Mheshimu Rais Wako

2:20:00 PM Unknown 0 Comments

MHESHIMU RAIS WAKO
(Ni kwa Heshima ya aliyemweka katika kiti hicho)
Ukiwa mtawala au mmiliki wa biashara unaweza kumweka yeyote asimamie biashara hiyo kwa niaba yako, asimame kama mwakilishi wako. Mwakilishi huyu bila shaka atakuwa na amri (authority and power) kwa wale utakao waweka chini yake ili awaongoze na kuwasimamia vema. Mwakilishi huyu akidharauliwa bila shaka wewe uliyemweka umedharauliwa pia. Serikali  haziwekwi na wapiga kura, zinawekwa na Mungu. Maeneo mengi tumeshuhudia wenye kura nyingi wakikosa Urais. Wanademokrasia wenye imani wanaelewa hili.
Tunapaswa kuwaheshimu viongozi si kwa sababu ni wema au ni wabaya bali, ni kwa heshima ya yule aliyewaweka watuongoze yaani, Mungu Baba. Ameandika Mchungaji Kenneth Copeland, “Hakukuwa na Serikali korofi kama ile ya wakati wa Yesu Kristo, lakini bado Yesu alitaka iheshimiwe na akasema, ‘yaliyo ya Kaisari apewe Kaisari.’” Kwa maneno mengine Kristo aliwataka watu walipe kodi kwenye Serikali ambayo kimsingi ilikuwa inawakandamiza, hata wao hawakuamini kama Yesu amesema waheshimiwe kama Serikali. Serikali yaweza kuwa dhalimu lakini Mungu aliyeiweka kwa majira husika si dhalimu, na anamakusudi nayo.
Muda mzuri wa kuiheshimu Serikali ni pale inapofanya vibaya, maana ikifanya vema hata wapagani huiheshimu (Luka 6:28). Muda mzuri wa kubariki ni pale watu watakapo kulaani. Katika agano la kale Serikali ya Farao yule wa wakati wa Musa ilikuwa korofi na yenye kiburi hata mbele za Mungu, lakini Mungu alisema ni yeye aliyeiweka kwa makusudi yake. Kuna kusudi kwa serikali yako. Serikali haijiweki madarakani inawekwa. Katika Warumi 9:17 neno nimekusimamisha linaweza kuwa na maana, nimekuweka. Kwa maana maandiko yasema juu ya Farao, ya kwamba, Nilikusimamisha kwa kusudi hili, ili nionyeshe nguvu zangu kwako, jina langu likatangazwe katika nchi yote.Warumi 9:17
Tunamuheshimu mkuu wa nchi  kwa sababu tunayo hofu ya Mungu aliyemweka. Si kila Mtawala (Boss) anastahili heshima kutokana na tabia yake, wengine wanatabia mbaya. Pamoja na hayo kila Mkristo anapaswa kutoa heshima kwa kila mtawala bila kujali tabia yake.
Angalizo:
Katika kumtii kiongozi lazima tuhakikishe hatumkosei Mungu, kiongozi asigeuke sanamu moyoni mwetu. Sauti ya kiongozi ikiwa kinyume na injili ya Kristo na ipuuzwe. Mijadala mambo ya mapenzi ya jinsia moja, mauji ya holela, utoaji wa mimba unaohalalishwa kisheria, ndoa za mitala ni mambo ambayo ni kinyume na injili. Yapuuzwe hata kama msemaji atakuwa ni mkuu wa Nchi.
Mungu anaweza kubadilisha moyo wa kiongozi ikiwa watu watasimama kuomba. Maombi kwa Mungu mwenye nguvu yanaweza kuelekeza nchi wapi ielekee ikiwa mwombaji ataomba kwa bidii. Mungu anaendesha mioyo ya watawala kupitia maombi ya watakatifu.
Endelea kuombea nchi yako….., Shallom Israel, Shallom Tanzania….


0 comments :