Ili kufikia malengo yako

2:10:00 PM Unknown 0 Comments

 
ILI KUFIKIA MALENGO YAKO
Kila mwaka mpya unapoanza watu wengi huwa na kawaida ya kujiwekea malengo katika mwaka husika. Karibu kila mtu au mahali huzungumia mipango au malengo anayotamani na kujipangia; Lengo ni kupata taswira ya mahali ambapo mtu anataka kwenda au kufanikisha katika mwaka huo. Hili ni jambo zuri kwa kuwa linaleta hamasa, nguvu na matumaini ya kusonga mbele katika maisha ya kila siku; kwa kuwa kama mtu hajui anapotaka kwenda (hana malengo au mipango) njia yoyote itamfikisha.
Changamoto moja ambayo hutokea ni kwamba watu wengi huwa na hamasa kubwa juu ya kuweka na kutamani kutimiza malengo yao mwanzoni mwa mwaka; lakini kadiri muda unavyozidi kwenda hamasa na nguvu ya kuyaendea malengo waliojiwekea hupungua au hutoweka kabisa. Na hivyo wanapofika mwisho wa mwaka wanagundua kuwa hawana kitu cha kuonesha au wanakitu kidogo tu ukilinganisha na malengo waliokuwa nayo wakati wanaanza mwaka.
Jambo hili tunaweza kuliona hata kwa wanaisraeli walipokuwa wanatolewa katika utumwa na kupelekwa katika nchi yao ya ahadi. Wakati wanatoka walikuwa na hamasa kubwa na nguvu na matumaini ya kufikia nchi ya ahadi; lakini kwa kadiri walivyokuwa wanaendelea na safari hamasa, matumaini na nguvu ya kufikia ahadi iliyokuwa mbele yao ilikuwa ikipungua kwa baadhi yao. Ukitizama safari yao utagundua kuwa kilichofanya hamasa na matumaini yao kupungua kadiri walivyosonga mbele, ni kitendo cha wao kuacha kuangalia (Paying attention) Ahadi na kuanza kuangalia changamoto walizokuwa wanakutana nazo njiani.
Je unapokutana changamoto katika mipango uliojiwekea katika mwaka huu, unachagua kuangalia nini? Unaangalia changamoto au unaangalia malengo yako? Ukitumia muda mwingi kutafakari changamoto uwe na uhakika hamasa na nguvu hupungua na hatimaye huweza kutoweka kabisa. Lakini ukitumia muda wako kutafakari malengo yako na kutafuta namna ya kufanikisha (Mfano; Kutafuta maarifa zaidi kwa kusoma vitabu au kurudi shule tena, kutenga muda mwingi zaidi wa kufanyia kazi jambo hilo, kutafuta ushauri, kujifunza kwa waliokutangulia/ waliofanikiwa, kurudia tena uliposhindwa mara ya kwanza n.k) uwe na uhakika mwisho wa mwaka au muda uliojiwekea  utakuwa na kitu cha kuonesha na sio maneno matupu ya kwanini ulishindwa.
Katika kufikia malengo au mipango uliojiwekea mwanzoni mwa mwaka au mwezi au kipindi chochote kile changamoto hutokea au naweza kusema haziepukiki kwa namna moja au nyingine. Changamoto ndizo zinatufanya tushangilie na kuwa na moyo wa shukrani pale ambapo tumefikia malengo hayo. Kumbuka jambo hili: Kama ni rahisi (hakuna changamoto) kila mtu angefanya. Changamoto haziji ili kufisha ahadi yako, bali zinakupa fursa ya kuona Ukuu na Utukufu wa Mungu kwa namna ambayo hujawahi kuona. Ni changamoto ya wanaisraeli ndio iliyofanya tutambue Mungu anaweza kufanya njia mahali pasipo na njia. Mtu hapewi tuzo kwa kusimulia namna changamoto zilivyomkwamisha; hupewa tuzo kwa kuonesha namna gani ameweza kufikia malengo yake katikati ya changamoto.
There’s a place for you at the top!

0 comments :