WEWE NDANI YA KUSUDI LA MUNGU

8:12:00 PM Unknown 0 Comments

 
WEWE NDANI YA KUSUDI LA MUNGU
(Samaki ndani ya maji, wewe ndani ya kusudi la Mungu)

Hapo mwanzo kila alichokiumba Mungu aliona kuwa ni chema ‘good’; alionesha kuridhishwa na hali yake. Mungu huvipenda vitu vyote alivyoviumba. Mungu hupenda watu tofauti tofauti, wenye vionjo na tabia tofauti tofauti. He is God of Varieties! Alimpenda Musa mpole, lakini alimtaka Haruni ambaye ni msemaji (mwongeaji) amsaidie Musa. Mungu anakusudi jema na watu wa haiba zote, kasumba mbali mbali au silika yoyote ile. [Mwanzo 1:31]
Kama aliyekuumba amesema wewe ni mwema ‘good’ maana yake uko tayari kwa kazi fulani. Alipoitazama ile kazi na alipokutazama wewe akasema vema, maana yake ameonesha kuridhishwa na uhusiano uliopo baina yako wewe na kusudi uliloitiwa.
Ukiona uko katika eneo ambalo linakuhitaji ujifanyie marekebisho makubwa sana (massive change) ili uwepo wako ufae katika eneo hilo, lazima ujiulize mara mbili; inawezekana si eneo lako.  Ukiona uko na mtu anayetaka ubadilike sana ili umfae yeye, ujiulize mara mbili pia; yawezekana si wa shirika lako. Kusudi la kuumbwa kwako ndiyo bahari pekee unayoweza kuogelea kwa urahisi.  Samaki hafanyi marekebisho yoyote ili afae kukaa majini, wala tai hafanyi marekebisho ili kuruka, anafanana na kusudi lake. Sihitaji kuwa mtu fulani ili niwe mimi.
Tunapoteza muda mwingi tukisubiri kubadilika, ati! ndio tuanze. Ukweli ni huu: “Agent of change never change” yaani, wakala wa mabadiliko habadiliki. Kama umezaliwa kubadilisha ulimwengu maana yake wewe umeshabadilika tangu hujaja duniani. Kama umezaliwa kuwatoa watu utumwani maana yake wewe si mtumwa. Musa hakuwahi kuwa mtumwa japo alikuwapo Misri. Yesu hakuwahi kutenda dhambi japo aliishi duniani. Kama umezaliwa ili kufa, maana yake umeshakufa hata kabla hujazaliwa (mkumbuke Yesu). ...Mwana-Kondoo, aliyechinjwa tangu kuwekwa misingi ya dunia” Ufunuo 13:8
Mungu haleti wanafunzi wa kada fulani hapa duniani, Yeye hushusha watendaji ambao tayari ni imara kabisa.  Huleta askari walio tayari kwa vita na si kwa mafunzo. Ukizaliwa tu, ujue umeshatumwa; si lazima ukae na Yesu miaka mitatu kama mitume; ni hasara kuwa mwanafunzi asiyehitimu. Habari yako ni ya tofauti, umezaliwa ukiwa tayari. Bwana akawatuma (wakazaliwa) Yerubaali, na Baraka, na Yeftha, na Samweli, akawaokoa ninyi na mikono ya adui zenu pande zote, nanyi mkakaa salama.” 1 Samweli 12:11 [Maneno ya kwenye mabano ni msisitizo wa mwandishi].
Shida zako zinakusaidia kujua jambo moja kubwa kwamba, “wewe ni mkimbizi.”  You’re not where you belong! Bora uwe mkimbizi katika nchi jirani kuliko kuwa mkimbizi katika kusudi la Mungu. Unafanya vizuri kazi isiyokupasa kufanya, unakula usichopaswa kula, na una marafiki usiopaswa kuwa nao. Hii ilimpata mwana mpotevu; alikula na nguruwe, badala ya kula na Mungu, si unajua ukifungua moyo Yesu atashinda kwako na kula pamoja na wewe. Usipofungua mlango ndio habari ya kula na nguruwe inakuja. {Ufunuo 2:20}
Mwana mpotevu alipogundua ukweli kwamba, anatawaliwa na mazingira badala ya yeye kuyatawala aliamua kuondoka. Kusudi ndilo linakupa uwezo wa kuyatawala mazingira badala ya mazingira kukutawala wewe. Tukimtosa mtu baharini bila ya kumwokoa au kumpa vifaa vya kumsaidia, bila shaka baada ya kitambo atakufa. Si kifo cha bahati mbaya, mazingira (maji) yamemtawala. Mungu alitaka tuyatawale mazingira yetu kupitia kuishi  kusudi, kila yanapotutawala yanaashiria kifo.
Baba anaweza kukukataa, hata mama anaweza pia. Ni sehemu moja tu unayoweza kupokelewa bila ya kuambiwa ondoa hiki na kile kwanza, nayo ni katika kusudi lako. Your purpose will adopt you as a lovely son/daughter
Kama nimezaliwa kucheza mpira si lazima nicheze kwenye kiwanja cha mtu asiyenitaka, pia si lazima nicheze katika timu isiyonikubali. Ndio maana kuna viwanja vingi na timu nyingi. Kamwe usibadili uamuzi wako wa kucheza mpira bali badilisha timu na viwanja.  Nimewahi soma nukuu hii: “Change direction but don’t change your decision.”
Ni sehemu moja tu ambapo hisia zako zote hupokelewa, ni mahali pale tu ndipo kimo chako huleta maana, ni katika kusudi uliloitiwa na Mungu ndipo haiba yako; utanashati wako, kujisahau kwako, ukimya wako, mihemko yako, haraka zako, udadisi wako, ujasiri wako, hekima yako na upole wako hupokelewa kwa moyo wote. Ni katika kusudi la Mungu ndipo Musa mpole na Haruni msemaji wote huwa na  maana. {Kutoka 4:14}
Sijui unapata taswira gani unapomuona kaka mtanashati, sijajua unawaza nini unapomuona dada mrembo, binafsi ninajua jambo moja, “mwili ni kwa BWANA.” Kama alivyoagiza Yesu mitume wamfungue yule punda na atakayeuliza ajibiwe hivi: “BWANA anahaja naye.” Ndivyo ilivyo kwako, BWANA anahaja nawe na namna ulivyo. ... Lakini mwili si kwa zinaa, bali ni kwa Bwana, naye Bwana ni kwa mwili.” 1Wakorintho 6:13
Mungu ni Roho, roho haili nyama ya mtu wala ya punda. Ukisikia maandiko yanasema BWANA anahaja nawe ujue kinachotajwa hapo ni utumishi au kusudi la kuumbwa kwako wala si ,’lunch’. Biblia inasema “mwili si kwa zinaa bali ni kwa ajili ya BWANA.” Mwili wako unaakisi kusudi lako. UKiliendea kusudi lako litakupokea bila ya kukuambia jikarabati kwanza. Kwani  tayari unafanana na kusudi lako, hakuna haja ya ukarabati.
Biblia inatafsiri, mwili ni nyumba ya roho. Si kila nyumba ni kwa ajili ya kulala, nyingine ni ofisi. Nadhani kwa mtazamo wa biblia, mwili ni ofisi. Ofisi huakisi kazi za taasisi husika. Kwa mamantilie jiko ni ofisi, kwa fundi makenika Gereji ni ofisi. Jiulize nini kinafanyika katika mwili wako kama ofisi.  Muonekana mzuri na tabasamu bashasha usio sadifu matendo unatupa nafasi ya kujua kwamba hauishi kusudi lako. Kaka mzuri unavuta sigara, balaa gani kama hii! Dada mzuri lakini kahaba, ni msiba gani kama huu! Jengo linaashiria kusudi jema lakini kinachotendeka ndani ya ofisi (mwili) ni ubatili.
Hadi biblia ikasema, “mwili si kwa ajili ya zinaa” maana yake watu hudhani mwili ni kwa ajili ya zinaa. Mtazamo huo mbovu umepelekea kusudi la Mungu kusahaulika.Tujifunze kwa Yesu, alipata mwili ili autumie katika mateso na kuleta ukombozi. Alikuwa na sababu za kiofisi za kuvaa mwili. Bila mdomo asingelikunywa siki, bila mabega asingelibeba msalaba.  Mwili ni kwa ajili ya utimilifu wa kusudi. Mwili wake ulikuwa ofisi ya kutimizia kusudi. Alionekana kama kusudi lake, wewe pia umefanana na kazi fulani au wito fulani na Mungu amekushakupa ofisi yaani, mwili.
Kama una mwili lazima ujue lipo kusudi kwa ajili yako. Unamsubiri Mungu? Alishasema imekwisha, tena akasema kila alichokiumba ni chema; Anakusubiri wewe. Badilisha mtazamo wako, anza hiyo safari, anza sasa hiyo biashara, ondoka huo mkoa uende anapokupeleka Mungu. Labda ulikimbia shule rudi masomoni, anza kulifanyia kazi hilo wazo, chukua fomu na ugombanie hiyo nafasi, anza kuamka mapema, anza kuishi hilo kusudi, anza kuwasaidia yatima, labada ni mhudumu anza sasa kuhudumu, tekeleza azma ya moyo wako na kuyatawala mazingira yako. Badala ya kuishia kujivika nguo nzuri (pamba kali) za kisasa wewe tinga kusudi la Mungu na kisha utoke, wakati ni sasa! Ogelea.

0 comments :