Linda Maamuzi yako ...

8:24:00 PM Unknown 0 Comments

LINDA MAAMUZI YAKO, HASA WAKATI UNAPOKUTANA NA CHANGAMOTO
Je baada ya miaka mitano au kumi au baada ya muda kupita kutoka sasa, utajipongeza kwa uamuzi uliochukua au utajilaumu? Utafurahi na kushangilia au utajutia na kutamani kurudi nyuma ili kusahihisha uamuzi uliochukua? Kumbuka kila kitu kipo katika uweza wa mtu mwenyewe na anawajibika kwa matokeo yote ya uchaguzi na uamuzi wake.
Maamuzi yako ya leo yana sehemu kubwa sana katika kuamua (determine) hali yako ya baadae kiroho, kiuchumi, kihuduma na hata kifamilia; lakini pia maamuzi yako ya leo yana sehemu kubwa katika kuamua hali ya baadae ya watu wanao kuzunguka. Kesho yako, unaiamua leo kwa kujua au kwa kutokujua. Maisha yako ya kesho yamefungwa katika maamuzi yako ya leo. Kesho nzuri inajengwa na maamuzi mazuri ya leo; maamuzi yako ya leo ni ‘mbegu’ unayopanda, ndani yake imebeba maisha yako ya kesho (maisha ya baadae).
“Kesho nzuri inajengwa na maamuzi mazuri ya leo; maamuzi yako ya leo ni ‘mbegu’ unayopanda, ndani yake imebeba maisha yako ya kesho.”
Jambo kubwa ambalo adui anawinda wakati mtu anapitia changamoto fulani katika maisha, ni maamuzi yake; rafiki yangu hupenda kusema, “Kwa mtu mwenye njaa hata sumu kwake huwa ni chakula” ikiwa na maana kwamba, mtu anaekutana na changamoto anaweza kufanya maamuzi hata yatakayomdhuru yeye mwenyewe baadae. Mtu huyu anafanya maamuzi kulingana na hali ya changamoto anayokutana nayo wakati huo. Ndio maana ni muhimu sana kulinda na kuwa muangalifu na maamuzi unayofanya hasa wakati wa changamoto (challenge).
Shauku ya adui ni kuona unakosea kuamua. Mara nyingi “presha” ya jambo inapoongezeka ni rahisi sana kusahau au kutokuzingatiza mambo ya msingi uliyokwisha kuamua au kuyajua kabla ya jambo hilo kutokea. Presha ya mazingira unayoyaona sasa inaweza kukusahaulisha dira na malengo makuu ya maisha. Mtu anapopitia wakati mgumu, huweza kufikiri ndio mwisho wa maisha yake, au mwisho wa ndoto na mipango yake. Ukweli ni kwamba hakuna changamoto itakayo dumu milele.
Esau alifanya uamuzi wa kuidharau na kuiuza haki yake ya mzaliwa wa kwanza kwa mlo mmoja na hivyo akaikosa Baraka inayoambatana na haki hiyo. Maamuzi ya siku moja yaliharibu na kubadili kabisa uelekeo wa maisha yake na uzao wake (Mwanzo 25:29-34, Ebr 12:16).
Kabla ya kufanya uamuzi au uchaguzi fulani katika maisha, ni muhimu kuangalia picha ya mbele ya maisha unayoyataka. Kuamua kwa kuangalia mazingira yanayotuzunguka hakutupi uhakika wa kufikia malengo makuu katika maisha. Ndio maana ni muhimu kuwa na maono na ndoto inayokupa picha ya maisha ya baadae na kutupa msingi wa kujengea maamuzi yetu ya kila siku ili kufikia ndoto hizo.
Na hiki ndicho lilichomsaidia Yusufu kusonga mbele pamoja na changamoto zote alizokutana nazo hata kufikia ndoto na picha ya maono ya maisha yake ya kuwa kiongozi mkuu katika jamii. Kwa Yusufu, changamoto hazikuwa kikwazo bali jiwe la kukanyagia ili kufikia ndoto yake. Changamoto zilimpa nguvu ya kusonga mbele huku akijua Aliyeahidi ni Muaminifu na kwamba atatenda sawa sawa na alivyoahidi katika Neno lake
“Lakini akiiona ahadi ya Mungu hakusita kwa kutoamini, bali alitiwa nguvu katika imani, Akimtukuza Mungu. Huku akijua hakika ya kuwa Mungu aweza kufanya yale aliyoahidi” Warumi 4:20-21 (Msisitizo umeongezwa).”
Tunaweza kupoteza muelekeo katika kuamua pale tunapoacha kuangali ahadi ya Mungu na kuanza kuangalia mazingira au hali zinazotuzunguka kwa wakati huo. Kumbuka jambo hili; Mungu anapokupa wazo au maono (vision), mara nyingi mazingira yako hayatalingana na maono hayo. Wakati Habakuki anapitia changamoto pamoja na jamii yake, hili ndilo lililokuwa jibu la Mungu kwake ili kumsaidia kulinda maamuzi yake na jamii yake kwa wakati huo;
“…Bwana akajibu, akasema, iandike njozi (ndoto, maono) ukaifanye iwe wazi sana katika vibao, ili aisomaye apate kuisoma kama maji. Maana njozi hii bado ni kwa wakati ulioamuriwa, inafanya haraka ili kuufikilia mwisho wake, wala haitasema uongo; ijapokawia, ingojee; kwa kuwa haina budi kuja, haitakawia” Habakuki2:2-3 (Msisitizo umeongezwa)