ULIMWENGU MKAMILIFU

11:24:00 AM Unknown 0 Comments


ULIMWENGU MKAMILIFU
“Imagine a world without a loser, a world without a purposeless person”
Dunia kamilifu inategemea sana ukamilifu wa mwanadamu. Kwa asili mwanadamu ni mkamilifu na mwenyehaki. Hebu jaribu kufikiri kwamba ulimwengu ungekuwa mkamilifu ungependeza namna gani; hata hivyo ukamilifu wake unategemea wanadamu. “Basi ninyi mtakuwa wakamilifu, kama Baba yenu wa mbinguni alivyo mkamilifu.”Mathayo 5:48

Katika ulimwengu mkamilifu hakuna askari polisi wala askari magereza, katika ulimwengu mkamilifu hakuna chuki wala mapigano watu hukaa kwa amani. Amani yao huja kwa sababu kila mtu anafanya anachopenda na alichotumwa na Mungu kukifanya hapa duniani. Kama Yohana mbatizaji alivyotoka kwa Mungu na kuja duniani, ndivyo kila mmoja wetu pia alivyotoka mbinguni ili kuja kutekeleza wajibu wake hapa duniani. Palitokea mtu, ametumwa kutoka kwa Mungu, jina lake Yohana. Huyo alikuja kwa ushuhuda, ili aishuhudie ile nuru, wote wapate kuamini kwa yeye.”Yohana 1:6-7
“Tukiwa na watu wakamilifu yaani, watendao kwa ukamilifu tunaweza kuwa na ulimwengu mkamilifu ”
Kwa kupitia msalaba wa Yesu Kristo ukamilifu umewezekana. Lengo la Mungu ni sisi sote turejee Mwanzo sura ya kwanza ambapo mwanadamu ameonekana katika ukamilifu wake. Ni muhimu kuwa na picha ya ulimwengu wa watu wakamilifu hata kama ulimwengu huo utahusisha watu watatu tu. Mungu ametuumba wanadamu tukiwa wakamilifu, ni katika mwanzo sura ya tatu ndipo Adamu na Eva walipopoteza ukamilifu wao. Ni wakati huo ndipo Chuki, usaliti, uchoyo na mauti vilipata nafasi katika maisha ya mwanadamu na ukamilifu ukapotea. Kwa upendo Mungu aliendelea kumtafuta mwanadamu tena ili kumrejesha katika ukamilifu aliokuwa nao mwanzoni.
Tukiwa na watu wakamilifu yaani, watendao kwa ukamilifu tunaweza kuwa na ulimwengu mkamilifu. Ni rahisi mtu kutenda kwa ukamilifu na kwa upendo ikiwa tu mtu atafanya anachopenda kufanya. Kama kila mtu atafanya kazi aipendayo (aliyoitwa na Mungu kuifanya), tena kama kila mmoja wetu atamruhusu Mungu atende ndani yake basi tutashuhudia ulimwengu mkamilifu. Mwanadamu huweza hutenda kwa ukamilifu kwa sababu ni Mungu ambaye hutenda ndani yake.
“Ukijenge maisha yako katika eneo ambalo Mungu atatenda kazi ndani yako basi utakuwa mtu mkamilifu”
Basi, Mungu wa amani aliyemleta tena kutoka kwa wafu Mchungaji Mkuu wa kondoo, kwa damu ya agano la milele, yeye Bwana wetu Yesu, awafanye ninyi kuwa wakamilifu katika kila tendo jema, mpate kuyafanya mapenzi yake, naye akifanya ndani yetu lipendezalo mbele zake, kwa Yesu Kristo; utukufu una yeye milele na milele. Amina.” Waebrania 13:20-21
Ukijenge maisha yako katika eneo ambalo Mungu atatenda kazi ndani yako basi utakuwa mtu mkamilifu. Inawezekana ni katika kuwalisha masikini, huenda ni katika siasa, au katika kufundisha, lakini liko eneo ambalo Mungu atatenda pamoja nawe. Na huenda hata sasa anatenda kazi pamoja nawe pasipo wewe kujua. Uzuri wa kusudi ni kwamba si wewe utendaye, bali ni Mungu ndani yako. Kwa maana ndiye Mungu atendaye kazi ndani yenu, kutaka kwenu na kutenda kwenu, kwa kulitimiza kusudi lake jema.”Filipi 2:13
Palipo na furaha ya kweli pana ukamilifu wote, ndio maana imenenwa “furahini katika BWANA.” Kuna furaha ya ajabu katika kutii mapenzi ya Mungu, kila mtoto wa Mungu mtiifu anajua jambo hili.  Lazima ujiulize ni wakati gani katika kutenda kwako umekuwa mwenye furaha sana. Ukipata jawabu basi jenga maisha yako kuzunguka jambo hilo. Binafsi napenda kuhubiri habari za Mungu na ninakaza mwendo ili kujenga maisha yangu katika jambo hili moja; napenda mtu wa jambo moja.
Ukamilifu huenda pamoja na uaminifu. Hizi mbili hazitofautiani kamwe. Hakuna mtu mkamilifu asiye mwaminifu. Nimewahi kumtazama mwezeshaji mmoja akiwahoji watu kuhusu uaminifu wao katika saa za kazi. Aliwauliza, “Katika saa kumi na mbili za kazi ni saa ngapi wanakuwepo ofisini kimwili, kiakili na kimawazo?” Aliyesema saa nyingi ni tatu yaani katika saa 12 ni kwa muda wa saa tatu tu ndio akili yake huwa pale kwa asilimia 100%. Wengine walisema saa moja kati ya 12 na wengine saa mbili kati ya 12. Hakuna ambaye anakuwepo pale kiakili kwa muda wote wa saa 12, lakini kimwili wanakuwepo. Huu pia si uaminifu. Hii ni shida itokanayo na kufanya kazi usiyoipenda.
Ukamilifu unachagizwa sana na mwanadamu ambaye anafanya apendacho alichoumbwa kukifanya. Unamkumbuka Yona aliyekuwa na mawazo ya Ninawi ilhali anaelekea Tarshishi ili kujiepusha na uso wa Mungu. Wako maaskari ambao wameshika bunduki badala ya Biblia Takatifu, wanaenda lindo ilhali walipaswa kwenda katika mkesha. Wanafanya wasichokipenda na hivyo hawapati furaha ya kweli. Wako vijana wanaoishi nje ya kusudi la kuumbwa kwao, wako wahandisi hata waashi ambao wamepishana na wito wao.
Ni muhimu kila mtu ajue alichoitiwa, akipokee na kukiheshimu. Ni lazima kila mtu atambue upekee wake katika sayari hii. Ni sayari ambayo kila mtu ni halisi wala si nakala ya mwingine. Dunia yetu ingekuwa nzuri mno kama kila mtu angekitumia kipawa au kipaji chake kwa upendo. Kila mtu angefanya kazi kwa utulivu na amani angestawi.
Hakuna amani katika nchi ya watu wasiotimiza waliyoitiwa na Mungu. Ni hatari kukaa na mtu asiyeenda katika kazi aliyoagizwa na Mungu. Watu waliosafiri na Yona walitaka kufa kwa sababu Yona alikataa kwenda katika maagizo ya Mungu. Watu waliosafiri na Paulo waliokoka kwa sababu Paulo amekwenda katika maagizo ya Mungu.
Kama hatuendi katika makusudi ya kuumbwa kwetu basi kufa kabla ya wakati “pre mature death” si ajali. Hatua muhimu katika kuibadili hatima yako ni kubadilisha kwanza mwelekeo wako. Yona alibadilisha mwelekeo wake kwa kutubu akiwa ndani ya tumbo la samaki na baadaye akaenda Ninawi kama alivyoagizwa.
Inawezekana haukitendei haki kipaji chako, hauishi kusudi la Mungu wala haunendi kwa kadiri ya wito wako ni muda mzuri leo wa kufanya mabadiliko. Chukua uamuzi anza kuishi sawasawa na kusudi la Mungu katika maisha yako leo. Ama uteseke kwa kuanza upya, au ufe katika eneo ambalo Mungu hakutaka kabisa udumu hapo. Nje ya wito hakuna ukamilifu, ni sawasawa na samaki nje ya maji.
“Mtu anayefikiri kuhusu sababu, kwanini hawezi kufikia malengo makuu katika maisha yake, hutumia nguvu ile ile katika kufikiri, sawa na mtu anayefikiri kuhusu namna [njia] ya kufikia malengo hayo; yamkini huyu wa pili hutumia nguvu kidogo”
Kila mtu huwa na sababu nyingi sana za kumzuia kwenda katika kusudi la Mungu. Uchungu wa kutokwenda ni majuto na maisha ya yasiyo na furaha ya kweli, uchungu wa kwenda ni changamoto. Kila mtu anayo sababu yake inayomdanganya ili asifikie malengo makuu, mwingine  atasema umasikini, mwingine ugonjwa, mwingine ulemavu, mwingine familia aliyotokea, mwingine elimu ndogo.
Kumbuka, Sababu 1000 za kutokwenda au kutokufanya kusudi la Mungu hazina mashiko ukilinganisha na ile moja itokayo kwa Mungu inayokuhimiza kuyatendea kazi makusudi ya kuumbwa kwako. Mtu anayefikiri kuhusu sababu, kwanini hawezi kufikia malengo makuu katika maisha yake, hutumia nguvu ile ile katika kufikiri, sawa na mtu anayefikiri kuhusu namna [njia] ya kufikia malengo hayo; yamkini huyu wa pili hutumia nguvu kidogo.
“If you really want to do something you’ll find a way. If you don’t. You’ll find an excuse” Jim Rohn

0 comments :