Nani analeta maana...!

1:27:00 PM Unknown 0 Comments


NANI ANALETA MAANA KATIKA MAISHA YETU
(Mungu ndiye huleta maana katika maisha ya mwanadamu) 
Siku moja nilisoma mtandaoni mtu ameandika kiboko ya wachungaji wenye walinzi binafsi (board guards) ni hii Zaburi ya 127:1-2, nikacheka sana. Ninachoweza kuandika ni kwamba, hata kama wanadamu wanahusika Mungu lazima ahusishwe pia.  Imeandikwa, “1. Bwana asipoijenga nyumba Waijengao wafanya kazi bure. Bwana asipoulinda mji Yeye aulindaye akesha bure. 2. Kazi yenu ni bure, mnaoamka mapema, Na kukawia kwenda kulala, Na kula chakula cha taabu; Yeye humpa mpenzi wake usingizi.

Tafsiri ya huo mstari ni kwamba, usiingie kwenye mradi (project) ambao Mungu haufanyi. Usiwekeze nguvu zako mahali ambapo Mungu hawekezi. Usilinde asipolinda, ukisikia analinda basi hapo na wewe kalinde. Kwa lugha nyingine ni kwamba, fanya pamoja na Mungu. Shirikiana na Mungu katika kazi zako, Do not try to work alone! Ukishaona Mungu hayumo katika mchakato fulani lazima ujue matokeo yatakuwa sifuri. Magumu na mabaya yaliyowapata Adamu na Eva yalitokana na kutengana na Mungu. Hata asingewalaani kwa kinywa chake bado matokeo ya kazi zao na maisha yao ingekuwa ni sifuri. Alama ya juu unayoweza kuipata unapotenda jambo bila ya Mungu ni sifuri (bure). Petro alionja sehemu ya laana ya  hawa wazazi wa kale yaani, Adamu na Eva baada ya kukesha usiku kucha katika uvuvi na kuambulia sifuri. We need Jesus! Luka 5:5

 Zamani niliona nembo (logo) ya shule moja imeandika, Life – Jesus = 0 yaani, maisha bila Yesu ni sifuri. BWANA Yesu ndiye anayeleta maana ya michakato yote ya maisha yetu. Mfumo wetu wa elimu bila Yesu ni bure, mfumo wetu wa ulinzi bila Yesu ni bure. Kazi bila Yesu ni sifuri, utajiri bila ya Mkono wa BWANA ni sifuri pia. Hakuna jambo ambalo linamuhusu mwanadamu ambalo Mungu hataki kushiriki. Kwa kuwa linamhusu mwanadamu linamhusu Mungu pia. Yesu alikwenda harusini kana ya Galilaya (Yohana 2), Yesu alikwenda msibani Lazaro alipokufa (Yohana 11), Yesu alikwenda kazini kwa Petro ambapo ni baharini kwa kuwa alikuwa mvuvi. Yesu alikwenda kushinda nyumbani kwa Zakayo na mara nyingine kwa Martha na Mariamu.

Ingawa kanisa lilikabidhiwa kwa Petro bado Kristo ndiye alikuwa mjenzi. Alimwambia, “Na juu ya mwamba huu nitalijenga kanisa langu” yaani, mjenzi ni Kristo (Mathayo16:18). Neno nitalijenga linaonesha wazi si Petro ambaye atajenga bali ni Yesu aliyemmiliki wa kanisa ndio atakayejenga; maana anasema, na juu ya mwamba huu (Petro) nitalijenga kanisa langu. Anahusika na furaha na huzuni zetu, anahusika na taaluma na siasa zetu. Ni BWANA wa watu wote tena ni BWANA  wa vitu vyote. Nadhani unafahamu mwenye nyumba anaweza hata asishike tofali lakini kwa kuwa ndiye aliyenunua kila kitu na ndiye anayetoa vitendea kazi huhesabika kuwa anajenga. Utasikia najenga huko mbezi au Madale. Anayetoa nguvu, vitendea kazi, ramani na maelekezo ndiyo mjenzi. Kristo ndiye mjenzi wa Kanisa wala si mtume, nabii, mchungaji wala kasisi.

Tunapotenda tukiwa na Mungu matokeo huwa makubwa na kazi huwa nyepesi kama usingizi. Tukiwa na Mungu tunaweza kupata matokeo makubwa (Big Results Now BRN); maandiko husema, “Yeye huwapa wapenzi wake usingizi.” Ni kama Petro alivyopata matokeo makubwa baada ya kutii, Utii wetu kwa Kristo ni mwisho wa laana. Hakuna hukumu wala laana kwa waliondani ya Kristo. Luka 5:5

Paulo anasema kuishi kwake ni Kristo, vipi wewe? Kuishi kwako ni anasa, ulevi au ni kazi yako?  Kuishi kwako ni mumeo au rafiki yako wa kiume au wa kike? Ni pale tu ambapo kuishi kwako ni Kristo ndipo uko salama. Ni rahisi kusema kuishi kwako ni Kristo kwa kuwa unalijua andika, lakini je, Kristo ndio maisha yako?  Mpaka umekubali kuishi kwako kuwe Kristo, maisha yako hayataleta maana. Kuishi kwetu ni bure ikiwa tuko nje ya Kristo. Flp 1:21

Tafakari na acha maisha yako yalete maana kwa kujitoa kwa Yesu.

0 comments :