Biblia ina majibu yote

BIBLIA INAMAJIBU YOTE
ISOME!
Ni mwaka mpya sasa nuia idadi ya vitabu unavyopaswa kusoma mwaka 2018, zaidi ya yote usisahau mpango wa kusoma Biblia, yearly bible reading plan! Tatizo la kutokusoma linaendelea kuwatesa watu wa leo, kizazi hiki hakijajijengea tabia ya kujisomea. Majibu mengi ya matatizo yetu yanayotukumba katika maisha ya kila siku yako katika vitabu, bahati mbaya hatusomi.
Hivi karibuni nikiwa naelekea Bagamoyo kwenye daladala nilifarijika baada ya mtoto wa miaka kumi kuingia ndani ya gari na kisha kutoa kitabu na baada ya mwendo kidogo akaanza kusoma. Nilitamani kupiga naye picha (selfie) kwa furaha, kuona utamaduni ninao upenda umejengeka kwa mtoto yule. Miji na majiji yenye foleni hutoa fursa kwa watu kujisomea wakiwa barabarani. Nyumbani utasema watoto wasumbufu barabarani je? Furaha tunayoikosa vijiweni iko kitabuni, nguvu tunayoikosa pahala pa kazi iko vitabuni, knowledge is power!! Mwenye maarifa mengi ni mwenye nguvu nyingi hili halipingiki. Kile ambacho baba yangu hakusema vitabu vimeniambia, kile ambacho dini ilinificha vitabu vimeniweka bayana. What a royal friend!
Nakushauri usome vitabu, lakini soma zaidi Biblia. Katika neno la Mungu kuna umilele wote. Yesu akasema, “ninyi mmekuwa safi kwa sababu ya lile neno mliliosikia”. Lile neno la Mungu unalosikia linafanya unakuwa safi mwili na roho.
Neno la Mungu limebeba majibu ya hali unazopitia wewe binafsi na Taifa lako pia. Unapotazama uchumi wako na hali ya taifa lako usiende tu kwa kutumia elimu ya uchumi ya darasani, ni muhimu utazame kiroho pia. Ukiona hali ngumu ya uchumi kwenye nchi jiulize Mungu anataka nini kwa taifa lako, inawezekana kabisa anataka toba. Badala ya kwenda kuchukua shahada ya uzamili ya uchumi mara nyingine ni muhimu kusoma Biblia mfululuzo. Daniel kwa kusoma maandiko (neno la Mungu) aligundua nini kinaendelea kwenye taifa lake.
Jifunze kujua chanzo, anayejua chanzo halalamiki sana. Taifa linapopewa mtawala mkorofi ni lazima ujue kuna mahali dhambi ilitendeka katika Taifa hilo na Mungu amemweka mtawala huyo kwa makusudi yake ili watu wake watubu na kurejea. Katika hali kama hiyo kufanya kazi kwa bidii hakutasaidia ila toba ya kweli kwa wateule wote wa Mungu walioko kwenye taifa hilo inaweza kuleta suluhisho.
Moja ya njia kuu ambayo Mungu amekuwa akiitumia kuzungumza na nchi na watu binafsi ni hali ya uchumi. Ukiaona kuna mvua ya kutosha, tena kwa wakati wake ni lazima ujue kuna kitu kizuri Mungu anazungumza, ukiona ukame na watu wanakufa kwa njaa ujue kuna kitu Mungu anadai au ibada ya sanamu imekithiri, ukiona watu wengi wanakimbia nchi ujue kuna laana ya ukiwa.
Katika kila jambo lihusulo hali ya hewa, mahali pa kuishi, hali ya uchumi ni muhimu utafute makusudi ya Mungu katika Biblia. Mambo haya yote ndani yake kuna makusudi ya Mungu, ukiyatafute ndani ya neno la Mungu utayajua! Jipatie ufahamu uyajue yanayokuhusu na yanayohusu nchi yako kwa kusoma maandiko. Barikiwa.

Bwana alipoamuru baraka

 
BWANA ALIPOAMURU BARAKA
MUDA MWAFAKA ENEO MWAFAKA. 
Katika mambo ambayo Mungu hata subiri ufanye maandalizi ni hukumu na fursa. Kila siku unapaswa kuwa tayari, katika eneo husika, mwenye maandalizi kamili, ndio maana ya lile neno kesheni. Si kila eneo, si kila Mkoa, si kila medani wala si kila nchi itakuwa na Baraka zako; liko eneo moja, iko aina ya biashara fulani, uko mkoa na pahala ambapo Mungu ameamuru baraka zako zipatikane. Wakati mwingine tunachagua miji kwa macho ya nyama na hivyo tunavyokwenda ndani yake hatufanikiwi sana. Si kila aliyeko Ulaya anamafanikio, kuna wengine wako huko na wanaomba chakula, hawana uhakika wa kupata milo mitatu.
Kuna watu ambao walikuwa jijini Dar es salaam ilhali baraka yao ilikuwa Dodoma. Kwa vyovyote vile haikuwa rahisi kuwapeleka watu hao Dodoma inawezekana walifikiri hakuna maisha bora nje ya jiji la Dar es salaam. Lakini Mungu kwa kutumia Tangazo la Serikali la kuhamia Dodoma amewawezesha pia maelfu ya watanzania kwenda kwenye baraka yao iliyoamriwa mjini Dodoma. Tangu nyakati za Yesu Kristo mpaka sasa matangazo mengi ya Serikali yamekuwa yakibeba makusudi ya Mungu ya amani. Amani maana yake uchumi mzuri, Baraka na mafanikio. Yanaweza matangazo hayo yakaonekana magumu na mabaya yenye kubeba usumbufu lakini baadaye Mungu hujitwalia utukufu na watu wake hustawi.
Ukihamishwa kwa Tangazo la Serikali usigome, Matangazo hayo hubeba baraka.  Katika saa yako ya kusimama kiuchumi na kiutumishi tangazo hilo halitaweza kukudhuru hata kama lilitolewa ili kukuangamiza wewe. Tangazo la Herode la kuua watoto wote chini ya miaka miwili halikuweza kumua Yesu maana ilikuwa ni wakati wa Yesu kung’aa na kuokoa, halikuweza kumzuia.
Si miji peke yake, hata changamoto nyingine za maisha zenye ukakasi  ndani yake kuna baraka pia. Wako watu ambao bila talaka wasingelipata wokovu, bila kuachwa wasingelijua kusimama wenyewe, wako wale ambao bila kufeli masomo wasingeli jaribu biashara ambazo leo zimewapandisha na kuwafanya wakuu.
Baraka hizo zisingepatikana ikiwa kila kitu kingekuwa shwari, mara nyingi inapokuwa ni shwari watu hujisahau sana na kufanya yasiyo ya msingi. Biblia inasema, “Katika shida yangu nalimwona BWANA”.  Kuna nyakati ambapo ni kupitia shida na usumbufu tunaweza kumwona Mungu. Ni methali ya zamani ya wazungu, “Bahari shwari haitoi wanamaji hodari” ni kweli baharia hodari ni lazima atakuwa na uzoefu wa kutatua shida za majini.
Usiogope sura ya mji, usiogope ukubwa wa changamoto inayokukabiri; cha msingi hakikisha uko mahali sahihi ukisubiri wakati sahihi wa kuinuliwa kwako. Mahali ambapo Mungu ameamuru baraka pana changamoto lakini pia pana baraka nyingi. Kuwa mahali pa baraka haina maana hapatakuwa na changamoto kabisa! Mara nyingi ustawi wako katika eneo hilo utategemea pia namna unavyomkumbuka Mungu, kumkumbuka maana yake kushika amri zake na kumshuhudia kwamba ni yeye ni Mungu aliyekufikisha hapo Sayuni yako.
Barikiwa na Endelea mbele…

Mwaka 2018 Uwe Mwaka wa Kujihatarisha.......

 
MWAKA 2018 UWE MWAKA WA KUJIHATARISHA ZAIDI ILI KUPATA MAFANIKIO
Wengi wanashindwa kwa sababu hawafanyi kitu mpaka waone ni salama kabisa, hawaanzi mradi mpaka waone ni faida tupu, tabia hii imezuia mafanikio ya wengi. Mwaka jana niliingia kwenye biashara ya mtandaoni (online business) na kupata hasara ya milioni nne, mwaka huo huo bila ya kukata tamaa nikaingia katika biashara nyingine na kupata faida ya milioni nne! Ukipata hasara katika biashara moja haina maana kwamba na biashara nyingine utapata hasara pia.
Kitabu cha Mhubiri kinasema, “Mwenye kuuangalia upepo hatapanda; Naye ayatazamaye mawingu hatavuna” Mhubiri 11:4. Ukichunguza chunguza sana huji kufanikiwa katika uwekezaji na maendeleo. Kuna wakulima ambao wakijua ni msimu wa kilimo wanalima na hawa ndio hufanikiwa. Na kuna wale ambao hata kama ni msimu wa kilimo wao huchunguza chunguza mawingu na mwishowe wanashindwa kupanda mbegu zao.
Tabia ya kujihatarisha ni njema na imewasaidia wengi. Fanya kitu kwa wakati uchunguzi utakuja baadaye! Amesema Ratan Naval Tata mwanzilishi wa kampuni ya kutengeneza mitambo na magari aina ya TATA, “I don’t believe in taking right decision, I take decisions and then make them right” kwa tafsiri yangu amesema, “Siamini katika kuchukua maamuzi sahihi, bali nafanya maamuzi na baadaye nayafanya kuwa maamuzi sahihi”
Kujihatarisha inaweza ikawa ni kuachana na uhusiano mbaya, inaweza ikawa ni kuhama mji mmoja kwenda mwingine, inaweza ikawa ni kufunga na kuomba licha ya dalili za vidonda vya tumbo. Inawezekana ikawa ni kurejea nyumbani usiku kila siku kwa sababu za msingi, au ikawa ni kuamka mapema. Pia kujihatarisha inaweza ikawa ni kufanya kinyume na walio wengi, kwenda katika upekee wako au katika njia ya ubunifu ambayo wengi hawapiti. Vyovyote vile kama hatukujihatarisha kabisa hatutapata badiliko lolote.
Matajiri wengi akiwemo Bill Gates na Oprah Winfrey wamekuwa na sifa ya kukatiza masomo au kuacha kabisa ili kwenda kutumikia ndoto zao. Hii nayo ni kujihatarisha, kuacha kile ambacho dunia inaamini ni ufunguo wa maisha ilikuwa ni sawa na kuyafunga maisha yao. Lakini pamoja na hatari ya kuacha shule bado wamefanikiwa na wamewaajiri waliohudhuria vizuri shuleni. Kama kunamafanikio nje ya elimu basi ni muhimu tukajua elimu si ufunguo pekee. Maisha ni zaidi ya vidato!
Maskini wote wanachukia vurugu na hatari, hawapendi biashara nje ya kiyoyozi hata mara moja hawajitumi kutembeza bidhaa. Wanapenda usalama, kulala mapema na kuchelewa kuamka. Hawapendi kusafiri juu ya magari aina ya Fuso yanayokwenda minadani, wanapenda usafiri tulivu na salama, hawataki usumbufu wa wachuuzi wadogo wadogo wenye kutembeza biashara. Hawawazi kuajiri, wao wanataka kuajiriwa tu!
Nakumbuka mwaka 2015 baada ya sala na maombi niliamua kuondoka nyumbani umbali wa  mikoa mitano na kuhamia jijini Dar-es-salaam na ndani ya miezi miwili nilipata nilichokuwa nahitaji kwa muda ule. Si kila mtu atafanikiwa mjini wengine wanahitaji kurudi vijijini na wengine kwenda mjini ili kukutana na mafanikio yao. Ili kukutana na ndoto zao wengine itawalazimu kutoka Ulaya na kurejea katika nchi zao.
Unapopanga mipango yako mipya weka na mipango yenye kukuhatarisha (bila kuvunja sheria) na ndiyo mipango ya mafanikio.
Take risks, if possible take calculated risk……

2018 Mwaka wa Masahihisho

2018
MWAKA WA MASAHIHISHO
Kama wanadamu tunakosea na kila mwaka unatupa fursa ya kufanya mambo mawili mosi, unatupa fursa ya kufanya mambo mazuri na sahihi; pili, unatupa fursa ya kukosea. Amesema mzaburi, “BWANA kama wewe ungehesabu maovu yetu nani angesimama?” Kwa siku zaidi ya mia tatu za mwaka 2017 yako mengi yasiofaa ambayo tumeyatenda na hayapaswi kuendelea kufanyika; yako pia ya kufaa ambayo yanatakiwa kuendelezwa katika mwaka 2018. Yako pia mazuri ambayo tulitakiwa kufanya na hatukuyafanya!
Kwa kuwa katika mwaka 2017 kulikuwa na makosa na mapungufu ambayo kwa hekima ya kawaida huwa tunayachukua kama shule kwa ajili ya mwaka 2018 basi mapungufu hayo yasituumize. Hatutegemei katika mwaka 2018 kuendelea na makosa ya 2017 ambayo tumesha hitimu shule yake.
Tunaweza kutaka mabadiliko katika mwaka 2018 na tusiweze, pengine nguvu zetu ni kidogo na hutuwezi kugeuka, lakini uko msalaba na iko damu ya Yesu! Nguvu ile iliyohuisha mwili wake kaburini naye akafufuka mzima, yaweza kutuhuisha roho zetu na dhambi na kutufanya kuwa watu bora kabisa katika mwaka 2018. Najua nguvu zetu ni kidogo lakini panapo msalaba pana nguvu kubwa ya mageuzi.
Mamilioni ya watu wamekuwa wakipinduliwa kwa nguvu ya msalaba toka utumwa wa dhambi mpaka utakatifu. Nguvu hii ni kwa ajili yetu katika mwaka 2018. Kama tulikosea 2017 imetosha sasa, sasa tumejifunza, sasa ni wakati wa kugeuka. Moja na malengo yako katika mwaka 2018 ni muhimu kuwa kufanya yale uliyotakiwa kuyafanya katika mwaka 2017 na hukufanya. Hii pia ni lengo la kizazi cha sasa yaani, kufanya yale ambayo vizazi vilivyopita vilitakiwa kufanya na havikufanya. Mwalimu Jim Rohn amesema jambo la kufanana na somo hili, “Don’t let learning from your own experiences take too long. If you have been doing it wrong for the last ten years, I would suggest that’s long enough
Masahihisho ni jambo jema kabla ya hukumu, masahihisho yanatupa nafasi ya kujitathmini, kujikosoa na kuanza upya, kamwe yasitazamwe kama hukumu. Katika kitabu nikipendacho cha, “The Virgin Way” kilichoandikwa na Richard Branson imesisitizwa kama unafanya makosa na uyafanye haraka. Kipindi chako cha kukosea na kujifunza kutokana na makosa kisiwe kipindi kirefu mno. Hii imepelekea kukusihi, mwaka 2018 iwe muda wako wa kuanza upya. If you’re doing a mistake do it very quickly in these few days before 2018.
Tufikapo 2018 tuwe wapya tayari kwa ushindi.
Barikiwa!

Inachukua Muda....

 
Inachukua Muda...

Tunaishi katika ulimwengu ambao karibu kila eneo watu hutaka huduma kwa haraka; usafiri wa haraka (mwendokasi), chakula cha haraka (fast food), mikopo ya haraka, huduma za kifedha na afya kwa haraka (fast track) n.k ! Hakuna anayetaka kukaa muda mrefu kwenye foleni kusubiria huduma. Maendeleo ya sayansi na tekinolojia yamerahisisha upatikana wa huduma nyingi katika jamii na kwa haraka zaidi wakati huu, kuliko miaka kumi iliyopita.
Pamoja na mchango mkubwa wa sayansi na tekinolojia katika upatikanaji wa huduma, watu wengi wamesahau baadhi ya kanuni muhimu za mafanikio ya kweli; katika ulimwengu huu wa haraka haraka, jamii imesahau kuwa mafanikio ya kudumu huchukua muda kuyajenga. Kanuni hii ni rahisi sana kusahaulika katika ulimwengu wa haraka.  Ya kwamba mahusiano mazuri yanachukua muda kuyajenga, familia nzuri inachukua muda kuijenga, mafanikio ya kifedha, huduma, taaluma pamoja na 'career' haya yote huchukua muda kuyajenga.
Ni mwanafunzi anayeamini katika ulimwengu wa haraka kwenye taalumu hufanya bidii aweze kuiba au kuibia kwenye mtihani, ni kijana anayeamini tu katika ulimwengu wa haraka hushinda kijiweni "akibeti" ili kufikia mafanikio ya kifedha. Ndio maana ni rahisi kwa mtu kwenda kucheza "desi" ili apokee mara asilimia mia tatu (300%) kuliko kuwekeza kwenye ufugaji wa kuku, kwa sababu anaona hatapata hiyo asilimia mia tatu haraka. Hutaka kupata kwa haraka bila kufanyia kazi. Nitajie tajiri aliyeko kwenye orodha ya matajiri kwa sababu alishida bahati nasibu au desi; go back to Work!!
Watu ambao hawajui kuwa mahusiano bora na imara huchukua muda kuyajenga wakitofautiana kidogo huvunja uhusiano huo na kama ni wana ndoa hutishia kutengana kabisa. Mzazi ambaye anayeamini katika ulimwengu wa haraka katika malezi, hana muda wa kukaa  na watoto kuwafundisha na kufuatilia malezi yao kwa karibu; wakishapotea na kuharibika kimwenendo hukimbilia kwa watumishi wamuombee ili wapone na kurudi kwenye njia sahihi kwa haraka, amesahau alikuwa na nafasi katika kujenga mwenendo bora kabla.
Anayejenga nyumba juu ya mwamba hutumia muda kuijenga, na kwa sababu hiyo nyumba hiyo itakuwa imara kuliko anayejenga juu ya mchanga.  Kuna baadhi ya maeneo ulimwengu wa haraka hauleti matokeo bora, bali kanuni ya muda!  Mwenyehekima mmoja amewahi kusema "usikimbie mahali panapokutaka kutembea; na usitembee mahali panapokutaka kukimbia "
Mali iliyopatikana kwa haraka itapunguka; Bali yeye achumaye kidogo kidogo atazidishiwa-Mithali 13 :11
There's a place for you at the top