Bwana alipoamuru baraka

10:22:00 PM Unknown 0 Comments

 
BWANA ALIPOAMURU BARAKA
MUDA MWAFAKA ENEO MWAFAKA. 
Katika mambo ambayo Mungu hata subiri ufanye maandalizi ni hukumu na fursa. Kila siku unapaswa kuwa tayari, katika eneo husika, mwenye maandalizi kamili, ndio maana ya lile neno kesheni. Si kila eneo, si kila Mkoa, si kila medani wala si kila nchi itakuwa na Baraka zako; liko eneo moja, iko aina ya biashara fulani, uko mkoa na pahala ambapo Mungu ameamuru baraka zako zipatikane. Wakati mwingine tunachagua miji kwa macho ya nyama na hivyo tunavyokwenda ndani yake hatufanikiwi sana. Si kila aliyeko Ulaya anamafanikio, kuna wengine wako huko na wanaomba chakula, hawana uhakika wa kupata milo mitatu.
Kuna watu ambao walikuwa jijini Dar es salaam ilhali baraka yao ilikuwa Dodoma. Kwa vyovyote vile haikuwa rahisi kuwapeleka watu hao Dodoma inawezekana walifikiri hakuna maisha bora nje ya jiji la Dar es salaam. Lakini Mungu kwa kutumia Tangazo la Serikali la kuhamia Dodoma amewawezesha pia maelfu ya watanzania kwenda kwenye baraka yao iliyoamriwa mjini Dodoma. Tangu nyakati za Yesu Kristo mpaka sasa matangazo mengi ya Serikali yamekuwa yakibeba makusudi ya Mungu ya amani. Amani maana yake uchumi mzuri, Baraka na mafanikio. Yanaweza matangazo hayo yakaonekana magumu na mabaya yenye kubeba usumbufu lakini baadaye Mungu hujitwalia utukufu na watu wake hustawi.
Ukihamishwa kwa Tangazo la Serikali usigome, Matangazo hayo hubeba baraka.  Katika saa yako ya kusimama kiuchumi na kiutumishi tangazo hilo halitaweza kukudhuru hata kama lilitolewa ili kukuangamiza wewe. Tangazo la Herode la kuua watoto wote chini ya miaka miwili halikuweza kumua Yesu maana ilikuwa ni wakati wa Yesu kung’aa na kuokoa, halikuweza kumzuia.
Si miji peke yake, hata changamoto nyingine za maisha zenye ukakasi  ndani yake kuna baraka pia. Wako watu ambao bila talaka wasingelipata wokovu, bila kuachwa wasingelijua kusimama wenyewe, wako wale ambao bila kufeli masomo wasingeli jaribu biashara ambazo leo zimewapandisha na kuwafanya wakuu.
Baraka hizo zisingepatikana ikiwa kila kitu kingekuwa shwari, mara nyingi inapokuwa ni shwari watu hujisahau sana na kufanya yasiyo ya msingi. Biblia inasema, “Katika shida yangu nalimwona BWANA”.  Kuna nyakati ambapo ni kupitia shida na usumbufu tunaweza kumwona Mungu. Ni methali ya zamani ya wazungu, “Bahari shwari haitoi wanamaji hodari” ni kweli baharia hodari ni lazima atakuwa na uzoefu wa kutatua shida za majini.
Usiogope sura ya mji, usiogope ukubwa wa changamoto inayokukabiri; cha msingi hakikisha uko mahali sahihi ukisubiri wakati sahihi wa kuinuliwa kwako. Mahali ambapo Mungu ameamuru baraka pana changamoto lakini pia pana baraka nyingi. Kuwa mahali pa baraka haina maana hapatakuwa na changamoto kabisa! Mara nyingi ustawi wako katika eneo hilo utategemea pia namna unavyomkumbuka Mungu, kumkumbuka maana yake kushika amri zake na kumshuhudia kwamba ni yeye ni Mungu aliyekufikisha hapo Sayuni yako.
Barikiwa na Endelea mbele…

0 comments :