Wito binafsi

2:01:00 PM Unknown 0 Comments


WITO BINAFSI.
(Umeitwa kwa jina lako)
Wakristo, wanafunzi, wachungaji, waimbaji, wainjilishaji, wafanyakazi, wataalamu, wanaharakati n.k, ni majina ya vikundi ambayo hayatoi wajibu mkubwa kwa mtu binafsi. Ukweli ni kwamba wito ni ile sauti inayokuhamisha kutoka katika kikundi fulani, nchi yako, mipango yako binafsi na hata katika mwelekeo binafsi.
Wito si jambo jepesi, unaweza ukuleta usumbufu. Wito unahitaji aliyeitwa awe shupavu katika kukata kona (kuitikia wito), awe na uwezo wa kugeuka haraka. Pale mwanafunzi anapoteseka miaka zaidi ya mitano katika masomo yake ili awe daktari na baadaye sauti ya Mungu inamwita katika mwelekeo mwingine tofauti na udaktari, kunahitajika ushupavu na usikivu. Pamoja na kuwepo kwa gharama ya usumbufu, wale wanaotii sauti ya Mungu baadaye hufurahi na kufaidika.
Kuna wito ambao Mungu anamwita kila mtu, wito huu huhusisha aina na mtindo wa maisha tunaopaswa kuenenda nao hapa duniani. Uko wito wa kuishi maisha matakatifu, uko wito wa wokovu uko wito wa kumfuata Yesu yaani ufuasi. Wito wa ujumla haubagui kila mtu lazima aitikie sauti hiyo.
Katika makala hii ninalenga wito wa kipekee, wito ambao hauhusishi mke wala mume, hauhusu kikundi fulani cha watu bali unahusu mtu binafsi. Ameandika mchungaji mmoja, “Yuko wapi mke wa Petro?” Hatutazamii kumuona mwingine katika wito wako bali wewe peke yako.  Ibrahim aliacha nchi, baba na nduguze kwa ajili ya wito. “Basi walipokwisha kula, Yesu akamwambia Simoni Petro, Je! Simoni wa Yohana, wewe wanipenda kuliko hawa? Akamwambia, Naam, Bwana, wewe wajua kuwa nakupenda. Akamwambia, Lisha wana-kondoo wangu.” Yohana 21:15
Yesu alimwita Petro kwa jina, na alimpa kazi kwa jina. Alimwita mara tatu kwa jina lake. Badala ya kusema mitume alisema, Simoni Petro lisha kondoo zangu, Baadaye akamtaja kwa jina kwamba, achunge kondoo zake.
Watu wenye wito wa pekee mara nyingi wanashangaa kwa nini hawasaidiwi au kupunguziwa mzigo, mara nyingi wanajiuliza, “kwani watu wengine hawaoni umuhimu wa jambo hili?” Yesu alipokuwa akiomba alishangaa mitume wake wakilala usingizi, alijaribu kuwaamsha mara kadhaa lakini bado walilala. Ninaamini ni kwa sababu wito wa wokovu si wa kwao, ulikuwa ni wa Yesu Kristo peke yake. Kwenye familia kunaweza kukawa na watoto wengi lakini si wote wanakuwa na mzigo wa kuwasaidia ndugu na jamaa, mara nyingi mzigo wa kusaidia wazazi na ndugu unaweza kumwangukia mmoja. Mwenye mzigo huo (wito wa kusaidia) huwa anatamani apate msaada na mara nyingi haiwi hivyo kwa kuwa ameitwa kwa jina lake.
Ili kijana afanikiwe ni muhimu ajue wazi kwamba kati ya vijana bilioni 1.8 waliopo duniani ni yeye tu ameitwa tena kwa jina lake. Ili mtu mwenye wito wa pekee afanikiwe ni lazima ajue kwamba katika dunia hii yenye watu bilioni nane ameitwa peke yake, tena kwa jina lake. John Wesley akitambua hili alisema, “Naona dunia nzima kama parokia yangu”.
Endelee kubakia kilele…..mpaka wiki ijayo shalom.

0 comments :

Mungu anaheshimu chanzo chako

12:53:00 PM Unknown 0 Comments


MUNGU ANAHESHIMU CHANZO CHAKO
(Heshimu ulikotoka)
Ni usemi wa kawaida kwamba usidharau ulikotoka, au usisahau kwenu. Mungu anaheshimu walio kulea, wazazi wako, walezi, nchi unayotoka, anaheshimu pia kanisa ulilotoka hata shule uliyosoma awali.
Uhai wako umefungwa na chanzo chako, maendeleo yako ya kudumu yanategemea sana uhusiano wako na chanzo chako. Taasisi zinaweza kuwa chanzo chako, wazazi ni chanzo chako pia. Epuka kuwa mjane au mgani ukiwa angali kijana.  Ameandika mwalimu Mwakasege, “Unataka kujua mchumba wako ataishi miaka mingapi? Chunguza uhusiano wake na wazazi wake.”
Vyanzo vyetu ni vingi, vipo vya kiroho, kimwili, kifedha, kitaaluma na hata kimaisha. Wako waliotuzaa kwa kutupa mitaji, wako waliotupa ushauri, na wako pia waliotuadabisha ili tufanye mambo ya msingi. Usidharau shule uliyosoma, usidharau chuo ulichosoma, usidharau hata kanisa lako mama. Mungu anaheshimu chanzo cha awali (primary producer) na ameufunga uhai wako na chanzo chako cha awali. Ukitoka toka kwa heshima na amani.
Unapaswa kuheshimu wazazi wako wa kiroho, unapaswa kuheshimu kanisa ulilotoka kabla hujaanzisha huduma yako. Ustawi wako katika huduma mpya unategemea namna ulivyoondoka katika chanzo chako. Si vyema kutukana au kutamka maneno mabaya dhidi ya chanzo chako. Usidharau wale waliokuhubiria injili ya kwanza ni watu muhimu kwako.
Kanisa katoliki ni kanisa mama na linamchango mkubwa katika uenezaji wa injili na huduma za jamii. Naliheshimu kanisa Katoliki kwa mchango wake mkubwa wa kuzaa madhehebu mengi mno ya Kikristo, umewahi kuwaza nini kingetokea kama kanisa hili kongwe lingesambaza uislamu au upagani.  Siku nilipowaza kwamba, ingekuwaje kama kanisa lingeeneza uislamu kupitia huduma zake za jamii (shule, elimu, maji, ungozi na ushawishi) nilijikuta nikilipatia heshima badala ya kuona mapungufu yake kama wengi walivyozoea kutazama.
Haya ni maneno ya heshima kutoka kwa Strive Masiyiwa bilionea mwafrika aliyeitikia wito wa kikao cha Papa Francis na mabilionea wa ulimwengu. Bilionea huyu si Mkatoliki ila ni mkristo tu aliyeokoka alisema, “Mimi si mkatoliki, lakini ninatoa heshima kubwa kwa kazi ya awali ambalo kanisa hili limeifanya”.
Kila mahali ambapo biblia imetaja chanzo imetaja pia uhai, maana yake uhai wako unaweza kuathiriwa na uhusiano wako na chanzo. Kumbukumbu la torati 22:7 na Kutoka 20:12
Ukiwaheshimu wazazi utapata miaka mingi na heri duniani, kwa sababu wazazi ni chanzo chako. Ukimkuta mama wa ndege na makinda yake katika kiota maandiko yanasema, usimuue huyo mama ili siku zako ziwe nyingi. Ni kwa sababu huyo mama ni mzalishaji (producer) anauwezo wa kukuzalishia sana. Wafanya biashara wanaheshimu kampuni mama, wanawakumbuka waliowapatia mitaji na kuwapa hisani.  Wafanya kazi wanaheshimu kazi zinazowapatia kipato chao kila mwaka. Rafiki yangu MC Mzonya hupenda kusema, “Chezea mshahara usichezee kazi.” Kazi ni chanzo chako, inahitaji kuheshimika.
Nakutakia heri katika 2017 BWANA  akupe uhusiano mzuri na chanzo chako.

0 comments :

Mimi si sehemu ya .......

12:45:00 PM Unknown 0 Comments


MIMI SI SEHEMU YA TAKWIMU MBAYA
(I’m not a bad statistic)
Januari tano 2017, nikiwa kwenye daladala  nilisikia kituo kimoja cha redio kikitoa takwimu kwamba, kwa mwaka 2017 ambao ulikuwa na siku tano tu tangu umeanza kwamba, tayari watoto laki tano na themanini na kenda (581,000) wameshatolewa kabla ya kuzaliwa.  Wastani wa kutoa mimba kwa siku ni watoto laki moja na kumi na sita kwa siku (116,000). Je, wewe ni sehemu ya takwimu hizi za mauaji ya kukusudia?
Hivi juzi juzi nchini Tanzania tumeona dawa za kulevya zikitafuna vijana, hususani wasanii wa kizazi kipya na waigizaji. Utumiaji wa mihadarati, pombe na aina nyingine za dawa za kulevya zinawaangamiza vijana kwa kasi ya ajabu. Je, wewe ni miongoni mwa waathirika hao?
Wakati takwimu za uovu zinaongezeka, wakati mambo yakiendelea kutisha katika ulimwengu huu, ni vizuri pia uchunguze nini kinaendelea katika ulimwengu wako. Ulimwengu wako ni moyo wako. Inawezekana baada ya siku moja na wewe ukaingia katika takwimu mbaya za ulevi, utoaji mimba, utazamaji wa picha chafu, ubakaji, wizi, utumiaji wa dawa za kulevya na kadhalika. Ni rahisi kuwa sehemu ya takwimu mbaya kuliko kuwa sehemu ya takwimu nzuri.  Chukua hatua, soon you may become a statistic! Mhubiri 9:12
Mwaka jana nilipata masomo mazuri kutoka kwa rafiki zangu Kassimu na Faraja, ambao mara kadhaa tumekuwa tukienda kunywa maziwa pamoja nyakati za jioni. Kassimu alitueleza jinsi mama yake mlezi alivyomuhusia kwamba, akitaka kuoa aangalie namna ambavyo mchumba wake anatatua matatizo. Mamaye alimwambia, wako watu wanatatua matatizo kwa kujiua, ukimuudhi anajiua na anaamini kwa njia hiyo ya kukatisha maisha yake ametatua tatizo. Kwa mtu mwenye kufanya kuuchukia uhai wake kama njia ya kutatua matatizo punde si punde ataingia katika takwimu za marehemu. Atatajwa kati ya waliojinyonga ambao ni wale wauchukiao uhai. (Mhubiri 2:17)
Ziko takwimu za talaka, ziko za wasio olewa na wanataka kuolewa, ziko pia za umasikini. Umejipanga vipi ili kuepusha haya? Ziko takwimu za magonjwa ziko pia za afya njema. Kila jambo lina sababu yake na hivyo linaweza kuzuilika. Ziko takwimu za wasio na kazi na wana uwezo wa kufanya kazi, ziko za wenye vipaji na serikali haijawaona na vipaji vyao. Kama serikali haijakuona ni muhimu ujione na ujitambue. Yusufu alijitangaza na kukitangaza kipaji chake, alimtuma mtu akakielezee kipaji chake. Mwanzo 40:14
Naamini 2017 ni mwaka wako wa kutoka katika takwimu mbaya mpaka nzuri. Hali mbaya haitajibadili yenyewe, bali inabadilishwa na watu kama wewe. Ifanye 2017 kuwa mwaka wako wa kuamka kama ulikuwa umelala, ufanye mwaka 2017 kuwa mwaka wa kutuma barua nyingi za maombi ya kazi. Uwe mwamini wa dini ya bouncebackability (uwezo wa kuanguka na kusimama kwa kishindo). Ni ule uwezo wa kutoka katika uathirika mpaka kuweza kuathiri jamii zetu (positively).  Ni ile hali ya kuifanya hali mbaya ikuzalie mambo mazuri kabisa.
Wakati natafuta kazi nilikutana na mtu aliyenunua stamp hamsini za barua za kuombea kazi, wakati huo nakutana naye alikuwa ametuma zaidi ya barua 50 bila ya kupata kazi. Mimi nilikuwa nimeanza kuchoka na kukata tamaa wakati hata barua kumi (10) zilikuwa hazijatimia. Huenda wewe pia unaanza kuchoka wakati hata barua ishirini hujafika. Amka na endelea Mungu wa mbinguni na afanye 2017 isiishe uwe kazini.
Mwombe Bwana ili mwaka huu, 2017 uwe mwaka wa majibu yako na mabadiliko yako. Uhamishwe kutoka takwimu zenye kuhuzunisha mpaka zenye kufurahisha sana. Katika mchakato wa mabadiliko kila siku ni muhimu, katika mchakato wa kuacha kutumia vilevi kila saa ni muhimu. Hatuwezi kuitawala siku kama hatukutawala saa, hatuwezi kutawala mwaka kama hatukutawala mwezi. Hatushindi mara moja kwa mwaka mzima, bali tunashinda kila siku ya mwaka katika BWANA (Daily victory in Jesus). Ukitaka kubadili mtindo wako wa maisha mara baada ya kumpokea Yesu basi itakupasa ubadili mtindo wako wa maisha ya siku.
Tukutane kileleni.

0 comments :

Sala ya mwaka mpya

12:03:00 PM Unknown 0 Comments


SALA YA MWAKA MPYA 2017
(EE, BWANA UNIUMBIE MOYO SAFI)
Mipango ya mwaka mpya 2017 bila badiliko la moyo na mtazamo ni kazi bure, ni sawa na kufukuza upepo. Sasa ni mwanzo wa mwaka ambapo kila mtu ana mipango lukuki. Iko ya kitabia, maana tungependa kuwa watakatifu Zaidi 2017, iko ya kiuchumi, maana hutupendi umasikini, iko ya kijamii maana tungependa kuwa na Amani na watu wote na kusaidia jamii zetu mwaka huu.
Katika kuanza mwaka nilipenda kuwasikia watumishi wengi wa Mungu wanasema nini kuhusu mwaka mpya 2017. Lakini katika wote na yote mimi nimeguswa na badiliko la moyo ambalo amelisema Billy Graham ambaye ni mhubiri mashuhuri tena mwenye alama. Kwamba, kama BWANA hakuniumbia moyo safi basi sitaonja badiliko lolote mwaka huu. Lakini kama mioyo yetu na mitazamo yetu kama haikubadilika basi mipango hiyo yote itakuwa ni bure. Ni lazima kufanywa upya nia zetu. [Warumi 12:1-2]
Moyo wako ndio kitovu cha mabadiliko yote. Moyo hutoa badiliko la kudumu, na ili badiliko liwe la kudumu lazima litoke katika msukumo wa ndani na si kutoka nje. Mimi pia nina mipango mingi mwaka huu lakini huu ni kipaumbele, ninataka badiliko la moyo, niwe safi zaidi na nifanane na Yesu. Ni muhimu tumwambia BWANA abadilishe mioyo yetu. Oh Lord Jesus, change my heart!
Unaweza ukajipinga mwenyewe, ikiwa mtindo wako wa maisha hauna uhusiano chanya na malengo yako basi tegemea 2017 kukuonesha mabadiliko kidogo sana. Ni vigumu kukua kiuchumi bila kupunguza matumizi ya anasa, wako wanaotaka kubadilika bila kumwomba Yesu abadilishe mioyo yao. Daudi alijua hawezi kujibadilisha wala hawezi kubadilika ikiwa Mungu si chanzo na egemeo la mabadiliko hayo. Haya ni maneno yake Daudi akihitaji badiliko kutoka dhambini mpaka katika utakatifu tena, Ee, Mungu uniumbie moyo safi…” Zaburi 51:10
Katika orodha ya mipango yako ya mwaka huu, ongeza mmoja, ongeza badiliko la moyo, fanya jambo hilo kuwa mpango mkuu.
Kila la kheri katika 2017.

0 comments :