Nguvu Zako ni Kidogo ..........

2:52:00 PM Unknown 0 Comments

 

NGUVU ZAKO NI KIDOGO, UNAMUHITAJI MUNGU
Nawapenda watu wanaotia moyo na kusisimua wengine, ingawa baadhi yao ni watu hatari. Naziogopa baadhi ya kauli zao, ndio maana mara zote husoma vitabu vyao kwa umakini mkubwa. Watia moyo wengi (motivators/inspirational speakers) humwondoa Mungu katika mahubiri yao, huwaaminisha watu katika uwezo wa akili na fikra chanya tu (positive thinking). Nimewahi kusoma kauli ya zamani kidogo ya mtu aliyejulikana kama kiongozi wa haki za wanawake, nikaogopa sana. Amenukuliwa hivi: “Ifikapo mwaka 2000 natumaini tutawalea watoto wetu kuamini katika uwezo wa kibinadamu, na si Mungu” Gloria Steinem, Mhariri wa Ms. Magazine.

0 comments :

Unayo Nafasi ........

4:29:00 PM Unknown 0 Comments

 

UNAYO NAFASI YA KUANDIKA
HISTORIA YAKO

Hatakama hatujui alipozikwa Nelson Mandela, Mama Teresa, Mwl. J. K. Nyerere, Dr. Myles Munroe; majina yao na kumbukumbu zao haziwezi kufutika; hatuhitaji kuona makaburi yako ili tujue kama wamewahi kuishi; kazi zao na michango yao juu ya ulimwengu ni alama tosha. Watu kama Mt. Paul, Moses, Joshua, Daudi hawakuhitaji msalaba wa chuma juu ya makaburi yao, wala hawakuhitaji kujengewa zege makaburi yao ili tujue kama wamewahi kupita hapa duniani; na tena hawahitaji majina yao kuwa juu ya majengo marefu; mahali ambapo tetemeko linaweza kuharibu. Kazi zao na mchango wao katika kuboresha maisha ya watu katika nyakati zao ni kaburi tosha; watu hawa wanaishi mioyoni mwetu; kwa kuwa kazi zao na kujitoa kwao kumerahisisha maisha yetu ya sasa, na kufanya ulimwengu kuwa bora zaidi.

Watu hawa walijua kuwa maisha yao ni dhamana, na kwamba mwanadamu anaishi mara moja; hivyo walihakikisha wanaishi katika ubora na ufanisi wote. Walijua kwanini wapo duniani katika nyakati zao; walijua wanawajibika kwa jamii zao na kwa vizazi vitakavyo kuja baada yao ambao wangehitaji kujenga juu ya msingi ambao ni mafanikio yao kama watangulizi; walitambua kuwa maisha yatakuwa na maana watakapoliishi kusudi la kuumbwa kwao kwa kuwa msaada kwa watu wengine. Wewe pia unayo nafasi ya kuandika historia yako, kalamu iko mkononi mwako.
Hata mimi sitaki jina langu liwekwe juu ya majengo na kaburi, mahali ambapo mafuriko na tetemeko vinaweza kuharibu na kufuta kabisa; na kumbukumbu yangu isiwepo tena; nataka jina langu na kumbukumbu yangu ibaki katika maisha ya wale niliowasaidia kufikia malengo [purpose] yao katika maisha; tetemeko na mafuriko halitaweza kuondoa kumbukumbu hiyo.
Watu wengi wanaogopa kufa kwa sababu hakuna jambo walilofanya duniani, linaloleta maana mbinguni. Rafiki yangu hupenda kusema, “Ulimwengu sio hifadhi ya wanyama, mahali ambapo hauruhusiwi hata kuacha ganda la pipi au ndizi”.
“ni katika kusudi la kuumbwa kwetu pekee ndipo tunaweza kuacha alama kwa kufanya jambo duniani litakalote maana mbinguni.”
Hivyo, kila mtu amekusudiwa kuacha alama [legacy] duniani itakayoleta maana Mbinguni. Na ni katika kusudi la kuumbwa kwetu pekee ndipo tunaweza kuacha alama kwa kufanya jambo duniani litakalote maana mbinguni.

Ninapoandika makala hii, moyoni mwangu najua, toleo hili sio la kila mtu; nashawishika kusema toleo hili ni maalumu ili kukuhamasisha na kukutia moyo wewe unaetaka kufanya jambo duniani litakaloleta maana mbinguni; toleo hili ni kwa ajili yako wewe unayetaka kuacha alama [legacy] na kuwa msaada kwa kizazi chako na vizazi vijavyo katika eneo la wito wako. Toleo hili ni kwa ajili yako wewe unayetamani kuishi sawa sawa na kusudi la Mungu katika maisha yako; ni kwa ajili yako wewe ambaye ndani ya moyo wako unatakama kusahihisha historia, kwamba katika dunia hii, amewahi kuwepo mtu aliyeishi na kutimiza kusudi la Mungu juu ya kuumbwa kwake. Hatutaki vizazi vijavyo wafikiri kuwa katika kizazi hiki waliishi mafisadi tu, wala rushwa tu, wafanyabiashara wasio waadilifu tu, wanasiasa wanaotumia nafasi zao vibaya tu, wanyonyaji tu wasiojali wengine; au viongozi wasioweza kusimamia yaliyo sahihi tu.

Usisubiri uwe kila kitu ili ufanye kitu


Mama Teresa hakuwa na fedha alipoanza kuwasaidia masikini kule India; alijua kamwe hawezi kuwafikia masikini wote na kuwapatia huduma muhimu katika maisha yao; hii haikumkatisha tamaa, alianza na mmoja. Huitaji kuwa millionea ili ujifunze kutoa, huitaji kuwa Bill Gate ili kusaidia muhitaji aliyekaribu nawe; Hauhitaji uwe Mwakasege ili utangaze habari njema ya Ufalme wa Mungu. Mother Teresa alianza na mtu mmoja, leo hii ulimwengu mzima unazungumza habari zake; binafsi sijui kaburi lake lilipo lakini naijua na kutambua kazi yake katika kuboresha maisha ya wengine.

Wanatheologia na wataalamu wa maandiko ya kale wanadai ni Veronica, aliyemfuta Yesu uso wakati akielekea msalabani; inawezekana, kama ni mimi ningekuwa mwandishi kwa wakati ule, nisingeandika tukio hili, inawezekana ningeandika miujiza ya Yesu tu zaidi;
“Hauhitaji kuwa mtu fulani ili uache alama; unahitaji kuwa wewe tu ili kuacha alama duniani, itakayoleta maana Mbinguni.”
Lakini Roho Mtakatifu alihakikisha jambo hili linaandikwa ili kutupa kujua kwamba haijalishi kitu tunachokifanya kinaonekana kuwa kidogo namna gani na kwamba hakuna mtu anaonekana kujali sana wala hakuna mwandishi aliyeandika habari hiyo, Kitu hicho Mbinguni hawawezi kusahau. Maria Magdalena alimfuta Yesu miguu kwa nywele zake, kila mtu aliyekuwa pale alisema alichoweza kusema juu ya kitendo kile, Lakini hakukatishwa tamaa kwa maneno yao; Na Yesu alisema kitendo kile kitajulikana duniani kwote; hata leo tunaposoma, tunatimiza unabii huo [Mathayo 26:7-13]

Hauhitaji kuwa mtu fulani ili uache alama; unahitaji kuwa wewe tu ili kuacha alama duniani, itakayoleta maana Mbinguni. Fanya unachoweza kufanya mahali ulipo. Usisubiri uwe kila kitu ili ufanye kitu; anza na unachoweza kufanya mahali unapoweza kufanya. Usisubiri uwe Mwakasege wa pili, Bill Gate wa pili. au mama Tereza wa pili.  Kama mtu anahitaji kutiwa moyo, fanya hivyo sasa, kama mtu anahitaji ushauri au msaada ili kufikia mafanikio yake, na unaweza kufanya hata jambo dogo, lifanye;
“Kama unaona kuna uhitaji mahali na unaweza kufanya jambo juu ya uhitaji huo, fanya; usisubiri uwe na kila kitu au uwe kila kitu.”
Kama unaona kuna uhitaji mahali na unaweza kufanya jambo juu ya uhitaji huo, fanya; usisubiri uwe na kila kitu au uwe kila kitu. Mwenyehekima mmoja amewahi kusema, “Tunapowasaidia wengine kupata wanayoyahitaji, ndipo na sisi tutapata tunayoyahitaka” [Luka 6:38a]
See you at the top

0 comments :

Mtu Mwaminifu

5:04:00 PM Unknown 0 Comments

 
 MTU MWAMINIFU
(Tujifunze kwa nabii Samweli)
Ukuaji wa tabia ni mchakato, sawa na ukuaji wa mwili. Mwili hupokea chakula kwa kupitia mdomo bali tabia hujengwa kupitia milango ya fahamu kama vile, macho na masikio. Tuonacho sana na kusikia sana hugeuka kuwa tabia yetu. Leo tunatamani usikie kuhusu Samweli ili tabia yake iwe tabia yako.
Samweli alikuwa kiongozi mwaminifu katika ofisi yake. Tunahitaji kuwa watu waaminifu katika mazingira yasiyo aminika. Mtu asiye mwaminifu hawezi kumudu mazingira korofi, yaani: umasikini, vishawishi na mivuto ya kidunia. Mtu mwaminifu anaaminika hata kama mazingira hayaaminiki, asiyemwaminifu haaminiki hata katika mazingira salama. Leo hii kuna nakisi ya watu waaminifu. Hatuna upungufu wa watendaji bali tunaupungufu wa watendaji waaminifu; hatuna upungufu wa wanasheria, bali tunaupungufu wa wanasheria waaminifu; hatuna upungufu wa wanasiasa bali tunaupungufu wa wanasiasa waaminifu. 
“Mtu mwaminifu anaaminika hata kama mazingira hayaaminiki, asiyemwaminifu haaminiki hata katika mazingira salama”

Uaminifu si hamasa au shauku ya siku moja, uaminifu ni tabia inayojengwa na kujengeka ndani ya mtu.  Uaminifu ni tunda la Roho (Gal 5:22), tunda halikomai na kuiva kwa siku moja, huchukua muda. Uaminifu ni uwezo wa kujifuata mwenyewe. Lazima tuweze kujifuata na kujiongoza wenyewe. Mitume pasipo Yesu, nasi pasipo mitume.
Nabii aishi katika uaminifu wa kinabii, baba wa familia na atimize wajibu wake kwa uaminifu na mwalimu ashike maadili yake. Jaji na afuate hadhi  ya ofisi yake. Kama umeitwa kumwimbia Mungu basi jifuate mwenyewe, usiwe mwimbaji wa nyimbo za dini lakini unapendelea kusikiliza taarabu ukiwa gizani.  Kama umeitwa kuwa mchungaji jifuate pia yaani, tabia yako ifanane na ofisi yako.

“kiongozi ni mtu mwenye kuijua njia, anayepita hiyo njia na anayeonesha wengine namna ya kupita njia hiyo.”
Samweli alikuwa mwaminifu alitenda kile alichosema; imani yake ndiyo ilikuwa tabia yake na huo ndio huitwa uaminifu. Lissy M. ameandika maneno haya katika kijitabu chake cha mafanikio, “kiongozi ni mtu mwenye kuijua njia, anayepita hiyo njia na anayeonesha wengine namna ya kupita njia hiyo.” 

Samweli alianza vizuri na kumaliza vizuri, ni mfano wa kuigwa. Alipowahutubia Israeli hotuba yake kuelekea mwisho wa uongozi wake hakupatikana mtu aliyeona dosari katika maisha yote ya Samweli. Samweli alihoji kama yuko mtu mwenye kumdai chochote na hakupatikana mtu awaye yote. Samweli hakuiba, hakuchukua rushwa, hakupotosha hukumu, wala hakujitia katika uchafu wowote. Samweli ni kiongozi mwenye karatasi safi yaani, clean sheet!1 Samweli12:3

Hata baada ya Samweli kuwaambia mkutano wa Israeli washuhudie kama kuna kosa au dosari yoyote aliyofanya katika huduma yake kama kiongozi wao, mkutano ulithibitisha  kwamba, hakuna tatizo lolote katika maisha yote ya Samweli tangu utoto hata utu uzima wake. Samweli ni mfano wa kuigwa kwa utumishi uliotukuka katika ofisi yake. 

Nani katika viongozi wa leo wa kiroho na hata ki-siasa atathubutu kugawa karatasi nyakati za mwisho wa muhula wa uongozi wake ili wananchi wamtathimini? Samweli alitenda hivyo na alimaliza vizuri, bila ya lawana wala bila ya kulitukanisha jina la BWANA Mungu wake. Uaminifu ni bidhaa adimu, kufuzu na kupata vyeti vya bodi kama vile; CPA(T), ACCA, PSPTB, bodi ya wakandarasi hata shule ya sheria haitawezesha upatikanaji wa watu waaminifu hadi wataalamu hawa wahusiane na Muumba wao. Ndivyo ilivyotokea kwa Zakayo mtoza ushuru.

Kilele cha tabia njema ni kufanana na Yesu (1Yohana 4:17b). Hatuwezi kusema tumefika au tumekamilika kitabia mpaka pale tutakapofanana na Yesu, kama hatujafikia hapo, basi tunapaswa kukaza mwendo kuendelea na safari yetu ya ukuaji kuelekea mwenendo bora.
Kwa kweli hakuna njia ya mkato, Christ likeness should be the summit of our good character!

0 comments :

Umuhimu wa kutambua ........

2:10:00 PM Unknown 0 Comments

 
UMUHIMU WA KUTAMBUA VIPAUMBELE KWA WAKATI
(Nioneshe vipaumbele vyako; nikuoneshe hatima yako)
Watu wengi hawafanikiwi si kwa sababu hawana uwezo wa kufanikiwa; bali, ni kwa sababu hawafanyi mambo yatakayowaletea mafanikio. Ile kwamba mtu hajafanikiwa haina maana mtu huyo hana uwezo wa kufanikiwa; bali ni kwa sababu mtu huyo hafanyi au hajafanya mambo yatakayomletea mafanikio.
Mafanikio katika ufalme wa Mungu sio mchezo wa bahati nasibu (lottery) au mchezo jackpot bingo bali ni matokeo ya utendaji kazi wa kanuni (principles) zilizopo katika neno la Mungu, kwa eneo husika na muda husika; kwa mfano; hata ukifunga na kulia mbegu ya mti iliyowekwa sakafuni haiwezi kuota na kufikia kuwa mti, unahitaji kuiweka katika kanuni ya mazingira na hali ya hewa sahihi ili iweze kuota (The principle of an environment). Kuongeza au kupunguza, katika utekelezaji wa kanuni yoyote huathiri matokeo yaliokusudiwa katika eneo husika.

Kanuni ya kuishi kwa kuweka vipaumbele (principle of priority)

Kanuni mojawapo inayoweza kukuhakikishia mafanikio katika maisha, ni uwezo wa kutambua na kuweka vipaumbele katika maisha ya kila siku; uwezo wa kutambua mambo ya msingi yanayotakiwa kupewa kipaumbele kwa wakati; hasa katika utekelezaji kabla ya jambo lingine lolote. Vipaumbele hutusaidia kuzingatia mambo yaliyo muhimu na yenye kufaa kwa wakati husika, hutusaidia kutokupoteza rasilimali katika mambo yasiyo ya msingi au muhimu.
Vipaumbele maana yake vitu vifaavyo sasa na muhimu, vitu vya kuwekwa kwanza kabla ya vingine, vitu vya kuwekwa mbele ya vingine katika mgawanyo na matumizi ya rasilimali muda na rasilimali nyingine; vipaumbele ni vitu au jambo lililo bora kwako kwa wakati huu kuliko mengine, uko tayari vingine vipotee ili kupata na kulinda kipaumbele chako.

Vipaumbele huendana na muda.

Jambo la kwanza sasa ukiliweka la kwanza kesho hutapata matokeo yaliyo bora (Mhubiri 3:1, 11a). Wanaisraeli walipata shida katika hali zao za uchumi kwa sababu ya kushindwa kuzingatia muda katika kuweka vipaumbele vyao; walipotakiwa kutoa sadaka na kujenga Nyumba ya BWANA wao walisema huu sio wakati na hivyo iliathiri hali yao ya kiuchumi na kimaisha (Hagai 1:2, 4).
Ndio maana biblia imeweka msingi wa vipaumbele kwa vijana katika muda wao wa ujana ili watumie muda wao huo kwa kujenga uhusiano bora na Mungu na kumtumikia kabla ya siku za uzee wao (mhu12:1). Hiki ni kipaumbele muhimu kuliko vyote unavyoweza kuwa navyo.
Mtu asiyetambua  nini ni kipaumbele kwa wakati husika, ni sawa na meli isiyokuwa na uelekeo katikati ya bahari. Vipaumbele vinasaidia kujua ufanye/usifanye nini kwa wakati huu; inakupa kujua njia (dira) sahihi ili kufikia malengo yako. Mtu asiyekuwa na vipaumbele ni sawa na mtu asiyejua njia. Mtu huyu hawezi kupotea njia, anaweza kufika anapotakiwa kufika na asijue kama amefika. What a waste!!
Ukiamka asubihi Tv inataka uingalie muda wote; Redio inataka uisikilize, hakuna muda watazima mitambo yao ili wakupe nafasi ya kufanya mambo yako mengine; masaa 24 wanarusha matangazo; simu inataka uchat muda wote; marafiki wanataka mkae masaa sita mpige stori tu. Magazeti yanataka uyasome, bado majukumu ya shule kama ni mwanafunzi au ofisi kama ni  mfanyakazi au mfanyabiashara. Kila kitu kinataka kutumia muda wako; usipojua nini kianze na nini kifuate; niulize, nami nitakuambia mwisho wako. Nioneshe vipaumbele vyako; nikuoneshe hatima yako.

Kipaumbele cha kwanza kuliko vyote unavyoweza kuwa navyo.

Kipaumbele cha kwanza ili kufanikiwa ni kuwa na uhusiano binafsi na Mungu (daily communion). Daudi alitafuta neno moja tu nalo ni kukaa nyumbani mwa BWANA. Mafanikio halisi huanza na Mungu mwenyewe. Maisha ya mwanadamu Huanza, Hukamilika na Kupata maana katika Mungu pekee; uhusiano huu ni zaidi ya kwenda kanisani jumapili, ni zaidi ya kwenda kwenye kikundi cha sala; ni kutamani kukaa katika uwepo wake Muda wote, kuzijua njia zake, kuungana naye na kushikamana naye katika Neno lake katika maisha yetu ya kila siku.
“Neno moja nimelitaka kwa BWANA, Nikae nyumbani mwa BWANA siku zote za maisha yangu. Niutazame uzuri wa BWANA, na kutafakari hekaluni mwake” Zab 27:4
Mwandishi wa kitabu cha ‘Momentary marriage’, John Piper amewahi kuandika jambo kuhusu umuhimu wa vipaumbele kwa kusema, “kuweka jambo la kwanza kuwa la kwanza, hufanya jambo la pili kuwa bora zaidi” (keeping first things first, makes second things better). Hivyo kuweka jambo la kwanza kuwa la pili huathiri matokeo ya mambo yote katika hali zote.
 “…Bwana akajibu akamwambia… Martha, unasumbuka na kufadhaika kwa ajili ya vitu vingi; lakini kinatakiwa kitu kimoja; na Mariamu amelichagua fungu lililo jema, ambalo hataondolewa” Luka 10:39-42
Kipaumbele cha Mariamu ilikuwa ni jambo moja tu ambalo lililokuwa linatakiwa kwa wakati huo, nalo ni kukaa miguuni pa Yesu ili apate kusikiliza maarifa yatakayompa ufahamu na hekima katika maisha. Kipaumbele hakikua katika kufanya kazi bali kukaa na kumsikiliza kwanza mwenye kazi. Ndio maana Mfalme Daudi alitaka kukaa nyumbani mwa BWANA siku zote apate kuutazama uzuri wa BWANA na kutafakari (meditate) Neno hekaluni mwake na hivyo alipata hekima iliyomsaidia kujua namna ya kuishi ili kufikia mafanikio katika maisha yake; si ajabu ni miongoni mwa wafalme waliofanikiwa sana katika nyakati zao (zab119:97-98, 104).
Ni muhimu kukumbuka kuwa, Maisha ya mwanadamu ni kama kitabu, kwa jinsi anavyokaa na Mungu ndivyo kinavyozidi kufunguka kurasa hadi kurasa. Unaposhindwa kutambua vipaumbele kwa wakati, maisha yanakuwa hayana ladha, yanabeba mafadhaiko, kulaumu wengine na masumbufu ya kila namna; kwa sababu kuweka jambo la kwanza kuwa la pili huathiri matokeo ya mambo yote katika hali zote.

Tujifunze kwa Nehemia

Usipokuwa na vipaumbele, hauwezi kusema hapana kwa mambo yanayoonekana kuwa mazuri (good) ili kuyafikia yaliyo bora (best). Nehemia wakati ameanza kazi ya ujenzi wa ukuta wa Yerusalemu uliokuwa umebomolewa, alijua kipaumbele kwa wakati ule ni kazi iliyokuwa mbele yake, hakukubali kuyumbishwa na jambo lingine lolote. Usipojua nini unatakiwa kufanya kwa wakati husika, utafanya kila kitu na kujitahidi kuwa kila kitu (committed in the wrong things).
Sanbalati na Geshemu wakatuma wajumbe kwangu, wakasema, Njoo, tukutane huko vijijini katika nchi tambarare ya Ono… Na mimi nikatuma wajumbe kwao, nikasema, Hii ni kazi kubwa ninayoifanya mimi, hata nisiweze kushuka; mbona kazi ikome, hapo ninapoiacha, niwashukie? Nao wakaniletea maneno hayo mara nne, nikawajibu maneno kama yale…” Nehemia 6:2-5
Iwe ni mfanyakazi, mwanafunzi, mzazi au mlezi ni muhimu kutambua na kuzingatia vipaumbele katika kila eneo muhimu la maisha yako kwa wakati; vipaumbele vyako ndivyo vitakavyoamua uelekeo wako na hatima yako, ni muhimu kujizoeza kutenga muda mara kwa mara na kujiuliza ni nini kipaumbele, nini kianze na nini kifuate iwe kwa mambo ya ofisi, biashara, shuleni au nyumbani;
“If you don’t know where you are going, any way can take you there”

0 comments :

YEYE badala ya Wewe

11:48:00 AM Unknown 0 Comments

 
“YEYE” BADALA YA WEWE 
(Alikwenda kama mwakilishi, kwa ajili yako) 
Watu wengi wanaposoma biblia wanadhani Adam na Eva walizeeka. Ukweli ni huu, walikufa mapema hawakuweza kudumu kabisa; kwa jinsi ya mwili waliishi miaka mingi na kuzeeka, lakini kwa jinsi ya kiroho walikufa mapema mno, kumbuka mtu ni roho, anayo nafsi na anakaa ndani ya mwili; mtu sio mwili bali roho. Siku waliyotenda dhambi, ndiyo siku waliyokufa. Ndivyo walivyoambiwa na Mungu na ndivyo ilivyokuwa. Hata sasa dhambi ni rafiki yake kifo, huwezi kwenda matembezini na dhambi na ukamuacha kifo nyumbani. Hawa ni mapacha, siku ya dhambi ni siku ya kifo. “walakini matunda ya mti wa ujuzi wa mema na mabaya usile, kwa maana siku utakapokula matunda ya mti huo utakufa hakika.” Mwanzo 2:17
Siku mtu anapotenda dhambi ndiyo siku anayokufa, uzima wa mwili unadanganya tu. Dhambi ni mbaya, mistari mingi katika biblia inayotaja dhambi, inaitaja kwa kuiunganisha na kifo (soma Methali 6:32, Warumi 6:23). Dhambi huoana na kifo. Kama ni msomaji wa biblia utakubaliana na mimi kwamba, ndoa kati ya dhambi na mauti ni imara sawasawa na shetani na kuzimu. Huwezi kutenda dhambi bila ya kukikaribia kifo. Hatua muhimu kuelekea kifo ni kuanza kutenda dhambi. Yesu alikufa kwa sababu alichukua dhambi zetu, mauti ilimpata kama mshahara wa dhambi zetu.
Mungu anachukia dhambi, chuki yake dhidi ya dhambi ni dhahiri. Chuki ya Mungu dhidi ya dhambi ni chuki ya milele. Dhambi zetu zilikusanywa mahali pamoja yaani, katika mwili wa Yesu Kristo. Kama mtu akusanyavyo takataka au uchafu sehemu moja na kisha akauchoma moto, ndivyo uasi wa wanadamu wote ulivyokusanywa katika mwili mmoja wa Yesu Kristo na kisha akafa msalabani kama fidia yetu. Maasi yote na uovu wote uliwekwa juu ya mwili wake.
Yesu ni mwakilishi wetu katika mauti, yeye badala yetu {vicarious death}. Badala ya sisi kwenda katika mauti yeye alikwenda kwa niaba yetu. Watu maalumu wanaposhindwa kuhudhuria katika hafla fulani au katika chakula cha jioni huteua wawakilishi wao. Ni rahisi kwa watu hawa wakuu kumpata mwakilishi  kwani ni suala la kwenda kula na kunywa. Lakini akitafutwa mwakilishi atakaye kwenda kufa kifo cha aibu kwa niaba yao, hakika hawezi kupatikana. Yesu hakutuwakilisha katika hafla na karamu za raha na furaha, bali alituwakilisha katika mauti naamu mauti ya msalaba na aibu. Alituwakilisha katika baridi, katika kukosa usingizi katika kuteswa na kuvuja jasho la damu, na katika kulia sana.
Kwa kitambo kirefu tulihitaji mwakilishi na hakupatikana, kwa nyakati tofauti tofauti nabii Isaya na Daudi walitamani Mungu aje na afanyike mwakilishi wetu. Walisikika wakisema, “laiti mbingu zingekuja duniani” au “laiti BWANA angepasua mbingu” walitamani kuona kile kinachoitwa kwa kizungu, ‘Heaven on Earth.’ Yaani mbingu duniani
Ombi lao lilijibiwa pale Yesu alipokuja duniani. Yesu ndiye ukamilifu wa mbingu dunian. Mungu pamoja nasi yaani, Mungu katika maisha na ratiba za kwaida kabisa za mwanadamu. Yesu ndio mbingu zote, badala ya kutazama mbinguni sasa tunamtazama Yesu aliyekuja na aliye mbingu duniani (Emanueli).
Ili uwe mpatanishi ni lazima uzifahamu pande zote zinazokinzana kwa uzuri wote. Ili uwe mkalimani ni lazima ujue lugha zote mbili kwa ufasaha, Yesu aliijua lugha ya Mungu na ya wanadamu pia. Yesu alimjua Mungu (alitoka kwa Mungu) lakini kwa kuwa alikuwa mwanadamu alimfahamu vizuri mwanadamu. Alijua namna Mungu anavyochukia dhambi (alikuwa Mungu) lakini alijua jinsi dhambi inavyomtesa mwanadamu kwa kuwa aliishi kama mwanadamu. Aliona magonjwa, hali zao ngumu za kimaisha, aliona utawala wa giza na utumwa wa dhambi. Kwa kuwa alizijua namna zote ndio maana hakulalamika kwamba mateso yamezidi pale msalabani, kwani aliijua chuki ya Mungu dhidi ya dhambi. Huwezi kujiandaa kufanya malipo kama hujui gharama au bei ya bidhaa.
Yesu alibatizwa ili aitimize haki yote. Ubatizo wa Yesu ni muhimu sawasawa na kifo chake. Alikufa kwa ajili yetu, alibatizwa kwa ajili yetu pia. Yesu hakuwa na haja ya kubatizwa, hata Yohana alitaka kukataa kumbatiza. Ubatizo wa Yohana ulikuwa ni ubatizo wa toba, Yesu hakuwa na sababu ya kutubu, hakutenda dhambi. Asiye na dhambi hana haja ya kubatizwa ubatizo wa toba. Lakini kwa ajili yako alibatizwa. “Wakati huo Yesu akaja kutoka Galilaya mpaka Yordani kwa Yohana ili abatizwe. Lakini Yohana alitaka kumzuia, akisema, Mimi nahitaji kubatizwa na wewe, nawe waja kwangu? Yesu akajibu akamwambia, Kubali hivi sasa; kwa kuwa ndivyo itupasavyo kuitimiza haki yote. Basi akamkubali.” Mathayo 3:13-15
Ubatizo ndio ulikuwa mlango pekee ambao Yesu alipitishwa ili kuutwaa uovu wetu na kuitimiza haki yote. Pale mtoni alikwenda kuchukua dhambi zetu, pale msalabani alikwenda kulipia deni lililotokana na dhambi alizochukua pale mtoni-katika ubatizo. Ni baada ya ubatizo ndipo yalinenwa maneno haya: “Siku ya pili yake amwona Yesu anakuja kwake, akasema, Tazama, Mwana-kondoo wa Mungu, aichukuaye dhambi ya ulimwengu!”Yohana 1:29
Ni muhimu kujua kwamba tu wadhambi na Yesu alituwakilisha katika kupokea mabaya. John Newton mtunzi wa wimbo wa ‘Amazing grace’ katika moja ya maandishi yake ameandika hivi: “mimi si mtu mwenye kuweza kukumbuka mambo yote lakini mambo mawili siwezi kuyasahau kwa hakika kwamba, ‘mimi ni mdhambi mkuu, na Yesu Kristo ni mwokozi Mkuu”. Ukweli huu ni muhimu kwa kila anayetaka kuwa karibu na Yesu
Mtu mmoja amewahi kusema “katika matendo yote atendayo mwanadamu, toba au kutubu ni tendo la Ki-mungu zaidi kupita yote.” Inawezekana kabisa hujazaliwa mara ya pili au bado una dhambi zinatendeka kwa siri, hakuna anayejua zaidi ya wewe; fanya uamuzi wa kuziacha leo, jikatalie ya dunia na ungana na Yesu sasa. Alikufa kwa ajili yetu, hatuna budi kuishi kwa ajili yake 2Kor5:15. Kama uko tayari basi tamka maneno haya kwa imani:
“BWANA YESU, NAOMBA UNIREHEMU MIMI MWENYE DHAMBI. NINAAMINI KATIKA UBATIZO WAKO, NINAKIRI WEWE NI BWANA NA NINAAMINI KWA MOYO KWAMBA, MUNGU ALIKUFUFUA KUTOKA KATIKA WAFU. NIPE NA ROHO WAKO BWANA ILI ANIONGOZE DAIMA.” AMINA
Hongera kwa uamuzi uliofanya, usisite kuwasiliana nasi kwa email au simu zetu, nasi tutazidi kukuombea na kukushauri.
MUNGU AKUBARIKI SANA.

0 comments :