Kata kiu yako

10:57:00 AM Unknown 0 Comments

 
KATA KIU YAKO
(Hakuna mbadala wa Mungu)
Mwanzoni nilizani ni gari, baadaye nilidhani ni kazi nzuri, mwishowe nilifikiri ni katika kuoa na kuolewa; kumbe ni uweponi mwa Mungu pekee ndimo ulimo utoshelevu wangu. Mtakatifu Agustino anasema, “Moyo wa mwanadamu hauta tulia mpaka umekutana na muumba wake”.  Ambao hawajaoa hudhani wakioa mioyo yao itatulia, wasio na kazi hufikiri kazi inatoa kitulizo na wasio na pesa nao hutamani kutulizwa kwa kupata pesa.
Nyakati za Ibrahimu, Nuhu, na waamuzi hakukuwa na mabasi ya mwendo kasi,wala hapakuwa na  ipad na kompyuta. Lakini bado watu hawa walikuwa na utoshelevu na amani ya ajabu. Je, amani hiyo waliipata wapi? Watu hawa hawakuwa na lift kwenye majengo yao, wengine hawakuwa hata na nyumba bali waliishi hemani. Lakini sasa licha ya kuwepo kwa mambo mengi mazuri bado wengi wana hali mbaya kuliko zamani, ni wenye uhitaji usiokwisha. Hakuna utoshelevu katika vitu. Paulo ananukuu fikra za Musa kwamba, hata upewe milki zote za Misri bado hautapata utoshelevu. Wakati huo Misri ilikuwa ni tajiri mno na kitovu cha uchumi wa nchi nyingi, pamoja na hayo Musa alijua hakuna utoshelevu ndani yake. [Ebr11:26]
Kuna nyakati nimekuwa na rafiki mzuri anayenipenda sana kila kitu kinakuwa murua kabisa [double double] lakini bado nafsi yangu ililia kwamba, inamtaka Mungu. Hakika, moyo wangu hautatulia popote ila kwa BWANA naam, BWANA peke yake.
Hata umpate mtu atakaye kupenda sana bado moyo wako hautatulia, nafsi yako italilia uwepo wa Mungu. Ayala ambaye ni ndege wa jangwani [kusiko na maji na unyevu] huvitamani sana vijito vya maji vivyo hivyo moyo wa mwanadamu hautanyamaza hata ukipewa vilivyo vinono utaendelea kumhitaji Mungu. Kukosekana kwa Mungu kutakuwa ni kama ukame ndani ya nafsi ya mtu.
Katika kisima cha Yakobo Yesu alikutana na mwanamke Msamaria,aliyekuwa ameolewa na wanaume wa tano na aliyekuwa naye ni wa sita. Lakini Je, alikuwa anatafuta nini kwa waume hao wote sita? Jibu ni rahisi alikuwa anatafuta utoshelevu yaani, alitaka kukata kiu yake.  Yesu akamwambia maji haya unayochota hayakati kiu. Pesa, sigara, wanaume, uasherati, hamu ya kuona picha chafu, wanawake, urembo, utanashati, vyeo na mali za thamani kamwe havitaweza kukata kiu yako.
Mwanamke Msamaria alisimama katika kisima cha Yakobo, lakini Yesu pia alisimama kama kisima. Kwa hiyo kuna kisima cha Yakobo na Kisima kingine ni Yesu Kristo. Ndani ya kisima cha Yakobo mlitoka maji yasiyo kata kiu, ndani ya Yesu Kristo mlitoka maji yakatayo kiu. Na Yesu anamwalika kila mtu aje anywe maji hayo ya uzima na asione kiu tena.
Baada ya Yesu kuzungumza na yule mwanamke mwishowe alikubali na akataka apewa kile kinacholeta utoshelevu kile kinachoondoa kiu yaani, Roho Mtakatifu ambaye ndiye maji yaletayo utoshelevu na kuridhika. Natamani sote tumkimbilie Yesu na kumsihi kwa maneno ya maombi kama alivyofanya mwanamke Msamaria: “Yule mwanamke akamwambia, Bwana, unipe maji hayo, nisione kiu, wala nisije hapa kuteka. ”Yohana 4:15
Samaki huwa katika ubora wake na ufanisi wa juu akiwa majini, mashine huwa katika ufanisi wa juu inapokuwa mpya tena inapowekewa vilainishi [oil] kwa wakati. Vivyo hivyo binadamu huonesha ufanisi wa hali ya juu awepo uweponi mwa Bwana ambamo kuna ushirika wa ajabu na Roho Mtakatifu.
Tafuta kukata kiu yako leo….tukutane chumba cha juu kama wale mia ishirini [120]

0 comments :