Umuhimu wa kutambua ........

2:10:00 PM Unknown 0 Comments

 
UMUHIMU WA KUTAMBUA VIPAUMBELE KWA WAKATI
(Nioneshe vipaumbele vyako; nikuoneshe hatima yako)
Watu wengi hawafanikiwi si kwa sababu hawana uwezo wa kufanikiwa; bali, ni kwa sababu hawafanyi mambo yatakayowaletea mafanikio. Ile kwamba mtu hajafanikiwa haina maana mtu huyo hana uwezo wa kufanikiwa; bali ni kwa sababu mtu huyo hafanyi au hajafanya mambo yatakayomletea mafanikio.
Mafanikio katika ufalme wa Mungu sio mchezo wa bahati nasibu (lottery) au mchezo jackpot bingo bali ni matokeo ya utendaji kazi wa kanuni (principles) zilizopo katika neno la Mungu, kwa eneo husika na muda husika; kwa mfano; hata ukifunga na kulia mbegu ya mti iliyowekwa sakafuni haiwezi kuota na kufikia kuwa mti, unahitaji kuiweka katika kanuni ya mazingira na hali ya hewa sahihi ili iweze kuota (The principle of an environment). Kuongeza au kupunguza, katika utekelezaji wa kanuni yoyote huathiri matokeo yaliokusudiwa katika eneo husika.

Kanuni ya kuishi kwa kuweka vipaumbele (principle of priority)

Kanuni mojawapo inayoweza kukuhakikishia mafanikio katika maisha, ni uwezo wa kutambua na kuweka vipaumbele katika maisha ya kila siku; uwezo wa kutambua mambo ya msingi yanayotakiwa kupewa kipaumbele kwa wakati; hasa katika utekelezaji kabla ya jambo lingine lolote. Vipaumbele hutusaidia kuzingatia mambo yaliyo muhimu na yenye kufaa kwa wakati husika, hutusaidia kutokupoteza rasilimali katika mambo yasiyo ya msingi au muhimu.
Vipaumbele maana yake vitu vifaavyo sasa na muhimu, vitu vya kuwekwa kwanza kabla ya vingine, vitu vya kuwekwa mbele ya vingine katika mgawanyo na matumizi ya rasilimali muda na rasilimali nyingine; vipaumbele ni vitu au jambo lililo bora kwako kwa wakati huu kuliko mengine, uko tayari vingine vipotee ili kupata na kulinda kipaumbele chako.

Vipaumbele huendana na muda.

Jambo la kwanza sasa ukiliweka la kwanza kesho hutapata matokeo yaliyo bora (Mhubiri 3:1, 11a). Wanaisraeli walipata shida katika hali zao za uchumi kwa sababu ya kushindwa kuzingatia muda katika kuweka vipaumbele vyao; walipotakiwa kutoa sadaka na kujenga Nyumba ya BWANA wao walisema huu sio wakati na hivyo iliathiri hali yao ya kiuchumi na kimaisha (Hagai 1:2, 4).
Ndio maana biblia imeweka msingi wa vipaumbele kwa vijana katika muda wao wa ujana ili watumie muda wao huo kwa kujenga uhusiano bora na Mungu na kumtumikia kabla ya siku za uzee wao (mhu12:1). Hiki ni kipaumbele muhimu kuliko vyote unavyoweza kuwa navyo.
Mtu asiyetambua  nini ni kipaumbele kwa wakati husika, ni sawa na meli isiyokuwa na uelekeo katikati ya bahari. Vipaumbele vinasaidia kujua ufanye/usifanye nini kwa wakati huu; inakupa kujua njia (dira) sahihi ili kufikia malengo yako. Mtu asiyekuwa na vipaumbele ni sawa na mtu asiyejua njia. Mtu huyu hawezi kupotea njia, anaweza kufika anapotakiwa kufika na asijue kama amefika. What a waste!!
Ukiamka asubihi Tv inataka uingalie muda wote; Redio inataka uisikilize, hakuna muda watazima mitambo yao ili wakupe nafasi ya kufanya mambo yako mengine; masaa 24 wanarusha matangazo; simu inataka uchat muda wote; marafiki wanataka mkae masaa sita mpige stori tu. Magazeti yanataka uyasome, bado majukumu ya shule kama ni mwanafunzi au ofisi kama ni  mfanyakazi au mfanyabiashara. Kila kitu kinataka kutumia muda wako; usipojua nini kianze na nini kifuate; niulize, nami nitakuambia mwisho wako. Nioneshe vipaumbele vyako; nikuoneshe hatima yako.

Kipaumbele cha kwanza kuliko vyote unavyoweza kuwa navyo.

Kipaumbele cha kwanza ili kufanikiwa ni kuwa na uhusiano binafsi na Mungu (daily communion). Daudi alitafuta neno moja tu nalo ni kukaa nyumbani mwa BWANA. Mafanikio halisi huanza na Mungu mwenyewe. Maisha ya mwanadamu Huanza, Hukamilika na Kupata maana katika Mungu pekee; uhusiano huu ni zaidi ya kwenda kanisani jumapili, ni zaidi ya kwenda kwenye kikundi cha sala; ni kutamani kukaa katika uwepo wake Muda wote, kuzijua njia zake, kuungana naye na kushikamana naye katika Neno lake katika maisha yetu ya kila siku.
“Neno moja nimelitaka kwa BWANA, Nikae nyumbani mwa BWANA siku zote za maisha yangu. Niutazame uzuri wa BWANA, na kutafakari hekaluni mwake” Zab 27:4
Mwandishi wa kitabu cha ‘Momentary marriage’, John Piper amewahi kuandika jambo kuhusu umuhimu wa vipaumbele kwa kusema, “kuweka jambo la kwanza kuwa la kwanza, hufanya jambo la pili kuwa bora zaidi” (keeping first things first, makes second things better). Hivyo kuweka jambo la kwanza kuwa la pili huathiri matokeo ya mambo yote katika hali zote.
 “…Bwana akajibu akamwambia… Martha, unasumbuka na kufadhaika kwa ajili ya vitu vingi; lakini kinatakiwa kitu kimoja; na Mariamu amelichagua fungu lililo jema, ambalo hataondolewa” Luka 10:39-42
Kipaumbele cha Mariamu ilikuwa ni jambo moja tu ambalo lililokuwa linatakiwa kwa wakati huo, nalo ni kukaa miguuni pa Yesu ili apate kusikiliza maarifa yatakayompa ufahamu na hekima katika maisha. Kipaumbele hakikua katika kufanya kazi bali kukaa na kumsikiliza kwanza mwenye kazi. Ndio maana Mfalme Daudi alitaka kukaa nyumbani mwa BWANA siku zote apate kuutazama uzuri wa BWANA na kutafakari (meditate) Neno hekaluni mwake na hivyo alipata hekima iliyomsaidia kujua namna ya kuishi ili kufikia mafanikio katika maisha yake; si ajabu ni miongoni mwa wafalme waliofanikiwa sana katika nyakati zao (zab119:97-98, 104).
Ni muhimu kukumbuka kuwa, Maisha ya mwanadamu ni kama kitabu, kwa jinsi anavyokaa na Mungu ndivyo kinavyozidi kufunguka kurasa hadi kurasa. Unaposhindwa kutambua vipaumbele kwa wakati, maisha yanakuwa hayana ladha, yanabeba mafadhaiko, kulaumu wengine na masumbufu ya kila namna; kwa sababu kuweka jambo la kwanza kuwa la pili huathiri matokeo ya mambo yote katika hali zote.

Tujifunze kwa Nehemia

Usipokuwa na vipaumbele, hauwezi kusema hapana kwa mambo yanayoonekana kuwa mazuri (good) ili kuyafikia yaliyo bora (best). Nehemia wakati ameanza kazi ya ujenzi wa ukuta wa Yerusalemu uliokuwa umebomolewa, alijua kipaumbele kwa wakati ule ni kazi iliyokuwa mbele yake, hakukubali kuyumbishwa na jambo lingine lolote. Usipojua nini unatakiwa kufanya kwa wakati husika, utafanya kila kitu na kujitahidi kuwa kila kitu (committed in the wrong things).
Sanbalati na Geshemu wakatuma wajumbe kwangu, wakasema, Njoo, tukutane huko vijijini katika nchi tambarare ya Ono… Na mimi nikatuma wajumbe kwao, nikasema, Hii ni kazi kubwa ninayoifanya mimi, hata nisiweze kushuka; mbona kazi ikome, hapo ninapoiacha, niwashukie? Nao wakaniletea maneno hayo mara nne, nikawajibu maneno kama yale…” Nehemia 6:2-5
Iwe ni mfanyakazi, mwanafunzi, mzazi au mlezi ni muhimu kutambua na kuzingatia vipaumbele katika kila eneo muhimu la maisha yako kwa wakati; vipaumbele vyako ndivyo vitakavyoamua uelekeo wako na hatima yako, ni muhimu kujizoeza kutenga muda mara kwa mara na kujiuliza ni nini kipaumbele, nini kianze na nini kifuate iwe kwa mambo ya ofisi, biashara, shuleni au nyumbani;
“If you don’t know where you are going, any way can take you there”

0 comments :