BIBLIA
INAMAJIBU YOTE
ISOME!
Ni
mwaka mpya sasa nuia idadi ya vitabu unavyopaswa kusoma mwaka 2018, zaidi ya
yote usisahau mpango wa kusoma Biblia, yearly bible reading plan! Tatizo la
kutokusoma linaendelea kuwatesa watu wa leo, kizazi hiki hakijajijengea tabia
ya kujisomea. Majibu mengi ya matatizo yetu yanayotukumba katika maisha ya kila
siku yako katika vitabu, bahati mbaya hatusomi.
Hivi
karibuni nikiwa naelekea Bagamoyo kwenye daladala nilifarijika baada ya mtoto
wa miaka kumi kuingia ndani ya gari na kisha kutoa kitabu na baada ya mwendo
kidogo akaanza kusoma. Nilitamani kupiga naye picha (selfie) kwa furaha, kuona
utamaduni ninao upenda umejengeka kwa mtoto yule. Miji na majiji yenye foleni
hutoa fursa kwa watu kujisomea wakiwa barabarani. Nyumbani utasema watoto
wasumbufu barabarani je? Furaha tunayoikosa vijiweni iko kitabuni, nguvu
tunayoikosa pahala pa kazi iko vitabuni, knowledge is power!! Mwenye maarifa
mengi ni mwenye nguvu nyingi hili halipingiki. Kile ambacho baba yangu hakusema
vitabu vimeniambia, kile ambacho dini ilinificha vitabu vimeniweka bayana. What a royal friend!
Nakushauri
usome vitabu, lakini soma zaidi Biblia. Katika neno la Mungu kuna umilele wote.
Yesu akasema, “ninyi mmekuwa safi kwa sababu ya lile neno mliliosikia”. Lile
neno la Mungu unalosikia linafanya unakuwa safi mwili na roho.
Neno
la Mungu limebeba majibu ya hali unazopitia wewe binafsi na Taifa lako pia. Unapotazama
uchumi wako na hali ya taifa lako usiende tu kwa kutumia elimu ya uchumi ya
darasani, ni muhimu utazame kiroho pia. Ukiona hali ngumu ya uchumi kwenye nchi
jiulize Mungu anataka nini kwa taifa lako, inawezekana kabisa anataka toba. Badala
ya kwenda kuchukua shahada ya uzamili ya uchumi mara nyingine ni muhimu kusoma
Biblia mfululuzo. Daniel kwa kusoma maandiko (neno la Mungu) aligundua nini
kinaendelea kwenye taifa lake.
Jifunze
kujua chanzo, anayejua chanzo halalamiki sana. Taifa linapopewa mtawala mkorofi
ni lazima ujue kuna mahali dhambi ilitendeka katika Taifa hilo na Mungu
amemweka mtawala huyo kwa makusudi yake ili watu wake watubu na kurejea. Katika
hali kama hiyo kufanya kazi kwa bidii hakutasaidia ila toba ya kweli kwa
wateule wote wa Mungu walioko kwenye taifa hilo inaweza kuleta suluhisho.
Moja
ya njia kuu ambayo Mungu amekuwa akiitumia kuzungumza na nchi na watu binafsi
ni hali ya uchumi. Ukiaona kuna mvua ya kutosha, tena kwa wakati wake ni lazima
ujue kuna kitu kizuri Mungu anazungumza, ukiona ukame na watu wanakufa kwa njaa
ujue kuna kitu Mungu anadai au ibada ya sanamu imekithiri, ukiona watu wengi
wanakimbia nchi ujue kuna laana ya ukiwa.
Katika
kila jambo lihusulo hali ya hewa, mahali pa kuishi, hali ya uchumi ni muhimu
utafute makusudi ya Mungu katika Biblia. Mambo haya yote ndani yake kuna
makusudi ya Mungu, ukiyatafute ndani ya neno la Mungu utayajua! Jipatie ufahamu
uyajue yanayokuhusu na yanayohusu nchi yako kwa kusoma maandiko. Barikiwa.
BWANA ALIPOAMURU BARAKA
MUDA MWAFAKA ENEO
MWAFAKA.
Katika mambo ambayo Mungu hata subiri
ufanye maandalizi ni hukumu na fursa. Kila siku unapaswa kuwa tayari, katika
eneo husika, mwenye maandalizi kamili, ndio maana ya lile neno kesheni. Si kila
eneo, si kila Mkoa, si kila medani wala si kila nchi itakuwa na Baraka zako;
liko eneo moja, iko aina ya biashara fulani, uko mkoa na pahala ambapo Mungu
ameamuru baraka zako zipatikane. Wakati mwingine tunachagua miji kwa macho ya
nyama na hivyo tunavyokwenda ndani yake hatufanikiwi sana. Si kila aliyeko
Ulaya anamafanikio, kuna wengine wako huko na wanaomba chakula, hawana uhakika
wa kupata milo mitatu.
Kuna watu ambao walikuwa jijini Dar es
salaam ilhali baraka yao ilikuwa Dodoma. Kwa vyovyote vile haikuwa rahisi
kuwapeleka watu hao Dodoma inawezekana walifikiri hakuna maisha bora nje ya
jiji la Dar es salaam. Lakini Mungu kwa
kutumia Tangazo la Serikali la kuhamia Dodoma amewawezesha pia maelfu ya
watanzania kwenda kwenye baraka yao iliyoamriwa mjini Dodoma. Tangu nyakati
za Yesu Kristo mpaka sasa matangazo mengi ya Serikali yamekuwa yakibeba
makusudi ya Mungu ya amani. Amani maana yake uchumi mzuri, Baraka na mafanikio.
Yanaweza matangazo hayo yakaonekana magumu na mabaya yenye kubeba usumbufu
lakini baadaye Mungu hujitwalia utukufu na watu wake hustawi.
Ukihamishwa
kwa Tangazo la Serikali usigome, Matangazo hayo hubeba baraka. Katika saa yako ya kusimama kiuchumi na
kiutumishi tangazo hilo halitaweza kukudhuru hata kama lilitolewa ili
kukuangamiza wewe. Tangazo la Herode la kuua watoto wote chini ya miaka miwili
halikuweza kumua Yesu maana ilikuwa ni wakati wa Yesu kung’aa na kuokoa, halikuweza
kumzuia.
Si miji peke yake, hata changamoto nyingine
za maisha zenye ukakasi ndani yake kuna
baraka pia. Wako watu ambao bila talaka wasingelipata wokovu, bila kuachwa
wasingelijua kusimama wenyewe, wako wale ambao bila kufeli masomo wasingeli
jaribu biashara ambazo leo zimewapandisha na kuwafanya wakuu.
Baraka hizo zisingepatikana ikiwa kila kitu
kingekuwa shwari, mara nyingi inapokuwa ni shwari watu hujisahau sana na
kufanya yasiyo ya msingi. Biblia inasema, “Katika shida yangu nalimwona BWANA”. Kuna nyakati ambapo ni kupitia shida
na usumbufu tunaweza kumwona Mungu. Ni methali ya zamani ya wazungu, “Bahari
shwari haitoi wanamaji hodari” ni kweli baharia hodari ni lazima atakuwa na
uzoefu wa kutatua shida za majini.
Usiogope sura ya mji, usiogope ukubwa wa
changamoto inayokukabiri; cha msingi hakikisha uko mahali sahihi ukisubiri
wakati sahihi wa kuinuliwa kwako. Mahali ambapo Mungu ameamuru baraka pana
changamoto lakini pia pana baraka nyingi. Kuwa mahali pa baraka haina maana
hapatakuwa na changamoto kabisa! Mara nyingi ustawi wako katika eneo hilo
utategemea pia namna unavyomkumbuka Mungu, kumkumbuka maana yake kushika amri
zake na kumshuhudia kwamba ni yeye ni Mungu aliyekufikisha hapo Sayuni yako.
Barikiwa na Endelea mbele…
MWAKA 2018
UWE MWAKA WA KUJIHATARISHA ZAIDI ILI KUPATA MAFANIKIO
Wengi
wanashindwa kwa sababu hawafanyi kitu mpaka waone ni salama kabisa, hawaanzi
mradi mpaka waone ni faida tupu, tabia hii imezuia mafanikio ya wengi. Mwaka
jana niliingia kwenye biashara ya mtandaoni (online business) na kupata hasara
ya milioni nne, mwaka huo huo bila ya kukata tamaa nikaingia katika biashara
nyingine na kupata faida ya milioni nne! Ukipata hasara katika biashara moja
haina maana kwamba na biashara nyingine utapata hasara pia.
Kitabu
cha Mhubiri kinasema, “Mwenye
kuuangalia upepo hatapanda; Naye ayatazamaye mawingu hatavuna” Mhubiri
11:4. Ukichunguza chunguza sana huji kufanikiwa katika uwekezaji na maendeleo.
Kuna wakulima ambao wakijua ni msimu wa kilimo wanalima na hawa ndio
hufanikiwa. Na kuna wale ambao hata kama ni msimu wa kilimo wao huchunguza
chunguza mawingu na mwishowe wanashindwa kupanda mbegu zao.
Tabia
ya kujihatarisha ni njema na imewasaidia wengi. Fanya kitu kwa wakati uchunguzi
utakuja baadaye! Amesema Ratan Naval Tata mwanzilishi wa kampuni ya kutengeneza
mitambo na magari aina ya TATA, “I don’t believe in taking right decision, I
take decisions and then make them right” kwa tafsiri yangu amesema, “Siamini
katika kuchukua maamuzi sahihi, bali nafanya maamuzi na baadaye nayafanya kuwa
maamuzi sahihi”
Kujihatarisha
inaweza ikawa ni kuachana na uhusiano mbaya, inaweza ikawa ni kuhama mji mmoja
kwenda mwingine, inaweza ikawa ni kufunga na kuomba licha ya dalili za vidonda
vya tumbo. Inawezekana ikawa ni kurejea nyumbani usiku kila siku kwa sababu za
msingi, au ikawa ni kuamka mapema. Pia kujihatarisha inaweza ikawa ni kufanya
kinyume na walio wengi, kwenda katika upekee wako au katika njia ya ubunifu
ambayo wengi hawapiti. Vyovyote vile kama hatukujihatarisha kabisa hatutapata
badiliko lolote.
Matajiri
wengi akiwemo Bill Gates na Oprah Winfrey wamekuwa na sifa ya kukatiza masomo
au kuacha kabisa ili kwenda kutumikia ndoto zao. Hii nayo ni kujihatarisha,
kuacha kile ambacho dunia inaamini ni ufunguo wa maisha ilikuwa ni sawa na
kuyafunga maisha yao. Lakini pamoja na hatari ya kuacha shule bado wamefanikiwa
na wamewaajiri waliohudhuria vizuri shuleni. Kama kunamafanikio nje ya elimu
basi ni muhimu tukajua elimu si ufunguo pekee. Maisha ni zaidi ya vidato!
Maskini
wote wanachukia vurugu na hatari, hawapendi biashara nje ya kiyoyozi hata mara
moja hawajitumi kutembeza bidhaa. Wanapenda usalama, kulala mapema na kuchelewa
kuamka. Hawapendi kusafiri juu ya magari aina ya Fuso yanayokwenda minadani,
wanapenda usafiri tulivu na salama, hawataki usumbufu wa wachuuzi wadogo wadogo
wenye kutembeza biashara. Hawawazi kuajiri, wao wanataka kuajiriwa tu!
Nakumbuka
mwaka 2015 baada ya sala na maombi niliamua kuondoka nyumbani umbali wa mikoa mitano na kuhamia jijini Dar-es-salaam
na ndani ya miezi miwili nilipata nilichokuwa nahitaji kwa muda ule. Si kila
mtu atafanikiwa mjini wengine wanahitaji kurudi vijijini na wengine kwenda
mjini ili kukutana na mafanikio yao. Ili kukutana na ndoto zao wengine
itawalazimu kutoka Ulaya na kurejea katika nchi zao.
Unapopanga
mipango yako mipya weka na mipango yenye kukuhatarisha (bila kuvunja sheria) na ndiyo mipango ya mafanikio.
Take risks,
if possible take calculated risk……
2018
MWAKA WA MASAHIHISHO
Kama wanadamu tunakosea na kila mwaka
unatupa fursa ya kufanya mambo mawili mosi, unatupa fursa ya kufanya mambo
mazuri na sahihi; pili, unatupa fursa ya kukosea. Amesema mzaburi, “BWANA kama
wewe ungehesabu maovu yetu nani angesimama?” Kwa siku zaidi ya mia tatu za
mwaka 2017 yako mengi yasiofaa ambayo tumeyatenda na hayapaswi kuendelea
kufanyika; yako pia ya kufaa ambayo yanatakiwa kuendelezwa katika mwaka 2018. Yako
pia mazuri ambayo tulitakiwa kufanya na hatukuyafanya!
Kwa kuwa katika mwaka 2017 kulikuwa na
makosa na mapungufu ambayo kwa hekima ya kawaida huwa tunayachukua kama shule
kwa ajili ya mwaka 2018 basi mapungufu hayo yasituumize. Hatutegemei katika
mwaka 2018 kuendelea na makosa ya 2017 ambayo tumesha hitimu shule yake.
Tunaweza kutaka mabadiliko katika mwaka
2018 na tusiweze, pengine nguvu zetu ni kidogo na hutuwezi kugeuka, lakini uko
msalaba na iko damu ya Yesu! Nguvu ile iliyohuisha mwili wake kaburini naye
akafufuka mzima, yaweza kutuhuisha roho zetu na dhambi na kutufanya kuwa watu
bora kabisa katika mwaka 2018. Najua nguvu zetu ni kidogo lakini panapo msalaba
pana nguvu kubwa ya mageuzi.
Mamilioni ya watu wamekuwa wakipinduliwa
kwa nguvu ya msalaba toka utumwa wa dhambi mpaka utakatifu. Nguvu hii ni kwa
ajili yetu katika mwaka 2018. Kama tulikosea 2017 imetosha sasa, sasa
tumejifunza, sasa ni wakati wa kugeuka. Moja na malengo yako katika mwaka 2018
ni muhimu kuwa kufanya yale uliyotakiwa kuyafanya katika mwaka 2017 na
hukufanya. Hii pia ni lengo la kizazi cha sasa yaani, kufanya yale ambayo
vizazi vilivyopita vilitakiwa kufanya na havikufanya. Mwalimu Jim Rohn amesema
jambo la kufanana na somo hili, “Don’t
let learning from your own experiences take too long. If you have been doing it
wrong for the last ten years, I would suggest that’s long enough”
Masahihisho ni jambo jema kabla ya hukumu,
masahihisho yanatupa nafasi ya kujitathmini, kujikosoa na kuanza upya, kamwe
yasitazamwe kama hukumu. Katika kitabu nikipendacho cha, “The Virgin Way” kilichoandikwa na Richard Branson imesisitizwa kama
unafanya makosa na uyafanye haraka. Kipindi chako cha kukosea na kujifunza
kutokana na makosa kisiwe kipindi kirefu mno. Hii imepelekea kukusihi, mwaka
2018 iwe muda wako wa kuanza upya. If
you’re doing a mistake do it very quickly in these few days before 2018.
Tufikapo 2018
tuwe wapya tayari kwa ushindi.
Barikiwa!
Inachukua
Muda...
Tunaishi katika ulimwengu ambao karibu
kila eneo watu hutaka huduma kwa haraka; usafiri wa haraka (mwendokasi),
chakula cha haraka (fast food), mikopo ya haraka, huduma za kifedha na afya kwa
haraka (fast track) n.k ! Hakuna anayetaka kukaa muda mrefu kwenye foleni kusubiria
huduma. Maendeleo ya sayansi na tekinolojia yamerahisisha upatikana wa huduma
nyingi katika jamii na kwa haraka zaidi wakati huu, kuliko miaka kumi iliyopita.
Pamoja na mchango mkubwa wa sayansi na
tekinolojia katika upatikanaji wa huduma, watu wengi wamesahau baadhi ya kanuni
muhimu za mafanikio ya kweli; katika ulimwengu huu wa haraka haraka, jamii
imesahau kuwa mafanikio ya kudumu huchukua muda kuyajenga. Kanuni hii ni rahisi
sana kusahaulika katika ulimwengu wa haraka.
Ya kwamba mahusiano mazuri yanachukua muda kuyajenga, familia nzuri
inachukua muda kuijenga, mafanikio ya kifedha, huduma, taaluma pamoja na 'career'
haya yote huchukua muda kuyajenga.
Ni mwanafunzi anayeamini katika ulimwengu
wa haraka kwenye taalumu hufanya bidii aweze kuiba au kuibia kwenye mtihani, ni
kijana anayeamini tu katika ulimwengu wa haraka hushinda kijiweni "akibeti"
ili kufikia mafanikio ya kifedha. Ndio maana ni rahisi kwa mtu kwenda kucheza "desi"
ili apokee mara asilimia mia tatu (300%) kuliko kuwekeza kwenye ufugaji wa kuku,
kwa sababu anaona hatapata hiyo asilimia mia tatu haraka. Hutaka kupata kwa
haraka bila kufanyia kazi. Nitajie tajiri aliyeko kwenye orodha ya matajiri kwa
sababu alishida bahati nasibu au desi; go back to Work!!
Watu ambao hawajui kuwa mahusiano bora na
imara huchukua muda kuyajenga wakitofautiana kidogo huvunja uhusiano huo na
kama ni wana ndoa hutishia kutengana kabisa. Mzazi ambaye anayeamini katika
ulimwengu wa haraka katika malezi, hana muda wa kukaa na watoto kuwafundisha na kufuatilia malezi yao
kwa karibu; wakishapotea na kuharibika kimwenendo hukimbilia kwa watumishi
wamuombee ili wapone na kurudi kwenye njia sahihi kwa haraka, amesahau alikuwa
na nafasi katika kujenga mwenendo bora kabla.
Anayejenga nyumba juu ya mwamba hutumia muda
kuijenga, na kwa sababu hiyo nyumba hiyo itakuwa imara kuliko anayejenga juu ya
mchanga. Kuna baadhi ya maeneo ulimwengu
wa haraka hauleti matokeo bora, bali kanuni ya muda! Mwenyehekima mmoja amewahi kusema
"usikimbie mahali panapokutaka kutembea; na usitembee mahali panapokutaka
kukimbia "
Mali iliyopatikana kwa haraka itapunguka;
Bali yeye achumaye kidogo kidogo atazidishiwa-Mithali 13 :11
There's a place for you at
the top