Mtu Mwaminifu

5:04:00 PM Unknown 0 Comments

 
 MTU MWAMINIFU
(Tujifunze kwa nabii Samweli)
Ukuaji wa tabia ni mchakato, sawa na ukuaji wa mwili. Mwili hupokea chakula kwa kupitia mdomo bali tabia hujengwa kupitia milango ya fahamu kama vile, macho na masikio. Tuonacho sana na kusikia sana hugeuka kuwa tabia yetu. Leo tunatamani usikie kuhusu Samweli ili tabia yake iwe tabia yako.
Samweli alikuwa kiongozi mwaminifu katika ofisi yake. Tunahitaji kuwa watu waaminifu katika mazingira yasiyo aminika. Mtu asiye mwaminifu hawezi kumudu mazingira korofi, yaani: umasikini, vishawishi na mivuto ya kidunia. Mtu mwaminifu anaaminika hata kama mazingira hayaaminiki, asiyemwaminifu haaminiki hata katika mazingira salama. Leo hii kuna nakisi ya watu waaminifu. Hatuna upungufu wa watendaji bali tunaupungufu wa watendaji waaminifu; hatuna upungufu wa wanasheria, bali tunaupungufu wa wanasheria waaminifu; hatuna upungufu wa wanasiasa bali tunaupungufu wa wanasiasa waaminifu. 
“Mtu mwaminifu anaaminika hata kama mazingira hayaaminiki, asiyemwaminifu haaminiki hata katika mazingira salama”

Uaminifu si hamasa au shauku ya siku moja, uaminifu ni tabia inayojengwa na kujengeka ndani ya mtu.  Uaminifu ni tunda la Roho (Gal 5:22), tunda halikomai na kuiva kwa siku moja, huchukua muda. Uaminifu ni uwezo wa kujifuata mwenyewe. Lazima tuweze kujifuata na kujiongoza wenyewe. Mitume pasipo Yesu, nasi pasipo mitume.
Nabii aishi katika uaminifu wa kinabii, baba wa familia na atimize wajibu wake kwa uaminifu na mwalimu ashike maadili yake. Jaji na afuate hadhi  ya ofisi yake. Kama umeitwa kumwimbia Mungu basi jifuate mwenyewe, usiwe mwimbaji wa nyimbo za dini lakini unapendelea kusikiliza taarabu ukiwa gizani.  Kama umeitwa kuwa mchungaji jifuate pia yaani, tabia yako ifanane na ofisi yako.

“kiongozi ni mtu mwenye kuijua njia, anayepita hiyo njia na anayeonesha wengine namna ya kupita njia hiyo.”
Samweli alikuwa mwaminifu alitenda kile alichosema; imani yake ndiyo ilikuwa tabia yake na huo ndio huitwa uaminifu. Lissy M. ameandika maneno haya katika kijitabu chake cha mafanikio, “kiongozi ni mtu mwenye kuijua njia, anayepita hiyo njia na anayeonesha wengine namna ya kupita njia hiyo.” 

Samweli alianza vizuri na kumaliza vizuri, ni mfano wa kuigwa. Alipowahutubia Israeli hotuba yake kuelekea mwisho wa uongozi wake hakupatikana mtu aliyeona dosari katika maisha yote ya Samweli. Samweli alihoji kama yuko mtu mwenye kumdai chochote na hakupatikana mtu awaye yote. Samweli hakuiba, hakuchukua rushwa, hakupotosha hukumu, wala hakujitia katika uchafu wowote. Samweli ni kiongozi mwenye karatasi safi yaani, clean sheet!1 Samweli12:3

Hata baada ya Samweli kuwaambia mkutano wa Israeli washuhudie kama kuna kosa au dosari yoyote aliyofanya katika huduma yake kama kiongozi wao, mkutano ulithibitisha  kwamba, hakuna tatizo lolote katika maisha yote ya Samweli tangu utoto hata utu uzima wake. Samweli ni mfano wa kuigwa kwa utumishi uliotukuka katika ofisi yake. 

Nani katika viongozi wa leo wa kiroho na hata ki-siasa atathubutu kugawa karatasi nyakati za mwisho wa muhula wa uongozi wake ili wananchi wamtathimini? Samweli alitenda hivyo na alimaliza vizuri, bila ya lawana wala bila ya kulitukanisha jina la BWANA Mungu wake. Uaminifu ni bidhaa adimu, kufuzu na kupata vyeti vya bodi kama vile; CPA(T), ACCA, PSPTB, bodi ya wakandarasi hata shule ya sheria haitawezesha upatikanaji wa watu waaminifu hadi wataalamu hawa wahusiane na Muumba wao. Ndivyo ilivyotokea kwa Zakayo mtoza ushuru.

Kilele cha tabia njema ni kufanana na Yesu (1Yohana 4:17b). Hatuwezi kusema tumefika au tumekamilika kitabia mpaka pale tutakapofanana na Yesu, kama hatujafikia hapo, basi tunapaswa kukaza mwendo kuendelea na safari yetu ya ukuaji kuelekea mwenendo bora.
Kwa kweli hakuna njia ya mkato, Christ likeness should be the summit of our good character!

0 comments :