Mabaya hayatakupata wewe

1:17:00 PM Unknown 0 Comments

 
MABAYA HAYATAKUPATA WEWE
(Hata baya litageuka na kuwa jema kwako)

Mungu haleti mabaya; hata kama yakitokea  huyageuza mabaya kuwa mazuri. Kwa wenye tumaini hata wanapoona jambo lenye sura ya kutisha bado wanaamini halitakuwa la kuwadhuru. Wana wa Israeli wakiwa utumwani Babeli, walipatwa na machungu mengi;  hawakuwa na makazi,  tena walitengana na ndugu zao. Katika kizazi chetu cha sasa hatujaonja hali ya utumwa wa kitaifa. Kama ilivyokuwa kwa wana wa Israeli, zamani watu walichukuliwa toka Afrika kama watumwa na kupelekwa Ulaya kufanyishwa kazi nzito. Si rahisi mtumwa kuamini kama bado Mungu ni mwema kwake.
Wana wa Israeli hawakujua mabaya hayo yangekuwa mpaka lini. Hawakujua ukomo wa utumwa wao. Katikati ya shida yao (utumwa) Mungu ananena kwa kinywa cha nabii Yeremia kwamba anawawazia mema. Anapanga mizuri kwa ajili yao kwa hiyo wasiogope. Maana nayajua mawazo ninayowawazia ninyi, asema Bwana, ni mawazo ya amani wala si ya mabaya, kuwapa ninyi tumaini siku zenu za mwisho.” Yeremia 29:11
Si rahisi kwa mtu aliyekatika shida kuamini kwamba Mungu anampango mzuri na maisha yake. Katikati ya ombwe la kukosa ajira lazima uamini Mungu anampango mzuri na wewe. Katika hali ya kuugua lazima ujipe moyo kwamba Mungu anampango mzuri. Katikati ya kutengwa na kuachwa bado lazima utambue Mungu ana kusudi jema. Katika hali ya utumwa Mungu anasema na Israeli kwamba mambo yatakuwa mazuri.
Njia za Mungu ni juu sana. Pale ambapo adui anapanga mabaya na kuleta utumwa Mungu hugeuza mabaya hayo na kuwa mazuri. Wakipanga kukwamisha watajikuta wanakufungulia njia bila wao kujua.
Tyndale Mwingereza ambaye ni mmoja kati ya watafsiri wa awali walioandika Biblia katika lugha ya kiingereza anahusishwa na simulizi zenye mafunzo mengi. Tyndale alifanya kazi kama mtafsiri katika nyakati ambazo Biblia ilikuwa katika lugha ya kilatini na haikuruhusiwa kutafsiri kwenda lugha nyingine. Kwa nia ya kumkwamisha, Askofu mmoja wa Durham alinunua nakala zote za Biblia toka kwa mwuza vitabu kwa nia ya kwenda kuziharibu, akidhania kwamba jambo hilo lingekwamisha kazi ya Tyndale. Badala yake pesa hiyo ilitumika kununua malighafi zilizoandaa toleo jipya na bora zaidi. Tyndale alipohojiwa akiwa gerezani alitakiwa amtaje aliyemfadhili katika uandishi wa toleo bora la Biblia alisema ni Askofu Durham. Nadhani umeona walipanga kumkwamisha kwa kununua Bibla zote na kuzichoma wasijue ya kwamba, pesa yao inaweza kusaidia kuandaa toleo bora zaidi.
Tangu kale mpaka sasa Mungu ni mwema. Kila mahali wanasema Mungu ni mwema wala huna haja ya kuogopa. Yesu Kristo ni mfalme na alikuja kutuokoa, lakini njia aliyoitumia kutuokoa haikueleweka mioyoni mwa wengi. Wengi walidhani mfalme atatuokoa kwa kutumia vita wala si kwa njia ya msalaba. Wengi waliona msalaba kama njia dhaifu, walitegemea kuona farasi wa moto, mabomu na mikuki, kwao kufa msalabani haikuwa njia sahihi ya kutuletea wokovu.
Oh! ilionekana ni njia dhaifu kumbe ni njia sahihi na kamilifu. Endelea kumtumaini Mungu, mwombe akuletee wokovu lakini usichague njia. Hata kama hatuoni wala kuzielewa njia za Mungu bado twaweza kuziamini. Don Moen mwimbaji wa nyimbo za injili mwenye alama amerekodi maneno haya kwa uchache nanukuu: “He (God) works in ways we cannot see” (Mungu hufanya kazi kwa namna tusiyoweza kuona)
Hata shetani hakujua kwamba kwa njia ya msalaba watu watakombolewa. Angelijua asingelimchinja Yesu Kristo. Hawakujua kwa njia ile dhaifu BWANA anatupatia ushindi. Mwenye hekima mmoja anasema: “When the devil killed Jesus, Jesus Killed the devil.” Yaani, “Pale shetani alipomuua Yesu, Ndipo Yesu alipomuua shetani.” Endelea kumwamini Mungu.

0 comments :