Fikra huru kamwe hazifungwi

7:42:00 PM Unknown 0 Comments


FIKRA HURU KAMWE HAZIFUNGWI
Mwili waweza kufungwa lakini fikra huru kamwe hazifungwi. Huwezi kubaki jela kama tayari akili yako iko nje kwenye uhuru. Kuwa na fikra chanya na sahihi ni oparesheni (brain surgery) unayoweza kuifanya mwenyewe. Ili kuwa na fikra chanya hauhitaji kwenda hospitali ya Apollo nchini India au kule John Hopkins Marekani , unahitaji taarifa sahihi tu. Neno la Mungu ambalo ni Habari njema ndio taarifa sahihi. Neno la Mungu ni taa ya miguu yetu, hutupa hekima kuliko watu wa rika letu. 
Kupata mtazamo chanya ni operesheni rahisi kuliko kuwa na mtazamo hasi. Matatizo mengi ambayo huwapelekea watu kwenda kwa waganga wa kienyeji yana majibu katika mfumo wa maandishi, majibu hayo yako katika biblia na katika maduka ya vitabu. Badala ya mkono wa albino iko elimu ya ujasiliamali, wako akina Kiyosaki wanatoa elimu hiyo. Wako akina Brian Tracy wanatoa elimu ya masoko.
“Shida yako inafanana na gereza, gereza linaweza kuwa na ukuta mrefu, lakini ni wazi pale ambapo mwanadamu hawezi kupanda kwa mikono na miguu anaweza kupanda kwa kuwa na mtazamo (mawazo) sahihi.”
Viko vitabu vya namna ya kujenga mahusiano bora vinavyoliwa na mchwa ilhali kuna mtu anaoga dawa barabarani bila nguo ili apendwe na mumewe. Hilo nalo ni gereza lililowafunga wengi. Naamini Ili uende kwa mganga wa jadi au kienyeji (mchawi) ni lazima ukamilishe mambo matatu: uwe na akili nyeusi, mtazamo feki, na roho nyeusi. Wapendwa tujifunze kwenda katika maduka ya vitabu, ili akina sangoma na wasoma nyota wajumuike katika sera ya kilimo kwanza.
Shida yako inafanana na gereza, gereza linaweza kuwa na ukuta mrefu, lakini ni wazi pale ambapo mwanadamu hawezi kupanda kwa mikono na miguu anaweza kupanda kwa kuwa na mtazamo (mawazo) sahihi. Unajua katika shida watu hulia, hatutegemei kumuona mfungwa anacheka, au anaimba kwa furaha. Ukiona mfungwa anaimba kwa shangwe ujue yuko gerezani kimwili bali akili yake iko nje ya gereza.
Hiki ndicho kilichotokea kwa Paulo na Sila, kwa kawaida usiku wafungwa hulala tena hugeuka kwa filimbi, wafungwa hawaimbi usiku. Unajua ili tujue kwamba wewe si mfungwa hauhitaji kuseme, ‘mimi si mfungwa’ matendo yako yakiakisi mtu huru tutajua wewe u huru kweli.
“Unaweza kuwafunga watu elfu kumi (10,000) wanaolia na kulalamika, lakini huwezi kumfunga mtu mmoja anayesifu na kumwabudu Mungu..”
Paulo na Sila kimwili walikuwa jela ila kimtazamo walitambua wao si wafungwa. Wakati wafungwa wamelala wao walianza ibada, mtazamo wao ni wa nje ya gereza. Mfungwa hafanyi ibada bila kibali wakati wa usiku. Ukiona ana ujasiri huo basi ujue huyo si mfungwa. Mtazamo wa Paulo na Sila uliwazalia matunda na wakatoka. Mwenye hekima mmoja anasema, “Unaweza kuwafunga watu elfu kumi (10,000) wanaolia na kulalamika, lakini huwezi kumfunga mtu mmoja anayesifu na kumwabudu Mungu.”
Inawezekana wewe pia una shida lakini ukuta ni mtazamo wako, labda uko jela ya kukosa kazi au mtoto; badilisha mtazamo wako, tembea kama mtu huru. Nakumbuka wakati sina kazi, nilikuwa na upako kuliko waendao kazini, nilikuwa nina sababu za kumshukuru Mungu kuliko wafanyakazi wa Benki Kuu ya Tanzania hata ya Washington DC. Nilitoa sadaka kama kawaida.
Siku nyingine nilikuwa navaa vizuri kama boss! Moyoni najua sina kazi. Nilikua naombea wengine kazi utadhani mimi ninayo. Mtazamo huru ulinivusha. Ukipata kazi utafanya nini? Fanya sasa. Paulo na Sila hawakusema tukitoka jela tutakusifu, walimsifu Mungu wakiwa jela kinyume cha sheria za bwana jela. Mtazamo huru ni kutenda bila kizuizi.
Jela ni kizuizi, lengo lake ni kukuzuia. Jela huzuia kicheko, jela huzuia tabasamu, jela hunyima usingizi, jela hutuzuia tusimsifu Mungu wala kutoa sadaka ya shukrani. Tukiweza kucheka, kutabasamu, kusifu na kushukuru basi tu watu huru, na milango ya gereza itafunguka.
Akili yako ikishatoka jela, mwili utakufuata tu. Unaposifu unaunganika na Mungu, unaalika mbingu duniani. Mungu hakai jela akishuka sehemu inabadilika jina, pengine aliposhuka huitwa Jehova Jire, mahali pengine Ebenezer na Jehovah Shama. Hawezi kushuka na eneo likabaki vile vile. Aliposhuka wafungwa wote walikuwa huru, Paulo na Sila wakageuka wahudumu na si wafungwa tena. Nadhani badala ya kupaita gereza la ukonga au segerea palipata jina lingine. Leo hii watu huenda Ugiriki kutazama mahali ambapo Paulo na Sila kwa sifa za BWANA waliandika historia ya ushindi. Mungu aliyeweka siku ya kuanguka kwako ndiye atakayeleta siku ya kusimama kwako. Hebu msifu BWANA na tetemeko litokee kwako leo kama wakati wa Paulo na Sila. Amen