Fikra sahihi kuhusu Mungu

5:36:00 PM Unknown 0 Comments


 
FIKRA SAHIHI KUHUSU MUNGU
(Orthodoxy) 
Nadhani tumewahi kusikia neno ‘orthodoxy’, likimaanisha usahihi. Lakini kwa somo hili naomba litafsiriwe kama fikra sahihi kuhusu Mungu. Fikra sahihi juu ya Mungu ziko nyingi lakini nitajaribu kuzifupisha katika aya moja. Mungu ni mmoja katika nafsi tatu, Baba, Mwana na Roho Mtakatifu. Mungu ni wa milele tena ameumba mbingu na nchi. Mungu ameumba vitu vyote vinavyoonekana na visivyo onekana na sisi wanadamu ni kazi ya mikono yake. Mungu ametukomboa wanadamu kwa kumtuma mwanaye pekee mpenzi Yesu Kristo katika umbo la binadamu.
Hizo ndizo fikra sahihi kuhusu Mungu, tukiwaza hivyo tunamuwazia vyema. Anazo sifa za ziada pia kwa uchache ni hizi zifuatazo. Mungu ni mwanzo tena mwisho, Mungu ni Mtakatifu, Mungu ni wa rehema na ni mwenye huruma, Mungu hughairi mabaya tena Mungu ni wa upendo.
Dhana dhaifu kuhusu Mungu (wrong thinking about God)
  1. Wametokana na nyani; Wanasayansi wachache (minority) wanakataa ukweli kwamba, tumeumbwa na Mungu. Hawa si wafuasi wa ‘orthodoxy’. Kwa haraka unaweza kudhani kwamba wanasababu yenye mashiko au wanaye mtu bora ambaye ndiye chanzo cha wanadamu. Nasikitika kuandika, wanadai wametokana na nyani. Yaani, sayansi yao ikiisha kumkataa Mungu inamchagua nyani. What a tragedy! Nimeogopa kuandika ‘tumetokana na nyani’ badala yake nimeandika, ‘wametokana na nyani’ yaani hao wanaoshikilia uongo huo. Hawa tunawaombea ili wajue wazi Mungu ndiye Baba yetu na muumba wetu. 1Yohana 4:4
  2. Hakuna Mungu; Wako wengine ambao Biblia inawaita wapumbavu, hawa wamesema hakuna Mungu. Hawa wanakana uwepo wake. Walipoomba pasipo imani, walipoomba pasipo saburi wakaona hawajapata majibu wakasema moyoni mwao hakuna Mungu. Hawa maandiko yanasema ni wapumbavu (Zab 14:1). Mwl. Mwakasege ananukuliwa akisema; “Mungu ni Mungu hata asipojibu maombi yako.” Anayasema haya katika msiba wa Sedekia ambaye licha ya watu kufunga na kuomba bado Mungu alimpenda zaidi. Zaburi 14:1
  3. Mpinga Kristo: Hawa ni wale walioshindwa kuelewa jinsi Yesu alivyoonekana katika ubinadamu. Hawa hawakupata neema ya kumwamini Mungu pamoja nasi yaani, Emanueli. Wanadai Mungu hawezi kuonekana katika ubinadamu. Hawa wanasahau kwamba, Mungu amewahi kuonekana katika moto (mlimani Sinai), Katika kichaka kinachowaka moto bila kuteketea (alipomtokea Musa) tena aliwahi kuwaongoza wana wa Israeli katika wingu na nguzo ya moto. Sasa kama Mungu ameonekana katika maumbo hayo kivipi ashindwe kuonekana katika umbo la mwanadamu? Dawa ya roho hii ya mpinga Kristo ni imani na ukiri wetu kwamba Yesu Kristo ni Bwana. Ni ujasiri wetu kwamba, Yesu Kristo ni mwana wa Mungu na ni mwokozi wetu. 1Yoh 4:3
  4. Wasio jali wokovu. Hawa wako bize na mambo yao, hawajali mambo ya imani; unaweza kuwaita wapagani. Hawa hawayajui maandiko na hawataki kujua, hawamjui Mungu na hawataki kumtafuta. Hawa wanamuhitaji muhubiri kwani, hawakubali ‘orthodoxy’ wala hawapingi. Hawa mambo ya msalaba wa Yesu ni upumbavu, wanatabia ya wale Wagiriki wasomi wa nyakati za Paulo, ambao kwao msalaba ulikuwa ni upumbavu. Wao usiwaambie kuhusu damu ya Yesu, ni afadhali uwaambie kuhusu vikoba, mikopo ya benki, mitihani ya bodi na kadhalika. Wanasahau usemi huu, “sanda haina mifuko” yaani, utakapokufa hautakwenda na pesa mifukoni wala PHD kichwani. 1Kor 1:18
Rai yangu kwako ni tumwamini Mungu mkuu, Baba wa Bwana wetu Yesu Kristo na Yesu Kristo ambaye Baba alimtuma ili atukomboe. Chukua nafasi hii kugeukia usahihi ikiwa uko katika kundi lolote kati ya hayo. Kitendo cha kuwepo kwenye kundi moja kati ya hayo manne kinatosha kukupeleka jehanamu ya moto hata kama haupo kwenye makundi mengine matatu. Tutubu na kuiamini injili. Tutembee katika usahihi. Right thinking about God!!!!

0 comments :