Unayo Nafasi ........

4:29:00 PM Unknown 0 Comments

 

UNAYO NAFASI YA KUANDIKA
HISTORIA YAKO

Hatakama hatujui alipozikwa Nelson Mandela, Mama Teresa, Mwl. J. K. Nyerere, Dr. Myles Munroe; majina yao na kumbukumbu zao haziwezi kufutika; hatuhitaji kuona makaburi yako ili tujue kama wamewahi kuishi; kazi zao na michango yao juu ya ulimwengu ni alama tosha. Watu kama Mt. Paul, Moses, Joshua, Daudi hawakuhitaji msalaba wa chuma juu ya makaburi yao, wala hawakuhitaji kujengewa zege makaburi yao ili tujue kama wamewahi kupita hapa duniani; na tena hawahitaji majina yao kuwa juu ya majengo marefu; mahali ambapo tetemeko linaweza kuharibu. Kazi zao na mchango wao katika kuboresha maisha ya watu katika nyakati zao ni kaburi tosha; watu hawa wanaishi mioyoni mwetu; kwa kuwa kazi zao na kujitoa kwao kumerahisisha maisha yetu ya sasa, na kufanya ulimwengu kuwa bora zaidi.

Watu hawa walijua kuwa maisha yao ni dhamana, na kwamba mwanadamu anaishi mara moja; hivyo walihakikisha wanaishi katika ubora na ufanisi wote. Walijua kwanini wapo duniani katika nyakati zao; walijua wanawajibika kwa jamii zao na kwa vizazi vitakavyo kuja baada yao ambao wangehitaji kujenga juu ya msingi ambao ni mafanikio yao kama watangulizi; walitambua kuwa maisha yatakuwa na maana watakapoliishi kusudi la kuumbwa kwao kwa kuwa msaada kwa watu wengine. Wewe pia unayo nafasi ya kuandika historia yako, kalamu iko mkononi mwako.
Hata mimi sitaki jina langu liwekwe juu ya majengo na kaburi, mahali ambapo mafuriko na tetemeko vinaweza kuharibu na kufuta kabisa; na kumbukumbu yangu isiwepo tena; nataka jina langu na kumbukumbu yangu ibaki katika maisha ya wale niliowasaidia kufikia malengo [purpose] yao katika maisha; tetemeko na mafuriko halitaweza kuondoa kumbukumbu hiyo.
Watu wengi wanaogopa kufa kwa sababu hakuna jambo walilofanya duniani, linaloleta maana mbinguni. Rafiki yangu hupenda kusema, “Ulimwengu sio hifadhi ya wanyama, mahali ambapo hauruhusiwi hata kuacha ganda la pipi au ndizi”.
“ni katika kusudi la kuumbwa kwetu pekee ndipo tunaweza kuacha alama kwa kufanya jambo duniani litakalote maana mbinguni.”
Hivyo, kila mtu amekusudiwa kuacha alama [legacy] duniani itakayoleta maana Mbinguni. Na ni katika kusudi la kuumbwa kwetu pekee ndipo tunaweza kuacha alama kwa kufanya jambo duniani litakalote maana mbinguni.

Ninapoandika makala hii, moyoni mwangu najua, toleo hili sio la kila mtu; nashawishika kusema toleo hili ni maalumu ili kukuhamasisha na kukutia moyo wewe unaetaka kufanya jambo duniani litakaloleta maana mbinguni; toleo hili ni kwa ajili yako wewe unayetaka kuacha alama [legacy] na kuwa msaada kwa kizazi chako na vizazi vijavyo katika eneo la wito wako. Toleo hili ni kwa ajili yako wewe unayetamani kuishi sawa sawa na kusudi la Mungu katika maisha yako; ni kwa ajili yako wewe ambaye ndani ya moyo wako unatakama kusahihisha historia, kwamba katika dunia hii, amewahi kuwepo mtu aliyeishi na kutimiza kusudi la Mungu juu ya kuumbwa kwake. Hatutaki vizazi vijavyo wafikiri kuwa katika kizazi hiki waliishi mafisadi tu, wala rushwa tu, wafanyabiashara wasio waadilifu tu, wanasiasa wanaotumia nafasi zao vibaya tu, wanyonyaji tu wasiojali wengine; au viongozi wasioweza kusimamia yaliyo sahihi tu.

Usisubiri uwe kila kitu ili ufanye kitu


Mama Teresa hakuwa na fedha alipoanza kuwasaidia masikini kule India; alijua kamwe hawezi kuwafikia masikini wote na kuwapatia huduma muhimu katika maisha yao; hii haikumkatisha tamaa, alianza na mmoja. Huitaji kuwa millionea ili ujifunze kutoa, huitaji kuwa Bill Gate ili kusaidia muhitaji aliyekaribu nawe; Hauhitaji uwe Mwakasege ili utangaze habari njema ya Ufalme wa Mungu. Mother Teresa alianza na mtu mmoja, leo hii ulimwengu mzima unazungumza habari zake; binafsi sijui kaburi lake lilipo lakini naijua na kutambua kazi yake katika kuboresha maisha ya wengine.

Wanatheologia na wataalamu wa maandiko ya kale wanadai ni Veronica, aliyemfuta Yesu uso wakati akielekea msalabani; inawezekana, kama ni mimi ningekuwa mwandishi kwa wakati ule, nisingeandika tukio hili, inawezekana ningeandika miujiza ya Yesu tu zaidi;
“Hauhitaji kuwa mtu fulani ili uache alama; unahitaji kuwa wewe tu ili kuacha alama duniani, itakayoleta maana Mbinguni.”
Lakini Roho Mtakatifu alihakikisha jambo hili linaandikwa ili kutupa kujua kwamba haijalishi kitu tunachokifanya kinaonekana kuwa kidogo namna gani na kwamba hakuna mtu anaonekana kujali sana wala hakuna mwandishi aliyeandika habari hiyo, Kitu hicho Mbinguni hawawezi kusahau. Maria Magdalena alimfuta Yesu miguu kwa nywele zake, kila mtu aliyekuwa pale alisema alichoweza kusema juu ya kitendo kile, Lakini hakukatishwa tamaa kwa maneno yao; Na Yesu alisema kitendo kile kitajulikana duniani kwote; hata leo tunaposoma, tunatimiza unabii huo [Mathayo 26:7-13]

Hauhitaji kuwa mtu fulani ili uache alama; unahitaji kuwa wewe tu ili kuacha alama duniani, itakayoleta maana Mbinguni. Fanya unachoweza kufanya mahali ulipo. Usisubiri uwe kila kitu ili ufanye kitu; anza na unachoweza kufanya mahali unapoweza kufanya. Usisubiri uwe Mwakasege wa pili, Bill Gate wa pili. au mama Tereza wa pili.  Kama mtu anahitaji kutiwa moyo, fanya hivyo sasa, kama mtu anahitaji ushauri au msaada ili kufikia mafanikio yake, na unaweza kufanya hata jambo dogo, lifanye;
“Kama unaona kuna uhitaji mahali na unaweza kufanya jambo juu ya uhitaji huo, fanya; usisubiri uwe na kila kitu au uwe kila kitu.”
Kama unaona kuna uhitaji mahali na unaweza kufanya jambo juu ya uhitaji huo, fanya; usisubiri uwe na kila kitu au uwe kila kitu. Mwenyehekima mmoja amewahi kusema, “Tunapowasaidia wengine kupata wanayoyahitaji, ndipo na sisi tutapata tunayoyahitaka” [Luka 6:38a]
See you at the top

0 comments :