Mungu Anakutazama

10:05:00 AM Unknown 0 Comments

MUNGU ANAKUTAZAMA
(Maovu na mema yote hutendeka mbele ya macho ya Mungu)
Katika tasnia ya michezo, wengi wetu tumezoea kucheza vizuri mahali ambapo mashabiki au watazamaji ni wengi. Si wachezaji wengi wanaweza kujituma na kucheza kwa bidii sirini. Wengi hupenda kucheza vizuri wakiwa wanatazamwa na maelfu ya mashabiki jukwaani. Si ajabu ndio maana viwanja kama Old Trafford na Stanford Bridge (viwanja vya soka) huchukua mashabiki wengi, na wachezaji hujiona wabarikiwa wakisakata katika nyasi hizo.
Lakini ni lazima tujue wazi kwamba, Mungu ni mkuu kuliko watazamaji, anaona ndani ya mioyo yetu na hata nafsini mwetu. Ufanisi wake katika kuyatazama maisha yetu ni mkubwa kuliko mamilioni ya mashabiki wasioweza kutazama mpaka moyoni. Mwenye hekima mmoja anasema, “You’re for an audience of one: GOD ” akimaanisha, “Tunaishi kwa ajili ya kusanyiko la mtazamaji mmoja; MUNGU.” Tunapaswa kulenga kumpendeza yeye na kumtukuza yeye peke yake ambaye kwa nyakati zote hutuona.
Ikiwa kusanyiko unalolenga kulipendeza ni la watu, basi uwe na hakika mwenendo wako utakuwa mbaya katika nyakati ambazo hawakuoni, na ikiwa unalenga kumpendeza Mungu mwenendo wako utakuwa safi nyakati zote. Mungu akiwa ndio kusanyiko lako, basi utaishi vema maana yeye anapatikana mahali kote, si uwanjani wala ukumbini tu; bali yuko nasi gizani na nuruni, asubuhi, mchana jioni hata usiku.
Kitendo cha Adam na Eva (kabla ya anguko) kuishi bila nguo, tena bila ya kuona aibu kilikuwa ni alama ya uaminifu na hali ya kuwa bila hatia mbele za Mungu. Hawakuwa na kitu cha kuficha mbele za Mungu, hawakusongwa na jambo lolote ambalo lingewafanya waone aibu mbele za Mungu. Mwanzo 2:25
Kundi kubwa leo tumekuwa na sura tatu, ile ambayo jamii inaijua, ile ambayo sisi na Mungu tunaijua, na ile ambayo Mungu peke yake huijua. Ni muhimu kuwa na sura moja isiyobadilika, ni vema kutokuwa vuguvugu tena ni muhimu kukataa unafiki ambao tafrisiri yake rahisi ni kuwa na sura nyingi (many faces).
Mtu mmoja alisifika sana ofisini ilhali nyumbani kwake hawakuwa na furaha naye kabisa, alikuwa mwema kwa watu wasio wake na aliwatesa walio wake. Sura yake ya nyumbani ilikuwa tofauti na u-malaika aliouonesha ofisini. Ni msemo wa kutisha na usiotakiwa, “saint at abroad and devil at home.” Yaani, “Mtakatifu akiwa mbali, shetani nyumbani.” Ni muhimu kutafuta sura moja, nyumbani na ugenini, usiku na mchana, chumbani na nje ya chumba.
Dhambi zote hutendeka mbele ya macho ya Mungu. Tafakari hili neno, mbele ya macho yake. Kila dhambi tutendayo tunamkosea Mungu peke yake. Maumivu ya dhambi humwelekea Mungu ndio maana kuna nyakati hushindwa kuvumilia. Usije fikiri hata mara moja kwamba, unajikosea au unamkosea jirani, mara nyingi tunapokosa tunamkosea Mungu. Unapomtendea jirani yako uovu unamtendea Mungu. Inatisha kwani mabaya yote hutendeka mbele ya macho yake.
Tafakari na kuchukua hatua, Mungu yuko tayari kusamehe nyakati zote.

0 comments :

Ninapotoa dhabihu ya shukurani

2:29:00 PM Unknown 0 Comments

NINAPOTOA DHABIHU YA SHUKRANI “
“Atoaye dhabihu za kunishukuru, ndiye anayenitukuza (anayeniheshimu); anaanda njia ya Mimi kumuonesha wokovu wa Mungu” Zab 50:23 (NIV)
Ili uweza kutafakari mstari tajwa hapo juu ni vema uweke jina lako au ujitazame katika mstari huo. Ni wewe unayemtukuza? Je, ni wewe unayejiandalia njia ya wokovu wa Mungu? Mara nyingi watu hufanya jambo baada ya kutambua uzito au umuhimu wa jambo hilo. Si watu wengi sana wanaelewa umuhimu wa kuwa na moyo wa shukrani mbele za Mungu; hivyo ni rahisi sana kwa mtu kuomba akiwa na hitaji, lakini ni watu wachache sana wanaokumbuka kushukuru baada ya kujibiwa mahitaji yao.  Lakini pia, Mbali na kumshukuru Mungu baada ya kujibu maombi yako, unaweza kujizoeza au kujifunza kuwa na moyo wa shukrani mbele za Mungu kama tabia au mtindo wa maisha yako (A grateful heart).
Kuna tofauti kubwa kati ya kushukuru baada ya Mungu kujibu ombi la mahitaji yako na kuwa na moyo wa shukrani. Moyo wa shukrani ni zaidi ya kushukuru, ni mfumo au utaratibu wa maisha ya mtu. Kushukuru kunaweza kutokea mara moja au kwa msimu, lakini moyo wa shukrani ni tabia au mfumo wa kimaisha endelevu.
Ni mtu mwenye moyo wa shukrani pekee ndiye anayeweza kumshukuru Mungu katika kila jambo. Kumbuka kuna tofauti ya kumshukuru Mungu kwa kila jambo na kumshukuru Mungu katika kila jambo. Tafasiri ya kiingereza ya 1 Wathesalonike 5:17 inasema “toeni shukrani kwa Mungu katika kila hali/jambo kwa kuwa hayo ni mapenzi ya Mungu kwenu” (tafasiri isiyo rasmi). Kinachowafanya baadhi ya watu washindwe kumshukuru Mungu ni hali ya kutokuamini kwamba hayo ni mapenzi ya Mungu. Tukijua kwamba yatupatayo ni mapenzi yake, tutapenda kumshukuru hata kama mambo hayo yameleta simanzi.
Moyo wa shukrani unamfanya mtu ahesabu Baraka za Mungu katika maisha yake kuliko changamoto zake. Ni moyo wa shukrani pekee ndio unaoweza kumfanya mtu aone Mungu ni mkubwa kuliko hali yake. Moyo wa shurani humfanya mtu kuacha kulalamika juu ya kile ambacho Mungu hajajibu na kuanza kumshukuru Mungu juu ya kile ambacho amewahi kujibu.  Moyo wa shukrani hutafuta sababu ya kumshukuru Mungu katika kila jambo na kila hali. (Zab77:2, 6-10,11-19)
Mtume Paulo alipopelekwa gerezani naweza kusema bila shaka hakumshukuru Mungu kwa kutupwa gerezani lakini nina uhakika kuwepo kwake gerezani hakukumzuia kumshukuru na kumsifu Mungu. Hii inatupa kuona kuwa inawezekana kumshukuru Mungu katika kila jambo, na huu ndio moyo wa shukrani yaani mfumo wa Maisha.  (Matendo ya Mitume 16:25-26)
Moyo wa shukrani unatoa fursa kwa Mungu kudhihirisha wokovu wake. Kwa lugha rahisi, moyo wa shukrani hutoa fursa kwa nguvu za Mungu kuwa tayari muda wote (standby) ili kukusaidia utakapohitaji; ndio maana mstari wetu wa kutufungulia hapo juu unasema, “anaandaa njia ya Mimi kumuonesha wokovu wangu”. Moyo wa shukrani huvuta upendeleo (kibali) wa Ki-Mungu katika maisha ya mtu kuliko anavyoweza kufikiri. Ningeweza kusema, kushukuru kunavuta wingu la upendeleo wa Ki-Mungu (God’s favor); lakini Moyo wa shukrani hushikilia wingu la upendeleo wa Ki-Mungu ili kukaa katika maisha ya mtu (cause it to dwell).

0 comments :

Jina lako nani?

1:14:00 PM Unknown 0 Comments


JINA LAKO NANI?
( Unajionaje nafsini mwako )
Zamani tulifuga mbwa na tuliwita jina kaburu, tulitaka awe mkali kama wale makaburu wa Afrika ya kusini. Makaburu hawakuwa na sifa njema, waliwatesa sana watu weusi kule nchini Afrika kusini. Waliwatendea kwa ukali na kwa ukatili mkubwa na hata kuwaua.
Mbwa yule alikuwa mkali sawa sawa na jina lake, alipokwenda kung’ata hakupiga kelele aling’ata kimya kimya. Mbwa yule alituletea kesi kadhaa za kuuma watu nyakati za asubuhi. Iko nguvu ya ajabu katika jina na katika namna unavyojiona wewe mwenyewe. Mtu hufanana na namna anavyojitazama ndani yake.
Unapoitwa jina lenye kukupinga au lenye kuashiria ulegevu na laana unapaswa kulikataa, au kuwa na mtazamo mpya ndani yako ili maisha yako yafanane na jina lako. Ukiitwa jina Shida, Mwadawa, Maganga, Sikitu, Lameck na majina mengine yafananayo na hayo ni lazima uyakatae na kuchagua jina jema. Hata kama watu wasiojua wataendelea kukuita kwa majina mabaya lakini tayari ndani yako utakuwa unajua wewe ni mtu tofauti. Utakuwa unajua wewe ni hodari, wewe ni tariji, wewe ni taifa takatifu na tena ni mtu wa mafanikio.
Moja ya watu wanaofanikiwa sana katika utawala ni wale wenye majina ya Benjamini tafsiri ya hili jina ni, mtu wa mkono wa kuume au kwa lugha nyingine ni mtu mkubwa. Mimi nawafahamu Benjamin wachache tu ambao walifanikiwa kuwa watu wakuu, Benjamin Mkapa alikuwa Rais wa Tanzani, Benjamin Franklin aliongoza huko Marekani na hata sasa Benjamin Natanyahu anaongoza huko Israel.
Wakati wa kuzaa kwake Raheli mke wa Yakobo alishikwa na utungu mkuu, na katika kujifungua kwake huko alifariki. Ikawa wakati wa kutoa roho yake alimwita mtoto wake jina Benoni, maana yake mwana wa uchungu wangu lakini Yakobo babaye alikataa asiitwe Benoni akasema aitwe Benjamini maana yake, mtoto wa mkono wangu wa kuume (mtawala) na tazama Benjamin alikuwa mtu mkubwa. Mwanzo 34:18
Na Yakobo anapombariki Benjamin anamfananisha na mbwa mwitu, mtu imara na mwenye nguvu ya kutafuta asubuhi na usiku, mtu asiyeishiwa chakula. Ninaamini kama angeliitwa Benoni asingeliweza kuwa shupavu na mwenye akili kama namna alivyokuwa. Mwanzo 49:27
Kabila la Benjamin lilikuwa na heshima na umahiri mkubwa (brave and active) kwa kuwa liliambiwa litaketi mkono wa kuume ambao ni mkono wa heshima kuliko kushoto (Zaburi 80:17). Ni kabila lililopigana vita mara nyingi na kushinda na kujitwalia nyara kama mbwa mwitu anayejitajirisha kwa vitoweo. Kila kilichonenwa katika jina la Benjamini, kilitokea katika kabila la Benyamini. Watu wake walikuwa hodari na watawala wenye nguvu vitani. Sauli na Yonathani mwanaye moja ya viongozi na mashujaa kutoka katika kabila la Benjamin na wasomaji wa Biblia wanajua jinsi walivyokuwa watu hodari kwa vita na katika uongozi. {1Samweli 9:1, Waamuzi 20:21-25, 3:15, 5:14,}
Wewe ni mtu muhimu sana katika kujenga Ufalme wa Mungu hapa duniani. Jina lako linabeba lile kusudi (mission) ambalo Mungu alilokuumbia ulitekeleze. Chunguza maana ya jina lako.  Kataa maana mbaya zote za jina lako, litakase kwa damu ya Yesu na nenea mazuri jina lako.

0 comments :

Nani analeta maana...!

1:27:00 PM Unknown 0 Comments


NANI ANALETA MAANA KATIKA MAISHA YETU
(Mungu ndiye huleta maana katika maisha ya mwanadamu) 
Siku moja nilisoma mtandaoni mtu ameandika kiboko ya wachungaji wenye walinzi binafsi (board guards) ni hii Zaburi ya 127:1-2, nikacheka sana. Ninachoweza kuandika ni kwamba, hata kama wanadamu wanahusika Mungu lazima ahusishwe pia.  Imeandikwa, “1. Bwana asipoijenga nyumba Waijengao wafanya kazi bure. Bwana asipoulinda mji Yeye aulindaye akesha bure. 2. Kazi yenu ni bure, mnaoamka mapema, Na kukawia kwenda kulala, Na kula chakula cha taabu; Yeye humpa mpenzi wake usingizi.

Tafsiri ya huo mstari ni kwamba, usiingie kwenye mradi (project) ambao Mungu haufanyi. Usiwekeze nguvu zako mahali ambapo Mungu hawekezi. Usilinde asipolinda, ukisikia analinda basi hapo na wewe kalinde. Kwa lugha nyingine ni kwamba, fanya pamoja na Mungu. Shirikiana na Mungu katika kazi zako, Do not try to work alone! Ukishaona Mungu hayumo katika mchakato fulani lazima ujue matokeo yatakuwa sifuri. Magumu na mabaya yaliyowapata Adamu na Eva yalitokana na kutengana na Mungu. Hata asingewalaani kwa kinywa chake bado matokeo ya kazi zao na maisha yao ingekuwa ni sifuri. Alama ya juu unayoweza kuipata unapotenda jambo bila ya Mungu ni sifuri (bure). Petro alionja sehemu ya laana ya  hawa wazazi wa kale yaani, Adamu na Eva baada ya kukesha usiku kucha katika uvuvi na kuambulia sifuri. We need Jesus! Luka 5:5

 Zamani niliona nembo (logo) ya shule moja imeandika, Life – Jesus = 0 yaani, maisha bila Yesu ni sifuri. BWANA Yesu ndiye anayeleta maana ya michakato yote ya maisha yetu. Mfumo wetu wa elimu bila Yesu ni bure, mfumo wetu wa ulinzi bila Yesu ni bure. Kazi bila Yesu ni sifuri, utajiri bila ya Mkono wa BWANA ni sifuri pia. Hakuna jambo ambalo linamuhusu mwanadamu ambalo Mungu hataki kushiriki. Kwa kuwa linamhusu mwanadamu linamhusu Mungu pia. Yesu alikwenda harusini kana ya Galilaya (Yohana 2), Yesu alikwenda msibani Lazaro alipokufa (Yohana 11), Yesu alikwenda kazini kwa Petro ambapo ni baharini kwa kuwa alikuwa mvuvi. Yesu alikwenda kushinda nyumbani kwa Zakayo na mara nyingine kwa Martha na Mariamu.

Ingawa kanisa lilikabidhiwa kwa Petro bado Kristo ndiye alikuwa mjenzi. Alimwambia, “Na juu ya mwamba huu nitalijenga kanisa langu” yaani, mjenzi ni Kristo (Mathayo16:18). Neno nitalijenga linaonesha wazi si Petro ambaye atajenga bali ni Yesu aliyemmiliki wa kanisa ndio atakayejenga; maana anasema, na juu ya mwamba huu (Petro) nitalijenga kanisa langu. Anahusika na furaha na huzuni zetu, anahusika na taaluma na siasa zetu. Ni BWANA wa watu wote tena ni BWANA  wa vitu vyote. Nadhani unafahamu mwenye nyumba anaweza hata asishike tofali lakini kwa kuwa ndiye aliyenunua kila kitu na ndiye anayetoa vitendea kazi huhesabika kuwa anajenga. Utasikia najenga huko mbezi au Madale. Anayetoa nguvu, vitendea kazi, ramani na maelekezo ndiyo mjenzi. Kristo ndiye mjenzi wa Kanisa wala si mtume, nabii, mchungaji wala kasisi.

Tunapotenda tukiwa na Mungu matokeo huwa makubwa na kazi huwa nyepesi kama usingizi. Tukiwa na Mungu tunaweza kupata matokeo makubwa (Big Results Now BRN); maandiko husema, “Yeye huwapa wapenzi wake usingizi.” Ni kama Petro alivyopata matokeo makubwa baada ya kutii, Utii wetu kwa Kristo ni mwisho wa laana. Hakuna hukumu wala laana kwa waliondani ya Kristo. Luka 5:5

Paulo anasema kuishi kwake ni Kristo, vipi wewe? Kuishi kwako ni anasa, ulevi au ni kazi yako?  Kuishi kwako ni mumeo au rafiki yako wa kiume au wa kike? Ni pale tu ambapo kuishi kwako ni Kristo ndipo uko salama. Ni rahisi kusema kuishi kwako ni Kristo kwa kuwa unalijua andika, lakini je, Kristo ndio maisha yako?  Mpaka umekubali kuishi kwako kuwe Kristo, maisha yako hayataleta maana. Kuishi kwetu ni bure ikiwa tuko nje ya Kristo. Flp 1:21

Tafakari na acha maisha yako yalete maana kwa kujitoa kwa Yesu.

0 comments :