Kwa kila ambaye....... I

10:11:00 AM Unknown 0 Comments

 KWA KILA AMBAYE HAJAOA AU KUOLEWA - I
(Amua kuwa na familia ya aina hii)
Ni rahisi sana mtu kuwa na ndoto za kumilika gari, nyumba nzuri, kufika mbali kitaalamu na hata kiuchumi. Ni nadra sana kwa vijana wa leo kuwaza kuwa na familia takatifu, ukimpata anayewaza hivyo ni kwa wale wachache wa mazingira ya kanisani. Wengi wanatamani kuwa na familia za kitajiri.
Hakuna shirika la kupima viwango au ubora wa familia, lakini naamini neno la Mungu linaweka kiwango. Kwa dunia ya leo familia bora inapimwa kwa msingi wa kipato, ambao kiuhalisia si msingi imara. Biblia inapozungumza kuhusu mwanamke mpumbavu au mwanaume mpumbavu inaoensha umuhimu wa hekima na maarifa ya kimungu kama msingi imara katika familia. Baba hapaswi tu kuwa na uwezo wa kutafuta na kupeleka mkate nyumbani (breadwinner) bali awe pia na uwezo wa kumpeleka Yesu nyumbani.
Katika maandiko yako maeneo mengi ambayo familia zimetajwa. Lakini kwa kusudi la soma hili naomba tujifunze kwa familia ya Kornelio Yule wa kwenye kitabu cha matendo ya mitume. Huyu ndiye kielezo cha familia bora. Ambayo kwa mtazamo wangu mimi, familia bora ni ile inayokula mkate wa kimwili na wa kiroho (neno) pia ni ile inayoshiriki katika kuwapa watu wengine mkate wa kimwili na wa kiroho. Kila kijana awe na ndoto (dream family) ya kuwa na familia ya namna hii: “Palikuwa na mtu Kaisaria, jina lake Kornelio, akida wa kikosi kilichoitwa Kiitalia, mtu mtauwa, mchaji wa Mungu, yeye na nyumba yake yote, naye alikuwa akiwapa watu sadaka nyingi, na kumwomba Mungu daima.” Matendo ya Mitume 10:1-2
Si Kornelio peke yake, bali hata watoto na mke wake walikuwa watoaji, watauwa na wachaji wa Mungu, ndio maana ikaandikwa yeye na nyumba yake yote. Huyu mtu na familia yake wanafaa kuigwa. Maandiko yamemweka makusudi ili tujifunze kitu.
Hakuna familia ambayo yenyewe peke yake imekamilika. Usiwaze kuishi kwa mfumo wa kujifungia na familia yako (closed system). Mungu anajua baba na mama hawatoshi, ndio maana akaleta kitu kinachoitwa kanisa. Lengo ni kwamba, yale mazuri yasiyopatikana nyumbani basi yakapatikana katika mwili wa Kristo yaani kanisani. Katika kanisa kuna mitume, manabii, walimu, wachungaji na wainjilisti. Usipange kukosa hekima zao. Wako ili kuwakamilisha watakatifu.
Mtandao umefanya kanisa kwa maana ya mwili wa Kristo kuwa pana zaidi. Vitabu na majarida vinarahisisha mawasiliano katika mwili wa Kristo. Leo hii unawaza ukawa na baba au kaka wa kiroho ambaye hamjawahi kuonana naye ana kwa ana. Mwili wa Kristo ni mpana, hakuna sababu ya kumchukia mtu wa kanisa lingine au wa dhehebu lingine sote tuko pamoja katika mwili mmoja.
Jaribu kufikiri ni mangapi ungekosa kama ungejifunza katika familia yako tu? Je, ni mangapi mazuri ungeyakosa kama ungejifungia kanisani kwenu tu? Leo ninakuletea familia ya Kornelio na naomba ujifunze toka kwao. Kwa Yule rafiki ambaye hajaolewa basi unanafasi bado, jipange na fikiria kuwa na familia nzuri kama ya kornelio. Familia ya sala siku zote, maombi siku zote, sadaka siku zote.
Wiki ijayo nitaendelea kuzungumzia mambo ya kuzingatia katika hutua za awali kuelekea kuoa au kuolewa.  Maisha ya Kornelio ni alama (legacy) na wewe unayo nafasi ya kuacha alama anza sasa kunuia kuacha alama katika familia na jamii yako.




0 comments :

Kata kiu yako

10:57:00 AM Unknown 0 Comments

 
KATA KIU YAKO
(Hakuna mbadala wa Mungu)
Mwanzoni nilizani ni gari, baadaye nilidhani ni kazi nzuri, mwishowe nilifikiri ni katika kuoa na kuolewa; kumbe ni uweponi mwa Mungu pekee ndimo ulimo utoshelevu wangu. Mtakatifu Agustino anasema, “Moyo wa mwanadamu hauta tulia mpaka umekutana na muumba wake”.  Ambao hawajaoa hudhani wakioa mioyo yao itatulia, wasio na kazi hufikiri kazi inatoa kitulizo na wasio na pesa nao hutamani kutulizwa kwa kupata pesa.
Nyakati za Ibrahimu, Nuhu, na waamuzi hakukuwa na mabasi ya mwendo kasi,wala hapakuwa na  ipad na kompyuta. Lakini bado watu hawa walikuwa na utoshelevu na amani ya ajabu. Je, amani hiyo waliipata wapi? Watu hawa hawakuwa na lift kwenye majengo yao, wengine hawakuwa hata na nyumba bali waliishi hemani. Lakini sasa licha ya kuwepo kwa mambo mengi mazuri bado wengi wana hali mbaya kuliko zamani, ni wenye uhitaji usiokwisha. Hakuna utoshelevu katika vitu. Paulo ananukuu fikra za Musa kwamba, hata upewe milki zote za Misri bado hautapata utoshelevu. Wakati huo Misri ilikuwa ni tajiri mno na kitovu cha uchumi wa nchi nyingi, pamoja na hayo Musa alijua hakuna utoshelevu ndani yake. [Ebr11:26]
Kuna nyakati nimekuwa na rafiki mzuri anayenipenda sana kila kitu kinakuwa murua kabisa [double double] lakini bado nafsi yangu ililia kwamba, inamtaka Mungu. Hakika, moyo wangu hautatulia popote ila kwa BWANA naam, BWANA peke yake.
Hata umpate mtu atakaye kupenda sana bado moyo wako hautatulia, nafsi yako italilia uwepo wa Mungu. Ayala ambaye ni ndege wa jangwani [kusiko na maji na unyevu] huvitamani sana vijito vya maji vivyo hivyo moyo wa mwanadamu hautanyamaza hata ukipewa vilivyo vinono utaendelea kumhitaji Mungu. Kukosekana kwa Mungu kutakuwa ni kama ukame ndani ya nafsi ya mtu.
Katika kisima cha Yakobo Yesu alikutana na mwanamke Msamaria,aliyekuwa ameolewa na wanaume wa tano na aliyekuwa naye ni wa sita. Lakini Je, alikuwa anatafuta nini kwa waume hao wote sita? Jibu ni rahisi alikuwa anatafuta utoshelevu yaani, alitaka kukata kiu yake.  Yesu akamwambia maji haya unayochota hayakati kiu. Pesa, sigara, wanaume, uasherati, hamu ya kuona picha chafu, wanawake, urembo, utanashati, vyeo na mali za thamani kamwe havitaweza kukata kiu yako.
Mwanamke Msamaria alisimama katika kisima cha Yakobo, lakini Yesu pia alisimama kama kisima. Kwa hiyo kuna kisima cha Yakobo na Kisima kingine ni Yesu Kristo. Ndani ya kisima cha Yakobo mlitoka maji yasiyo kata kiu, ndani ya Yesu Kristo mlitoka maji yakatayo kiu. Na Yesu anamwalika kila mtu aje anywe maji hayo ya uzima na asione kiu tena.
Baada ya Yesu kuzungumza na yule mwanamke mwishowe alikubali na akataka apewa kile kinacholeta utoshelevu kile kinachoondoa kiu yaani, Roho Mtakatifu ambaye ndiye maji yaletayo utoshelevu na kuridhika. Natamani sote tumkimbilie Yesu na kumsihi kwa maneno ya maombi kama alivyofanya mwanamke Msamaria: “Yule mwanamke akamwambia, Bwana, unipe maji hayo, nisione kiu, wala nisije hapa kuteka. ”Yohana 4:15
Samaki huwa katika ubora wake na ufanisi wa juu akiwa majini, mashine huwa katika ufanisi wa juu inapokuwa mpya tena inapowekewa vilainishi [oil] kwa wakati. Vivyo hivyo binadamu huonesha ufanisi wa hali ya juu awepo uweponi mwa Bwana ambamo kuna ushirika wa ajabu na Roho Mtakatifu.
Tafuta kukata kiu yako leo….tukutane chumba cha juu kama wale mia ishirini [120]

0 comments :

Anuani ya Muda

12:00:00 PM Unknown 0 Comments

 
ANUANI YA MUDA
(P.O. BOX 701, MBEYA)
Yesu aliposali alisema, “Baba yetu uliye mbinguni” hiyo ni anuani ambayo kila mmoja wetu anapaswa kuitamani baada ya maisha haya. Ni muhimu mara baada ya kifo tupatikane kwa anuani hiyo ya Mbinguni. Lakini kwa kuwa bado tuko duniani tunajulikana kwa anuani za makampuni, anuani binafsi, shule na taasisi ambazo tunaishi na kufanya kazi ndani yake. Na baadhi labda tuko vijiweni na pengine hatupatikani kabisa [Unreachable].
Inawezekana uko kwenye taasisi ambayo kwa namna moja au nyingine inakupa mateso, Inawezekana uko katika mazingira ambayo kwa namna moja au nyingine hayakupi furaha, jambo moja nataka ujue ni kwamba, uko hapo kwa kitambo tu. Kitambulisho ulichopewa na taasisi yako, anuani unayojulikana kwayo sasa ni ya muda tu, kamwe haita dumu milele. Zamani Nelson Mandela alipatikana kwa anuani ya gereza, waliomtembelea walilazimika kwenda huko; Yusufu pia alipatikana gerezani na mwishowe ikulu. Leo hii wote [Yusufu na Mandela] wanajulikana katika hadithi za kutoka jela mpaka ikulu.  From prison to palace story.
Maisha ya shule au chuo yanaweza kuwa magumu hata mtu akakata tamaa na kuzimia moyo, lakini maisha hayo ni ya kitambo kifupi tu, punde si punde utamaliza na maisha mapya yataanza. Nakumbuka anuani ya, P.O BOX  701, Mbeya ilikuwa anuani yangu ya shule ya Sekondari. Maisha ya shule pale hayakuwa mazuri, kidato cha kwanza wengi walikuwa wanapigwa na kuonenewa bila sababu. Lakini nilijipa moyo na nikamwomba Bwana anilinde ili nitoke salama katika taasisi ile. Niliomba sawa sawa na imani yangu kwa wakati ule, na kweli nilitoka salama. Ilikuwa anuani ya muda tu.
Sijui kwa sasa wewe uko wapi na una amani kiasi gani, lakini ninachojua ni kwamba unapita katika eneo hilo na hutokaa milele katika mateso hayo. Wakati mwingine ni vema kuomba Mungu akupe uvumilivu na namna ya kuishi katika mazingira fulani ili uishi vizuri katika kipindi cha mpito.
Inawezekana Bosi wako ni mkali, inawezekana pia wafanyakazi wenzako hawakutendei vizuri, jipe moyo kwa maana, wewe na wenzako hamta dumu katika taasisi hiyo milele. Cha msingi ni hekima itumike  ili muachane kwa usalama muda ukifika. Biblia inasema katika mambo yote tujipatie sifa njema, kwa hiyo hata katika maeneo yetu ya kazi, biashara na huduma ni lazima tujipatie sifa njema.
Na ili tuishi na watu hatuhitaji watu wabadilike bali tunahitaji kubadilika. Usimsubiri mkali awe mpole, bali wewe uwe mpole, usimsubiri mkorofi awe mtaratibu bali wewe uwe mtaratibu. Kwa hiyo haijalishi uko katika taasisi yenye changamoto namna gani lazima ujue uko hapo kwa muda tu, fanya vizuri na nuia kuacha alama mahali hapo. Upo hapo kwa kitambo tu. Anuani yao si kitambulisho chako cha milele.
Inawezekana sasa unatumia sanduku la posta la kijiji chako lakini ni nani ajuaye kwamba, mwishowe watu watumia anuani ya Ikulu kukupata?  Inawezekana sasa unajulikana kwa anuani ya kampuni ya mhindi lakini ni nani ajuaye kwamba, mwisho wa siku utajulikana kwa anuani ya kampuni yako binafsi? Inawezekana kabisa, pango mipango na kisha anza kuyaendea mafanikio yako.
Nataka nikutie moyo mpendwa, uko hapo  kwa muda tu, siku si nyingi utajulikana kwa jina jema na kwa anuani bora zaidi. Uko hapo ili kujifunza, kama haupati pesa za kutosha usijali, jitahidi upate uzoefu wa kutosha. Tunapofanya kazi tunafanya kwa ajili ya mambo matatu, ama kwa ajili ya Mungu, ama kwa ajili ya pesa, au kwa ajili ya uzoefu. Leo nasisitiza pata uzoefu wa kutosha na pesa zitakuja baadaye, uzoefu unavuta pesa. Uzoefu wa kazi ni pamoja na kujua tabia mbaya za wateja na wafanyakazi wenzako na namna ya kuzikabili changamoto za kitabia.
Daudi na Esta ni watu ambao kwa imani, na kwa ustadi wao walijikuta anuani zao zinabadilika. Walipatikana katika nyumba ya Mfalme ilhali hawakuzaliwa kwa mfalme. Na ndivyo ilivyo hadithi yako usipokata tamaa. Mungu anaweza kukutoa jaani na akakuketisha na wakuu. Endelea mbele. Mpaka wiki ijayo, tukutane katika nyumba ya mfalme, shalom!!!

0 comments :

Yesu Kazini

11:56:00 AM Unknown 0 Comments

YESU KAZINI
(Jesus in Action)
Miungu ya watu wengine ina miguu lakini haiendi, inamacho wala haioni, inamikono wala haishiki. Miungu hiyo [sanamu] imeumbwa na wale wanaoiabudu [wametengeza mungu wao]. Miungu hiyo ni pesa! Wako wanaozitumikia na kuziabudu. Miungu hiyo ni ng’ombe, tamaduni, mila au desturi zinazopingana na Mungu wa kweli. Miungu hiyo ni kitu chochote cha kufinyangwa, kuchongwa au kutengenezwa kinachochukua nafasi ya Mungu. Chochote kinachochukua nafasi ya Mungu katika moyo wa mwandamu ni sanamu.
Tukitegemea uwezo wetu kuliko Mungu uwezo huo unageuka sanamu. Tukitegemea uzoefu kuliko Mungu uzoefu huo unageuka sanamu. Tunapomfanya Mungu kuwa wa pili tunaingia katika mtego wa kuabudu sanamu. Tunaposema tujenge nyumba zetu kwanza ndipo tujenge nyumba ya Mungu tunaingia mtegoni kama watu wa nyakati za Hagai. God second! Selfish Priority.
Katika hekalu kulikuwapo na patakatifu pa patakatifu ambako kulikuwepo na kiti cha rehema mahali alipoketi Mungu wa rehema. Miili yetu pia ni mahekalu, iko sehemu ambayo ni maalamu kwa ajili ya Mungu wetu. Kama ilivyokuwa katika kiti cha rehema, leo Mungu anakaa katika mioyo yetu na hapo amestahili yeye tu, kutukuzwa na kuabudiwa. Mungu ni wa kwanza katika moyo wa mwandamu. Akikaa mwingine hapo huitwa sanamu, na akitambulika na kuheshimiwa huitwa ibada ya sanamu.
Yohana mbatizaji alitaka kujua kwamba, Yesu ndiye Kristo au vinginevyo. Yesu akitaka kumdhihirishia Yohana kuwa Kristo ni matendo alimjibu, “Vipofu wanapata kuona, viwete wanatembea, wenye ukoma wanatakasika, viziwi wanasikia, wafu wanafufuliwa na maskini wanahubiriwa habari njema” Kwa lugha nyingine ukisikia matendo haya ujue Yesu Kristo yuko kazini. Matendo haya yalitosha kumpa picha Yohana.
Mungu wetu anaonekana katika matendo mema, Mungu wetu anatembea katika maisha ya watu wake. Mungu wetu anawagusa vipofu, viwete, wenye ukoma [wenye dhambi], viziwi hata masikini pia. Tofauti na sanamu hazimgusi mtu, ni kazi ya mikono ya watu wala haziwezi kumstawisha mtu yeyote. Zinamikono wala hazishiki, zinamiguu wala hazitembei labda waliozifanya wazitembeze.
Tunaposikia uzima, amani, mafanikio na ustawi wa jamii zetu bila shaka tunatambua Yesu Kristo yuko kazini. Yesu ni matendo, Yesu ni upendo tena Yesu ni miujiza. “Nao walipofika kwake, walisema, Yohana Mbatizaji ametutuma kwako, akisema, Wewe ndiwe yule ajaye, au tumtazamie mwingine? Na saa ile ile aliwaponya wengi magonjwa yao, na misiba, na pepo wabaya; na vipofu wengi aliwakirimia kuona.  Ndipo alipojibu, akawaambia, Nendeni mkamweleze Yohana hayo mliyoyaona na kuyasikia; vipofu wanapata kuona, viwete wanatembea, wenye ukoma wanatakasika, viziwi wanasikia, wafu wanafufuliwa, maskini wanahubiriwa habari njema. Naye heri mtu ye yote asiyechukizwa nami. ” Luka 7:20-23
Wasiochukizwa na Yesu Kristo waseme na wabarikiwe. Mpaka wiki ijayo, amani iwe nawe.

0 comments :