakini Bwana huongoza hatua zake” (Tafsiri ya mwandishi). Hii inatupa kufahamu kuwa jukumu la kupanga mipango ili kufikia malengo fulani katika maisha yetu ni jukumu la mtu binafsi. Mpaka tumekuwa na mipango dhabiti katika kufikia  malengo tuliyonayo, Mungu hataongoza hatua zetu ili kufikia malengo hayo.
Akielezea umuhimu wa kuwa na mipango, na jinsi ambavyo Mungu huongoza hatua zetu ili kufikia malengo, kutimia kwa ndoto/maono, katika maisha ya mtu; mwenyehekima mmoja amewahi kusema, “Ni vigumu kuongoza meli iliyosimama”. Mtu mwenye malengo au ndoto/maono katika maisha yake lakini hana mipango dhabiti ya kufikia jambo hilo, ni kama meli iliyosimama; hakuna namna nahodha ataweza kuiongoza meli hiyo; na hivyo hakuna namna meli hiyo itaweza kufika mwisho wa safari yake.
Jambo moja muhimu napenda ukumbuke; Kabla ya mipango hutangulia malengo. Malengo ni mambo unayotaka kuyafikia katika kipindi cha muda fulani; Mipango ni hatua na njia za kupita ili kufikia malengo hayo. Watu wengi wanashindwa kufanikiwa, si kwa sababu hawana uwezo wa kufanikiwa; ila ni kwa sababu hawajui wanataka kufanikiwa katika jambo gani hasa [specific targets]. Mtu asiye na malengo ni sawa na msafiri anaye safari kwenda mahali kusipojulikana. Mpaka umekuwa na malengo mahususi, hauwezi kuwa na mipango dhabiti ya kukutoa hapo ulipo.
Nakumbuka wakati ninaanza mwaka 2015, mojawapo ya malengo niliyokuwa nayo ni kuhakikisha ninasoma angalau kitabu kimoja kipya kila mwezi; na nikaweka mipango/mikakati ya kufikia lengo hilo. Mpaka mwaka unaisha nimefanikiwa kutimiza na kuvuka lengo hilo la kusoma angalau kitabu kipya kila mwezi; hii ni mbali na machapisho mbalimbali ninayosoma; ambapo kwa ujumla imeongeza maarifa, ufahamu, hekima na kupanua uelewa wangu juu ya mambo kadhaa.
Kumbuka jambo hili; Ili kuishi maisha yenye ufanisi, ni muhimu kwa malengo yako kuendana na ndoto zako au maono au kusudi la Mungu juu maisha yako.  Kama mojawapo ya  malengo yako katika mwaka huu ni kuongeza au kukuza uhusiano wako na Mungu, au kujijengea tabia na mwenendo fulani wa kimaisha au kurudi shule au kusoma hadi kufikia ngazi fulani, kuanzisha biashara/jambo fulani au kuboresha mahusiano yako katika eneo fulani; weka mipango ya kufikia lengo hilo.
Mipango ni kama malighafi za kutengenezea bidhaa [malengo], tunapoanza mwaka huu mpya amua kupanga mipango na kuiweka mipango hiyo mbele za Mungu; na mwisho wa yote utapata bidhaa kamili yaani kufikia malengo/ndoto na maono uliyonayo ndani yako kwa mwaka huu [Mithali 16:3].
Unapokuwa na malengo pamoja na mipango dhabiti; inakuwezesha kuweka vipaumbele vyako vizuri juu ya matumizi yako ya fedha, rasilimali ulizonazo, muda wako na aina ya watu unaotaka kutumia nao muda wako; kama mtu hakusaidii kufikia malengo yako ni vizuri ukapunguza matumizi ya muda wako kwake.
Kumbuka; watu wanaosafiri kwenda mahali kusikojulikana hupenda kusafiri pamoja na watu wengine; watu wasiotaka kufikia malengo yoyote katika maisha yao, hupenda kila mtu afanye kama wao.

0 comments :

Weka imani yako .......

9:36:00 AM Unknown 0 Comments

 
WEKA IMANI YAKO KATIKA KAZI TIMILIFU YA YESU KRISTO
Kwa maana yeye aliyeingia katika raha yake amestarehe mwenyewe katika kazi yake, kama vile Mungu alivyostarehe katika kazi zake…” Waebrania 4: 10
Kazi yote aliyofanya Kristo hapa duniani haikuwa kwa ajili yake mwenyewe, ilikuwa ni kwa ajili ya mimi na wewe. Alikufa ili sisi tupate kuwa hai, alichukua magonjwa yetu ili sisi tupate kufurahia afya na uzima wake katika maisha yetu. Amechukua huzuni, mahangaiko, masikitiko na mizigo yote katika maisha ili sisi tupate amani na kustarehe kwa kazi yake. Kazi zote alizifanya kwa ajili yetu ili sisi tupate kustarehe katika Yeye. Ikiwa Kristo amekufa msalabani kwa ajili ya dhambi zetu, sisi hatuwezi kufa tena; bali tutastarehe katika kazi yake.
Njia pekee ya sisi kuona na kufurahi matokeo ya utimilifu wa kazi ya Mungu katika maisha yetu ni imani, Tunapoamini juu ya kazi yake katika eneo fulani la maisha yetu ndipo hapo matokeo ya kazi hiyo hudhihirika. Ikiwa kuna jambo unahisi limekuwa mzigo kwako[burden] na kukuelemea katika maisha yako au familia, kazi zako au shughuli zako; mwaka huu unapoanza weka imani yako katika kazi timilifu ya Yesu Kristo na katika Ahadi ya Neno lake. Kumbuka, Tunaitwa katika raha ya Kristo kwa njia ya imani yetu katika kazi yake timilifu.  
Njoni kwangu, ninyi nyote msumbukao na wenye kulemewa na mizigo, nami nitawapumzisha” Mathayo 11:28
Unapoanza mwaka mpya, wito wetu kwako ni kwamba, jifunze kuweka imani yako katika kazi timilifu ya Yesu Kristo ili upate kuona Ukuu wa Mungu ukifunuliwa katika maisha yako ndani mwaka huu. Ikiwa amesema atafanya jambo fulani katika maisha yako, huna sababu ya kumsaidia kufanya kwa kuwa hofu au mahangaiko nafsini mwako; kazi yako ni moja tu kuingia katika raha yake na kustarehe huku ukijua kuwa Yeye anawajibika na maisha yako [Kutoka 14:14].
Maana Yeye alisema, ikiwa; Na Yeye aliamuru, ikasimama” Zaburi 33:9
Tunapoweka imani katika kazi yake na ahadi yake, tunauhakika ya kwamba kila kitu kipo katika mikono salama; hivyo hofu, mashaka, kuelemewa katika nafsi na mahangaiko hutoweka. Unapoanza mwaka huu, amua kwa dhati kuweka imani yako katika kazi timilifu na Ahadi yake, haijalishi mwaka jana hali ilikuwaje; kwa kuwa Bwana anafanya jambo jipya. Mazingira ya mwaka jana, yasikukwamishe kumuamini Mungu  katika mwaka huu mpya. Kumbuka jambo hili, Mungu anapotoa ahadi; kwake jambo hilo limeshakamilika. Na tunapoamini ahadi hiyo, haiwi tu upendeleo bali inakuwa haki yako kisheria [legal right].
Lakini akiiona ahadi ya Mungu hakusita kwa kutokuamini, bali alitiwa mguvu kwa imani, akimtukuza Mungu; huku akijua hakika ya kuwa Mungu aweza kufanya [kudhihirisha] yale aliyoahidi. Kwa hiyo ilihesabiwa kwake kuwa ni haki” Warumi4: 20-21 [Msisitizo umeongezwa]
Kazi ya Yesu Kristo haikulenga tu katika kuleta utimilifu wa roho ya mtu [anayeamini], lakini pia ililenga kuleta utimilifu wa nafsi, mwili na jamii yake; ili kurejesha hadhi ya Kimungu katika maisha ya mtu huyo na mazingira yake. Hivyo, unayohaki ya kumuamini Mungu ili Kazi zake, Ukuu wake na Uweza wake uweze kuwa dhahiri [kufunuliwa] katika maisha yako, familia, watoto, mipango, biashara, kazi, jamii au Taifa…nk. [Luka 4:18-19]
Ni nani aliyesadiki habari tuliyoileta? Na mkono wa Bwana amefunuliwa nani?” Isaya 53:1 
Katika mwaka huu mpya 2016, Mwenyezi Mungu akufadhili na kukuangazia Nuru ya uso wake.
Heri ya Mwaka Mpya 2016

0 comments :