Anuani ya Muda

12:00:00 PM Unknown 0 Comments

 
ANUANI YA MUDA
(P.O. BOX 701, MBEYA)
Yesu aliposali alisema, “Baba yetu uliye mbinguni” hiyo ni anuani ambayo kila mmoja wetu anapaswa kuitamani baada ya maisha haya. Ni muhimu mara baada ya kifo tupatikane kwa anuani hiyo ya Mbinguni. Lakini kwa kuwa bado tuko duniani tunajulikana kwa anuani za makampuni, anuani binafsi, shule na taasisi ambazo tunaishi na kufanya kazi ndani yake. Na baadhi labda tuko vijiweni na pengine hatupatikani kabisa [Unreachable].
Inawezekana uko kwenye taasisi ambayo kwa namna moja au nyingine inakupa mateso, Inawezekana uko katika mazingira ambayo kwa namna moja au nyingine hayakupi furaha, jambo moja nataka ujue ni kwamba, uko hapo kwa kitambo tu. Kitambulisho ulichopewa na taasisi yako, anuani unayojulikana kwayo sasa ni ya muda tu, kamwe haita dumu milele. Zamani Nelson Mandela alipatikana kwa anuani ya gereza, waliomtembelea walilazimika kwenda huko; Yusufu pia alipatikana gerezani na mwishowe ikulu. Leo hii wote [Yusufu na Mandela] wanajulikana katika hadithi za kutoka jela mpaka ikulu.  From prison to palace story.
Maisha ya shule au chuo yanaweza kuwa magumu hata mtu akakata tamaa na kuzimia moyo, lakini maisha hayo ni ya kitambo kifupi tu, punde si punde utamaliza na maisha mapya yataanza. Nakumbuka anuani ya, P.O BOX  701, Mbeya ilikuwa anuani yangu ya shule ya Sekondari. Maisha ya shule pale hayakuwa mazuri, kidato cha kwanza wengi walikuwa wanapigwa na kuonenewa bila sababu. Lakini nilijipa moyo na nikamwomba Bwana anilinde ili nitoke salama katika taasisi ile. Niliomba sawa sawa na imani yangu kwa wakati ule, na kweli nilitoka salama. Ilikuwa anuani ya muda tu.
Sijui kwa sasa wewe uko wapi na una amani kiasi gani, lakini ninachojua ni kwamba unapita katika eneo hilo na hutokaa milele katika mateso hayo. Wakati mwingine ni vema kuomba Mungu akupe uvumilivu na namna ya kuishi katika mazingira fulani ili uishi vizuri katika kipindi cha mpito.
Inawezekana Bosi wako ni mkali, inawezekana pia wafanyakazi wenzako hawakutendei vizuri, jipe moyo kwa maana, wewe na wenzako hamta dumu katika taasisi hiyo milele. Cha msingi ni hekima itumike  ili muachane kwa usalama muda ukifika. Biblia inasema katika mambo yote tujipatie sifa njema, kwa hiyo hata katika maeneo yetu ya kazi, biashara na huduma ni lazima tujipatie sifa njema.
Na ili tuishi na watu hatuhitaji watu wabadilike bali tunahitaji kubadilika. Usimsubiri mkali awe mpole, bali wewe uwe mpole, usimsubiri mkorofi awe mtaratibu bali wewe uwe mtaratibu. Kwa hiyo haijalishi uko katika taasisi yenye changamoto namna gani lazima ujue uko hapo kwa muda tu, fanya vizuri na nuia kuacha alama mahali hapo. Upo hapo kwa kitambo tu. Anuani yao si kitambulisho chako cha milele.
Inawezekana sasa unatumia sanduku la posta la kijiji chako lakini ni nani ajuaye kwamba, mwishowe watu watumia anuani ya Ikulu kukupata?  Inawezekana sasa unajulikana kwa anuani ya kampuni ya mhindi lakini ni nani ajuaye kwamba, mwisho wa siku utajulikana kwa anuani ya kampuni yako binafsi? Inawezekana kabisa, pango mipango na kisha anza kuyaendea mafanikio yako.
Nataka nikutie moyo mpendwa, uko hapo  kwa muda tu, siku si nyingi utajulikana kwa jina jema na kwa anuani bora zaidi. Uko hapo ili kujifunza, kama haupati pesa za kutosha usijali, jitahidi upate uzoefu wa kutosha. Tunapofanya kazi tunafanya kwa ajili ya mambo matatu, ama kwa ajili ya Mungu, ama kwa ajili ya pesa, au kwa ajili ya uzoefu. Leo nasisitiza pata uzoefu wa kutosha na pesa zitakuja baadaye, uzoefu unavuta pesa. Uzoefu wa kazi ni pamoja na kujua tabia mbaya za wateja na wafanyakazi wenzako na namna ya kuzikabili changamoto za kitabia.
Daudi na Esta ni watu ambao kwa imani, na kwa ustadi wao walijikuta anuani zao zinabadilika. Walipatikana katika nyumba ya Mfalme ilhali hawakuzaliwa kwa mfalme. Na ndivyo ilivyo hadithi yako usipokata tamaa. Mungu anaweza kukutoa jaani na akakuketisha na wakuu. Endelea mbele. Mpaka wiki ijayo, tukutane katika nyumba ya mfalme, shalom!!!

0 comments :