Pasipo Msongo

5:13:00 PM Unknown 0 Comments

PASIPO MSONGO WA MAWAZO - I

[Stress Free Zone]
Katika maisha haya ya sasa watu wengi wanakabiriwa na maswali mengi; na wale wasio na maswali wana majawabu ya uongo yaani, ambayo si sahihi. Lini nitaajiriwa? Lini nitaolewa? Nitavaa nini? Nini itakuwa hatima ya maisha yangu? Ni miongoni mwa maswali tata katika kizazi chetu.
Kwa kuwa ukombozi wa Yesu Kristo unahusisha; mwili nafsi na roho hakuna namna tunavyoweza kuepuka kujibu maswali haya kama viongozi na watumishi katika Kristo. Kwa wanasiasa baadhi ya maswali haya ni mtaji wao wa kuwafikisha katika matarajio yao.
“Kila mmoja wetu anahitaji kuishi pasipo msongo/mgandamizo wa mawazo, pasipo moyo mzito; bila ya hofu wala mashaka yoyote.”
Kila mmoja wetu anahitaji kuishi pasipo msongo/mgandamizo wa mawazo, pasipo moyo mzito; bila ya hofu wala mashaka yoyote. Tunahitaji kuwa wepesi, tena tunapaswa kuwa wenye nguvu. Mt Francis De Sales amewahi kunukuliwa akisema: “Mtakatifu mwenye uso wa huzuni [asiye na furaha] ni mtakatifu bandia”
Moja ya kitu ninachokosa ninapozuru katika hoteli na maeneo mbali mbali ya huduma ni tabasamu. Watoa huduma wengi hawana tabasamu bashasha, wana uso unaonesha kwamba, maswali yao hayajajibiwa. Kwa nini ameniacha? Kwa nini nimepelekwa kule? Kwa nini mimi nimekosa? Kwa nini hajanitetea? Yote haya hupasua vichwa vya wengi.
Tuanze kujibu maswali haya ambayo huitwa pasua kichwa, tunatoa majibu ili uondokane na mganadamizo/msongo wa mawazo kwa kizungu, ‘stress’.
1.    Nitaweza kweli?
Mara nyingi tunakabiriwa na majukumu mazito na pengine tusiyoyaweza. Mara nyingi watu hujiuliza: nitaanzaje, nitasema nini mbele yao, nitamwambia nini, itakuwaje na watanionaje.  Nakumbuka siku yangu ya kwanza kazini nilijikuta katika wakati mgumu, nilitakiwa kufanya kila kitu cha uhasibu na hakukuwa na mtu wa kunielekeza. Stress nyingine husababishwa na kukabiliwa na tishio la majukumu mazito.
Katika Mithali 16:3 maandiko yanasema: Mkabidhi Bwana kazi zako, Na mawazo yako yatathibitika.” Biblia ya kiingereza inatumia neno, ‘roll’ yaani, kabidhi au achilia. Picha nzuri ni kama vile unapokuwa na kitu kizito cha duara au mviringo na kwa kuwa hauwezi kukibeba unaamua kukiachilia katika mteremko au mikononi mwa mwenye nguvu ili kiende haraka au ili akibeba na wewe ubaki huru. Hiyo ndio maana ya kumkabidhi, ni vema ujifunze kuviachilia na kuvisukuma [roll] vitu vyote vinavyokukabili ili kuondokana na mgandamizo wa mawazo. Visukume kuelekea mikononi mwa Mungu, yuko ili kukusaidia. Ni vizuri wewe ushindwe ili Mungu akuwezesha. Please roll!
“Muda huu unaposubiri ni kwa ajili ya faida ni ili kukuletea mema, kuna kitu kizuri Mungu anafanya wakati huu ambapo uko peka yako.”
2.   Nitaolewa lini na nani? Nitaoa lini, nitamuoa nani?
Kila kijana anapenda kupata kitu chema yaani, mke mwema na mume mwema. Nitakujibu kupitia historia yangu, siku moja nilipasua kichwa changu nikitafuta jibu la maswali haya. Nitamuoa nani na lini? Hatari mojawapo inayofutana na swali hili ni kujirahisisha siunajua usemi huu, “kwa mtu mwenye njaa hata sumu ni chakula.” Nikiwa nawaza niliamua kuomba, na katika sala Roho aliniambia taratibu mambo machache na moyo wangu ukalipuka kwa furaha. Alisema, “Jambo pekee ambalo Mungu angeweza kuwazuilia wanadamu (kuwanyima) ni kumtoa mwanaye wa pekee Yesu Krsito wala si mke mwema. Kwa kuwa alishamtoa Yesu pale msalabani hawezi kuacha kukupatia mke mwema.” Baadaye alinidokeza tena kwa kizungu, “everything works for good to them that love God” yaani, ‘Kila kitu kinafanya kazi ili kuwapatia mema wale wampendao Mungu.’ [Warumi 8:32]
Muda huu unaposubiri ni kwa ajili ya faida ni ili kukuletea mema, kuna kitu kizuri Mungu anafanya wakati huu ambapo uko peka yako. Wakati huu, kabla hujaolewa ni mwema na Mungu ana makusudi nao tafadhali furahi. 
Sala nzuri kwa mtu ambaye hajaoa au kuolewa ni ile inayomsaidia kujilewa na kuwaelewa watu wengine. Mithali hii ya kichina ni ya muhimu: “Seek to understand before seeking to be understood” Ni sala inayompa kijana nafasi ya kuvaa mavazi ya kiroho yaani, huruma, rehema, heshima, utakatifu, utu wema, fadhili na ibada {Waefeso 4:32}. Mpaka pale mtu anapovaa huruma, fadhili, na msamaha ndipo anaweza kuwa mtahiniwa sahihi wa ndoa [right candidate].
3.   Kwa nini nijishushe?
Changamoto nyingine ambayo ni pasua kichwa ni swala la unyenyekevu ambao wengi hudhani ni utumwa. Jambo hili limevunja mahusiano ya watu wengi katika ngazi mbalimbali, toka ofisini mpaka kwenye familia . Kwa mfano, kama umesoma uhasibu na siku moja ukafagia ofisi kitendo hicho hakikuondolei uhasibu wako. Tumezoea kuona watoto wakiwanawisha mikono wakubwa zao yaani, rika la juu; na ni utaratibu mzuri katika jamii zetu, tena ni wa kitambo. Siku moja baba mmoja aliamua kuacha kidogo utaratibu huu na akathubutu kuwanawisha mikono watoto wake wote. Na baada ya kumaliza kuwanawisha mikono na kuwafuta akawauliza swali, “Je, mmekuwa baba zangu?” wakajibu, “Hapana.”  Alitaka wajue soma hili la kunyenyekea, ukijishusha haikuondoi kwenye nafasi yako, badala yake inakupandisha zaidi. Alitaka wajue kwamba unyenyekevu hauwaondolei nafasi zao, baba atabaki kuwa baba hata kama ndiye atakayepika siku hiyo. Tusipojua hili tutaendelea kupigana, ni rahisi kusikia mtu akilaumu kwa maneno haya: huyu hana adabu, hajatoa vyombo, hajaniheshimu, anadhani tuko sawa. Yesu aliwaosha mitume miguu yao, na bado amebaki kuwa BWANA, MUNGU na MFALME. Kwa kutoa koti la nafasi zetu ndio tunaziimarisha zaidi wala hatutaondolewa. Mtu mmoja anasema, “Mambo ambayo nilikuwa nayafanya katika kazi ndogo, ndiyo niliyokutana nayo katika usaili wa kuelekea katika ofisi nyingine” Kukubali kwake kufanya kazi mahali penye hadhi ya kawaida ndio ilikuwa ngazi ya kumpeleka juu, tafadhali nyenyekea wala usidharau huo mwanzo mdogo.
“Neno linatukutaza kuisumbua kesho lakini halitukatazi kuwaza na kupanga kwa ajili ya mwisho wetu yaani, future.”
4.   Nini itakuwa hatima ya maisha yangu?
Mara nyingi tunawaza sana kuhusu hatima yetu na hivyo tunapoteza furaha ya sasa. Ibrahimu alikuwa anajikuta katika msongo wa mawazo kila alipowaza kuhusu hatima yake ya baadaye. Alikuwa mzee, tajiri na mwenye mafanikio mengi, lakini hukuwa na mtu atakayerithi hayo. Alikuwa anaumia, hakujua nani atarithi jina lake na mali zake. Alidhani ni Elieza mdamaskasi na kumbe ni Isaka. Usisahau mawazo mabaya huleta hoja au jawabu tofauti na mpango wa Mungu ambao ni amani. Neno linatukutaza kuisumbua kesho lakini halitukatazi kuwaza na kupanga kwa ajili ya mwisho wetu yaani, “future.” Kuna tofauti kati ya, tomorrow na future. Ukijipanga vizuri leo moja kwa moja kesho itakuwa nzuri lakini mwisho wako yaani, “future” itakuhitaji ujipange kila siku. Wengi kwa sababu ya kutokujua mwisho wa siku zetu tumejikuta katika msongo na mgandamizo wa mawazo. Ndio maana Mungu ameamua kututoa katika hali hiyo kwa neno lake: Maana nayajua mawazo ninayowawazia ninyi, asema Bwana, ni mawazo ya amani wala si ya mabaya, kuwapa ninyi tumaini siku zenu za mwisho.” Yeremia 29:11
Mawazo ni jambo la baadaye, huthibitika baada ya kitambo kupita. Mungu angeweza kuficha mawazo yake kwetu, lakini anayaweka wazi ili tusiwe na wasiwasi. Anataka tujue kwamba mambo yataenda vizuri yaani kila kitu viwili viwili [double-double]. Anasema ni mawazo ya amani. Mwanadiplomasia Helmet Coil amewahi kusema: “peace is more than absence of war.” Akimaanisha, “amani ni zaidi ya kutokuwepo/kukosekana kwa vita.” Amani maana yake, chakula cha kutosha, afya njema, fedha za kutosha, maji safi, familia nzuri, malazi mazuri na uhusiano mzuri na Mungu. Hii ndio amani anayotuwazia na anayotutamkia Mungu wetu, waipatao huwa kama mti uliopandwa kandokando ya maji.