Mwaka 2018 Uwe Mwaka wa Kujihatarisha.......

11:25:00 AM Unknown 0 Comments

 
MWAKA 2018 UWE MWAKA WA KUJIHATARISHA ZAIDI ILI KUPATA MAFANIKIO
Wengi wanashindwa kwa sababu hawafanyi kitu mpaka waone ni salama kabisa, hawaanzi mradi mpaka waone ni faida tupu, tabia hii imezuia mafanikio ya wengi. Mwaka jana niliingia kwenye biashara ya mtandaoni (online business) na kupata hasara ya milioni nne, mwaka huo huo bila ya kukata tamaa nikaingia katika biashara nyingine na kupata faida ya milioni nne! Ukipata hasara katika biashara moja haina maana kwamba na biashara nyingine utapata hasara pia.
Kitabu cha Mhubiri kinasema, “Mwenye kuuangalia upepo hatapanda; Naye ayatazamaye mawingu hatavuna” Mhubiri 11:4. Ukichunguza chunguza sana huji kufanikiwa katika uwekezaji na maendeleo. Kuna wakulima ambao wakijua ni msimu wa kilimo wanalima na hawa ndio hufanikiwa. Na kuna wale ambao hata kama ni msimu wa kilimo wao huchunguza chunguza mawingu na mwishowe wanashindwa kupanda mbegu zao.
Tabia ya kujihatarisha ni njema na imewasaidia wengi. Fanya kitu kwa wakati uchunguzi utakuja baadaye! Amesema Ratan Naval Tata mwanzilishi wa kampuni ya kutengeneza mitambo na magari aina ya TATA, “I don’t believe in taking right decision, I take decisions and then make them right” kwa tafsiri yangu amesema, “Siamini katika kuchukua maamuzi sahihi, bali nafanya maamuzi na baadaye nayafanya kuwa maamuzi sahihi”
Kujihatarisha inaweza ikawa ni kuachana na uhusiano mbaya, inaweza ikawa ni kuhama mji mmoja kwenda mwingine, inaweza ikawa ni kufunga na kuomba licha ya dalili za vidonda vya tumbo. Inawezekana ikawa ni kurejea nyumbani usiku kila siku kwa sababu za msingi, au ikawa ni kuamka mapema. Pia kujihatarisha inaweza ikawa ni kufanya kinyume na walio wengi, kwenda katika upekee wako au katika njia ya ubunifu ambayo wengi hawapiti. Vyovyote vile kama hatukujihatarisha kabisa hatutapata badiliko lolote.
Matajiri wengi akiwemo Bill Gates na Oprah Winfrey wamekuwa na sifa ya kukatiza masomo au kuacha kabisa ili kwenda kutumikia ndoto zao. Hii nayo ni kujihatarisha, kuacha kile ambacho dunia inaamini ni ufunguo wa maisha ilikuwa ni sawa na kuyafunga maisha yao. Lakini pamoja na hatari ya kuacha shule bado wamefanikiwa na wamewaajiri waliohudhuria vizuri shuleni. Kama kunamafanikio nje ya elimu basi ni muhimu tukajua elimu si ufunguo pekee. Maisha ni zaidi ya vidato!
Maskini wote wanachukia vurugu na hatari, hawapendi biashara nje ya kiyoyozi hata mara moja hawajitumi kutembeza bidhaa. Wanapenda usalama, kulala mapema na kuchelewa kuamka. Hawapendi kusafiri juu ya magari aina ya Fuso yanayokwenda minadani, wanapenda usafiri tulivu na salama, hawataki usumbufu wa wachuuzi wadogo wadogo wenye kutembeza biashara. Hawawazi kuajiri, wao wanataka kuajiriwa tu!
Nakumbuka mwaka 2015 baada ya sala na maombi niliamua kuondoka nyumbani umbali wa  mikoa mitano na kuhamia jijini Dar-es-salaam na ndani ya miezi miwili nilipata nilichokuwa nahitaji kwa muda ule. Si kila mtu atafanikiwa mjini wengine wanahitaji kurudi vijijini na wengine kwenda mjini ili kukutana na mafanikio yao. Ili kukutana na ndoto zao wengine itawalazimu kutoka Ulaya na kurejea katika nchi zao.
Unapopanga mipango yako mipya weka na mipango yenye kukuhatarisha (bila kuvunja sheria) na ndiyo mipango ya mafanikio.
Take risks, if possible take calculated risk……

0 comments :