Roho ya Batromayo Kipofu

10:25:00 PM Unknown 0 Comments

 
ROHO YA BATROMAYO KIPOFU
“ONA FURSA”
Batromayo aliona watu kama miti. Watu wengi wanasumbuliwa na roho hii hawaoni picha halisi, picha yao haijatulia. Ni kama vile ungo wao wa kudakia mawimbi haujatulia, hawapati picha halisi. Ni muhimu sana mwaka huu 2018 sote tumuombe Mungu afungue macho yetu tuweze kuona fursa!
Kwa uzoefu mdogo nathubutu kusema, “fursa haziwezekani bila imani”. Macho ya mwili hayotoshi, ile kwamba macho yetu yanaona taa za barabarani na tunavuka salama haina maana kama tunaona fursa pembezoni mwa barabara. Mtu anayeweza kufikiri kimkakati “strategic thinking” anaweza kuona fursa na kuzitumia. Kufikiri kimkakati kutakuwezesha uone miaka kumi ijayo na zaidi.
Kwa kukosa imani watu hauza mambo ambayo baadaye yangekuwa fursa kubwa, kwa uhaba wa imani watu huogopa kuanza jambo ambalo halijazoeleka. Anayewekeza miaka mia moja ijayo anaamini kwamba, Mungu atamlinda na kumpa uhai, ndani yake mtu huyo hamna hofu ya kifo. Fursa inataka imani katika sura tatu, kwanza mwamini Mungu muumba wako, jiamini na kisha amini wazo lako.  Adui mkubwa wa fursa ni hofu, uwekezaji unakwenda na ujasiri.
Zamani walituambia, “wasiwasi ndio akili” si kweli. Nenda msituni utagundua mnyama mfalme wa msitu ni simba ambaye ni mnyama jasiri. Njoo duniani utagundua mataifa makubwa yana ujasiri mkubwa pia. Alisema msemaji wa Marekani wa mambo ya nje wakati huo John carry, “Dola ya Washington haitatikisika” alisema hayo kwa ujasiri sana akionya taifa moja alilolitazama kama adui. Hatuna sababu ya kuogopa amesisitiza Shiv Khera katika kitabu cha, Unaweza Kushinda: “Losers want security, winners seek opportunity. Losers more afraid of life than death…”.
Tunawezaje kuona fursa? Maana kama hatukuijua fursa kabla ya kukutana nayo, siku ikitokea tutaiona kama mkosi. Lazima ujifunze kuhusu fursa na uzifahamu ili siku ukikutana nayo uitambue kirahisi. Wewe si tajiri ila jitahidi usome kuhusu utajiri. Leo wewe si mfanya biashara lakini jitahidi kusoma na kujifunza kuhusu biashara. Soma wasifu wa wafanya biashara kama; Mohamed Dewji, Warren Buffet, Reginard Mengi, Ratan Naval Tata, Alhaji Dangote, Said Bakhresa na wengine wenye ushawishi kwako.
Watu wengi wanapenda kushinda ila ni wachache tu ambao wanapenda maandalizi kwa ajili ya kushinda. Fursa zinakutaka ufanye maandalizi. Wewe ndiye unapaswa kuisubiri fursa kwani fursa haina nafasi ya kumsubiri mtu! Fursa huja kwa waliojiandaa. Preparation is the Key!
Sala: Ee Mungu Baba Muumbaji wetu, utufungue macho ili mwaka huu 2018 sote kwa umoja wetu tuweze kuona fursa. Katika Jina la Yesu Nimeomba. Amina.
Usisite kutuandikia kwa anuani yetu kwa maoni, ushauri na maombi. Barikiwa!

0 comments :

Biblia ina majibu yote

2:07:00 PM Unknown 0 Comments

BIBLIA INAMAJIBU YOTE
ISOME!
Ni mwaka mpya sasa nuia idadi ya vitabu unavyopaswa kusoma mwaka 2018, zaidi ya yote usisahau mpango wa kusoma Biblia, yearly bible reading plan! Tatizo la kutokusoma linaendelea kuwatesa watu wa leo, kizazi hiki hakijajijengea tabia ya kujisomea. Majibu mengi ya matatizo yetu yanayotukumba katika maisha ya kila siku yako katika vitabu, bahati mbaya hatusomi.
Hivi karibuni nikiwa naelekea Bagamoyo kwenye daladala nilifarijika baada ya mtoto wa miaka kumi kuingia ndani ya gari na kisha kutoa kitabu na baada ya mwendo kidogo akaanza kusoma. Nilitamani kupiga naye picha (selfie) kwa furaha, kuona utamaduni ninao upenda umejengeka kwa mtoto yule. Miji na majiji yenye foleni hutoa fursa kwa watu kujisomea wakiwa barabarani. Nyumbani utasema watoto wasumbufu barabarani je? Furaha tunayoikosa vijiweni iko kitabuni, nguvu tunayoikosa pahala pa kazi iko vitabuni, knowledge is power!! Mwenye maarifa mengi ni mwenye nguvu nyingi hili halipingiki. Kile ambacho baba yangu hakusema vitabu vimeniambia, kile ambacho dini ilinificha vitabu vimeniweka bayana. What a royal friend!
Nakushauri usome vitabu, lakini soma zaidi Biblia. Katika neno la Mungu kuna umilele wote. Yesu akasema, “ninyi mmekuwa safi kwa sababu ya lile neno mliliosikia”. Lile neno la Mungu unalosikia linafanya unakuwa safi mwili na roho.
Neno la Mungu limebeba majibu ya hali unazopitia wewe binafsi na Taifa lako pia. Unapotazama uchumi wako na hali ya taifa lako usiende tu kwa kutumia elimu ya uchumi ya darasani, ni muhimu utazame kiroho pia. Ukiona hali ngumu ya uchumi kwenye nchi jiulize Mungu anataka nini kwa taifa lako, inawezekana kabisa anataka toba. Badala ya kwenda kuchukua shahada ya uzamili ya uchumi mara nyingine ni muhimu kusoma Biblia mfululuzo. Daniel kwa kusoma maandiko (neno la Mungu) aligundua nini kinaendelea kwenye taifa lake.
Jifunze kujua chanzo, anayejua chanzo halalamiki sana. Taifa linapopewa mtawala mkorofi ni lazima ujue kuna mahali dhambi ilitendeka katika Taifa hilo na Mungu amemweka mtawala huyo kwa makusudi yake ili watu wake watubu na kurejea. Katika hali kama hiyo kufanya kazi kwa bidii hakutasaidia ila toba ya kweli kwa wateule wote wa Mungu walioko kwenye taifa hilo inaweza kuleta suluhisho.
Moja ya njia kuu ambayo Mungu amekuwa akiitumia kuzungumza na nchi na watu binafsi ni hali ya uchumi. Ukiaona kuna mvua ya kutosha, tena kwa wakati wake ni lazima ujue kuna kitu kizuri Mungu anazungumza, ukiona ukame na watu wanakufa kwa njaa ujue kuna kitu Mungu anadai au ibada ya sanamu imekithiri, ukiona watu wengi wanakimbia nchi ujue kuna laana ya ukiwa.
Katika kila jambo lihusulo hali ya hewa, mahali pa kuishi, hali ya uchumi ni muhimu utafute makusudi ya Mungu katika Biblia. Mambo haya yote ndani yake kuna makusudi ya Mungu, ukiyatafute ndani ya neno la Mungu utayajua! Jipatie ufahamu uyajue yanayokuhusu na yanayohusu nchi yako kwa kusoma maandiko. Barikiwa.

0 comments :

Bwana alipoamuru baraka

10:22:00 PM Unknown 0 Comments

 
BWANA ALIPOAMURU BARAKA
MUDA MWAFAKA ENEO MWAFAKA. 
Katika mambo ambayo Mungu hata subiri ufanye maandalizi ni hukumu na fursa. Kila siku unapaswa kuwa tayari, katika eneo husika, mwenye maandalizi kamili, ndio maana ya lile neno kesheni. Si kila eneo, si kila Mkoa, si kila medani wala si kila nchi itakuwa na Baraka zako; liko eneo moja, iko aina ya biashara fulani, uko mkoa na pahala ambapo Mungu ameamuru baraka zako zipatikane. Wakati mwingine tunachagua miji kwa macho ya nyama na hivyo tunavyokwenda ndani yake hatufanikiwi sana. Si kila aliyeko Ulaya anamafanikio, kuna wengine wako huko na wanaomba chakula, hawana uhakika wa kupata milo mitatu.
Kuna watu ambao walikuwa jijini Dar es salaam ilhali baraka yao ilikuwa Dodoma. Kwa vyovyote vile haikuwa rahisi kuwapeleka watu hao Dodoma inawezekana walifikiri hakuna maisha bora nje ya jiji la Dar es salaam. Lakini Mungu kwa kutumia Tangazo la Serikali la kuhamia Dodoma amewawezesha pia maelfu ya watanzania kwenda kwenye baraka yao iliyoamriwa mjini Dodoma. Tangu nyakati za Yesu Kristo mpaka sasa matangazo mengi ya Serikali yamekuwa yakibeba makusudi ya Mungu ya amani. Amani maana yake uchumi mzuri, Baraka na mafanikio. Yanaweza matangazo hayo yakaonekana magumu na mabaya yenye kubeba usumbufu lakini baadaye Mungu hujitwalia utukufu na watu wake hustawi.
Ukihamishwa kwa Tangazo la Serikali usigome, Matangazo hayo hubeba baraka.  Katika saa yako ya kusimama kiuchumi na kiutumishi tangazo hilo halitaweza kukudhuru hata kama lilitolewa ili kukuangamiza wewe. Tangazo la Herode la kuua watoto wote chini ya miaka miwili halikuweza kumua Yesu maana ilikuwa ni wakati wa Yesu kung’aa na kuokoa, halikuweza kumzuia.
Si miji peke yake, hata changamoto nyingine za maisha zenye ukakasi  ndani yake kuna baraka pia. Wako watu ambao bila talaka wasingelipata wokovu, bila kuachwa wasingelijua kusimama wenyewe, wako wale ambao bila kufeli masomo wasingeli jaribu biashara ambazo leo zimewapandisha na kuwafanya wakuu.
Baraka hizo zisingepatikana ikiwa kila kitu kingekuwa shwari, mara nyingi inapokuwa ni shwari watu hujisahau sana na kufanya yasiyo ya msingi. Biblia inasema, “Katika shida yangu nalimwona BWANA”.  Kuna nyakati ambapo ni kupitia shida na usumbufu tunaweza kumwona Mungu. Ni methali ya zamani ya wazungu, “Bahari shwari haitoi wanamaji hodari” ni kweli baharia hodari ni lazima atakuwa na uzoefu wa kutatua shida za majini.
Usiogope sura ya mji, usiogope ukubwa wa changamoto inayokukabiri; cha msingi hakikisha uko mahali sahihi ukisubiri wakati sahihi wa kuinuliwa kwako. Mahali ambapo Mungu ameamuru baraka pana changamoto lakini pia pana baraka nyingi. Kuwa mahali pa baraka haina maana hapatakuwa na changamoto kabisa! Mara nyingi ustawi wako katika eneo hilo utategemea pia namna unavyomkumbuka Mungu, kumkumbuka maana yake kushika amri zake na kumshuhudia kwamba ni yeye ni Mungu aliyekufikisha hapo Sayuni yako.
Barikiwa na Endelea mbele…

0 comments :

Mwaka 2018 Uwe Mwaka wa Kujihatarisha.......

11:25:00 AM Unknown 0 Comments

 
MWAKA 2018 UWE MWAKA WA KUJIHATARISHA ZAIDI ILI KUPATA MAFANIKIO
Wengi wanashindwa kwa sababu hawafanyi kitu mpaka waone ni salama kabisa, hawaanzi mradi mpaka waone ni faida tupu, tabia hii imezuia mafanikio ya wengi. Mwaka jana niliingia kwenye biashara ya mtandaoni (online business) na kupata hasara ya milioni nne, mwaka huo huo bila ya kukata tamaa nikaingia katika biashara nyingine na kupata faida ya milioni nne! Ukipata hasara katika biashara moja haina maana kwamba na biashara nyingine utapata hasara pia.
Kitabu cha Mhubiri kinasema, “Mwenye kuuangalia upepo hatapanda; Naye ayatazamaye mawingu hatavuna” Mhubiri 11:4. Ukichunguza chunguza sana huji kufanikiwa katika uwekezaji na maendeleo. Kuna wakulima ambao wakijua ni msimu wa kilimo wanalima na hawa ndio hufanikiwa. Na kuna wale ambao hata kama ni msimu wa kilimo wao huchunguza chunguza mawingu na mwishowe wanashindwa kupanda mbegu zao.
Tabia ya kujihatarisha ni njema na imewasaidia wengi. Fanya kitu kwa wakati uchunguzi utakuja baadaye! Amesema Ratan Naval Tata mwanzilishi wa kampuni ya kutengeneza mitambo na magari aina ya TATA, “I don’t believe in taking right decision, I take decisions and then make them right” kwa tafsiri yangu amesema, “Siamini katika kuchukua maamuzi sahihi, bali nafanya maamuzi na baadaye nayafanya kuwa maamuzi sahihi”
Kujihatarisha inaweza ikawa ni kuachana na uhusiano mbaya, inaweza ikawa ni kuhama mji mmoja kwenda mwingine, inaweza ikawa ni kufunga na kuomba licha ya dalili za vidonda vya tumbo. Inawezekana ikawa ni kurejea nyumbani usiku kila siku kwa sababu za msingi, au ikawa ni kuamka mapema. Pia kujihatarisha inaweza ikawa ni kufanya kinyume na walio wengi, kwenda katika upekee wako au katika njia ya ubunifu ambayo wengi hawapiti. Vyovyote vile kama hatukujihatarisha kabisa hatutapata badiliko lolote.
Matajiri wengi akiwemo Bill Gates na Oprah Winfrey wamekuwa na sifa ya kukatiza masomo au kuacha kabisa ili kwenda kutumikia ndoto zao. Hii nayo ni kujihatarisha, kuacha kile ambacho dunia inaamini ni ufunguo wa maisha ilikuwa ni sawa na kuyafunga maisha yao. Lakini pamoja na hatari ya kuacha shule bado wamefanikiwa na wamewaajiri waliohudhuria vizuri shuleni. Kama kunamafanikio nje ya elimu basi ni muhimu tukajua elimu si ufunguo pekee. Maisha ni zaidi ya vidato!
Maskini wote wanachukia vurugu na hatari, hawapendi biashara nje ya kiyoyozi hata mara moja hawajitumi kutembeza bidhaa. Wanapenda usalama, kulala mapema na kuchelewa kuamka. Hawapendi kusafiri juu ya magari aina ya Fuso yanayokwenda minadani, wanapenda usafiri tulivu na salama, hawataki usumbufu wa wachuuzi wadogo wadogo wenye kutembeza biashara. Hawawazi kuajiri, wao wanataka kuajiriwa tu!
Nakumbuka mwaka 2015 baada ya sala na maombi niliamua kuondoka nyumbani umbali wa  mikoa mitano na kuhamia jijini Dar-es-salaam na ndani ya miezi miwili nilipata nilichokuwa nahitaji kwa muda ule. Si kila mtu atafanikiwa mjini wengine wanahitaji kurudi vijijini na wengine kwenda mjini ili kukutana na mafanikio yao. Ili kukutana na ndoto zao wengine itawalazimu kutoka Ulaya na kurejea katika nchi zao.
Unapopanga mipango yako mipya weka na mipango yenye kukuhatarisha (bila kuvunja sheria) na ndiyo mipango ya mafanikio.
Take risks, if possible take calculated risk……

0 comments :