Mwaka 2018 Uwe Mwaka wa Kujihatarisha.......

 
MWAKA 2018 UWE MWAKA WA KUJIHATARISHA ZAIDI ILI KUPATA MAFANIKIO
Wengi wanashindwa kwa sababu hawafanyi kitu mpaka waone ni salama kabisa, hawaanzi mradi mpaka waone ni faida tupu, tabia hii imezuia mafanikio ya wengi. Mwaka jana niliingia kwenye biashara ya mtandaoni (online business) na kupata hasara ya milioni nne, mwaka huo huo bila ya kukata tamaa nikaingia katika biashara nyingine na kupata faida ya milioni nne! Ukipata hasara katika biashara moja haina maana kwamba na biashara nyingine utapata hasara pia.
Kitabu cha Mhubiri kinasema, “Mwenye kuuangalia upepo hatapanda; Naye ayatazamaye mawingu hatavuna” Mhubiri 11:4. Ukichunguza chunguza sana huji kufanikiwa katika uwekezaji na maendeleo. Kuna wakulima ambao wakijua ni msimu wa kilimo wanalima na hawa ndio hufanikiwa. Na kuna wale ambao hata kama ni msimu wa kilimo wao huchunguza chunguza mawingu na mwishowe wanashindwa kupanda mbegu zao.
Tabia ya kujihatarisha ni njema na imewasaidia wengi. Fanya kitu kwa wakati uchunguzi utakuja baadaye! Amesema Ratan Naval Tata mwanzilishi wa kampuni ya kutengeneza mitambo na magari aina ya TATA, “I don’t believe in taking right decision, I take decisions and then make them right” kwa tafsiri yangu amesema, “Siamini katika kuchukua maamuzi sahihi, bali nafanya maamuzi na baadaye nayafanya kuwa maamuzi sahihi”
Kujihatarisha inaweza ikawa ni kuachana na uhusiano mbaya, inaweza ikawa ni kuhama mji mmoja kwenda mwingine, inaweza ikawa ni kufunga na kuomba licha ya dalili za vidonda vya tumbo. Inawezekana ikawa ni kurejea nyumbani usiku kila siku kwa sababu za msingi, au ikawa ni kuamka mapema. Pia kujihatarisha inaweza ikawa ni kufanya kinyume na walio wengi, kwenda katika upekee wako au katika njia ya ubunifu ambayo wengi hawapiti. Vyovyote vile kama hatukujihatarisha kabisa hatutapata badiliko lolote.
Matajiri wengi akiwemo Bill Gates na Oprah Winfrey wamekuwa na sifa ya kukatiza masomo au kuacha kabisa ili kwenda kutumikia ndoto zao. Hii nayo ni kujihatarisha, kuacha kile ambacho dunia inaamini ni ufunguo wa maisha ilikuwa ni sawa na kuyafunga maisha yao. Lakini pamoja na hatari ya kuacha shule bado wamefanikiwa na wamewaajiri waliohudhuria vizuri shuleni. Kama kunamafanikio nje ya elimu basi ni muhimu tukajua elimu si ufunguo pekee. Maisha ni zaidi ya vidato!
Maskini wote wanachukia vurugu na hatari, hawapendi biashara nje ya kiyoyozi hata mara moja hawajitumi kutembeza bidhaa. Wanapenda usalama, kulala mapema na kuchelewa kuamka. Hawapendi kusafiri juu ya magari aina ya Fuso yanayokwenda minadani, wanapenda usafiri tulivu na salama, hawataki usumbufu wa wachuuzi wadogo wadogo wenye kutembeza biashara. Hawawazi kuajiri, wao wanataka kuajiriwa tu!
Nakumbuka mwaka 2015 baada ya sala na maombi niliamua kuondoka nyumbani umbali wa  mikoa mitano na kuhamia jijini Dar-es-salaam na ndani ya miezi miwili nilipata nilichokuwa nahitaji kwa muda ule. Si kila mtu atafanikiwa mjini wengine wanahitaji kurudi vijijini na wengine kwenda mjini ili kukutana na mafanikio yao. Ili kukutana na ndoto zao wengine itawalazimu kutoka Ulaya na kurejea katika nchi zao.
Unapopanga mipango yako mipya weka na mipango yenye kukuhatarisha (bila kuvunja sheria) na ndiyo mipango ya mafanikio.
Take risks, if possible take calculated risk……

2018 Mwaka wa Masahihisho

2018
MWAKA WA MASAHIHISHO
Kama wanadamu tunakosea na kila mwaka unatupa fursa ya kufanya mambo mawili mosi, unatupa fursa ya kufanya mambo mazuri na sahihi; pili, unatupa fursa ya kukosea. Amesema mzaburi, “BWANA kama wewe ungehesabu maovu yetu nani angesimama?” Kwa siku zaidi ya mia tatu za mwaka 2017 yako mengi yasiofaa ambayo tumeyatenda na hayapaswi kuendelea kufanyika; yako pia ya kufaa ambayo yanatakiwa kuendelezwa katika mwaka 2018. Yako pia mazuri ambayo tulitakiwa kufanya na hatukuyafanya!
Kwa kuwa katika mwaka 2017 kulikuwa na makosa na mapungufu ambayo kwa hekima ya kawaida huwa tunayachukua kama shule kwa ajili ya mwaka 2018 basi mapungufu hayo yasituumize. Hatutegemei katika mwaka 2018 kuendelea na makosa ya 2017 ambayo tumesha hitimu shule yake.
Tunaweza kutaka mabadiliko katika mwaka 2018 na tusiweze, pengine nguvu zetu ni kidogo na hutuwezi kugeuka, lakini uko msalaba na iko damu ya Yesu! Nguvu ile iliyohuisha mwili wake kaburini naye akafufuka mzima, yaweza kutuhuisha roho zetu na dhambi na kutufanya kuwa watu bora kabisa katika mwaka 2018. Najua nguvu zetu ni kidogo lakini panapo msalaba pana nguvu kubwa ya mageuzi.
Mamilioni ya watu wamekuwa wakipinduliwa kwa nguvu ya msalaba toka utumwa wa dhambi mpaka utakatifu. Nguvu hii ni kwa ajili yetu katika mwaka 2018. Kama tulikosea 2017 imetosha sasa, sasa tumejifunza, sasa ni wakati wa kugeuka. Moja na malengo yako katika mwaka 2018 ni muhimu kuwa kufanya yale uliyotakiwa kuyafanya katika mwaka 2017 na hukufanya. Hii pia ni lengo la kizazi cha sasa yaani, kufanya yale ambayo vizazi vilivyopita vilitakiwa kufanya na havikufanya. Mwalimu Jim Rohn amesema jambo la kufanana na somo hili, “Don’t let learning from your own experiences take too long. If you have been doing it wrong for the last ten years, I would suggest that’s long enough
Masahihisho ni jambo jema kabla ya hukumu, masahihisho yanatupa nafasi ya kujitathmini, kujikosoa na kuanza upya, kamwe yasitazamwe kama hukumu. Katika kitabu nikipendacho cha, “The Virgin Way” kilichoandikwa na Richard Branson imesisitizwa kama unafanya makosa na uyafanye haraka. Kipindi chako cha kukosea na kujifunza kutokana na makosa kisiwe kipindi kirefu mno. Hii imepelekea kukusihi, mwaka 2018 iwe muda wako wa kuanza upya. If you’re doing a mistake do it very quickly in these few days before 2018.
Tufikapo 2018 tuwe wapya tayari kwa ushindi.
Barikiwa!

Inachukua Muda....

 
Inachukua Muda...

Tunaishi katika ulimwengu ambao karibu kila eneo watu hutaka huduma kwa haraka; usafiri wa haraka (mwendokasi), chakula cha haraka (fast food), mikopo ya haraka, huduma za kifedha na afya kwa haraka (fast track) n.k ! Hakuna anayetaka kukaa muda mrefu kwenye foleni kusubiria huduma. Maendeleo ya sayansi na tekinolojia yamerahisisha upatikana wa huduma nyingi katika jamii na kwa haraka zaidi wakati huu, kuliko miaka kumi iliyopita.
Pamoja na mchango mkubwa wa sayansi na tekinolojia katika upatikanaji wa huduma, watu wengi wamesahau baadhi ya kanuni muhimu za mafanikio ya kweli; katika ulimwengu huu wa haraka haraka, jamii imesahau kuwa mafanikio ya kudumu huchukua muda kuyajenga. Kanuni hii ni rahisi sana kusahaulika katika ulimwengu wa haraka.  Ya kwamba mahusiano mazuri yanachukua muda kuyajenga, familia nzuri inachukua muda kuijenga, mafanikio ya kifedha, huduma, taaluma pamoja na 'career' haya yote huchukua muda kuyajenga.
Ni mwanafunzi anayeamini katika ulimwengu wa haraka kwenye taalumu hufanya bidii aweze kuiba au kuibia kwenye mtihani, ni kijana anayeamini tu katika ulimwengu wa haraka hushinda kijiweni "akibeti" ili kufikia mafanikio ya kifedha. Ndio maana ni rahisi kwa mtu kwenda kucheza "desi" ili apokee mara asilimia mia tatu (300%) kuliko kuwekeza kwenye ufugaji wa kuku, kwa sababu anaona hatapata hiyo asilimia mia tatu haraka. Hutaka kupata kwa haraka bila kufanyia kazi. Nitajie tajiri aliyeko kwenye orodha ya matajiri kwa sababu alishida bahati nasibu au desi; go back to Work!!
Watu ambao hawajui kuwa mahusiano bora na imara huchukua muda kuyajenga wakitofautiana kidogo huvunja uhusiano huo na kama ni wana ndoa hutishia kutengana kabisa. Mzazi ambaye anayeamini katika ulimwengu wa haraka katika malezi, hana muda wa kukaa  na watoto kuwafundisha na kufuatilia malezi yao kwa karibu; wakishapotea na kuharibika kimwenendo hukimbilia kwa watumishi wamuombee ili wapone na kurudi kwenye njia sahihi kwa haraka, amesahau alikuwa na nafasi katika kujenga mwenendo bora kabla.
Anayejenga nyumba juu ya mwamba hutumia muda kuijenga, na kwa sababu hiyo nyumba hiyo itakuwa imara kuliko anayejenga juu ya mchanga.  Kuna baadhi ya maeneo ulimwengu wa haraka hauleti matokeo bora, bali kanuni ya muda!  Mwenyehekima mmoja amewahi kusema "usikimbie mahali panapokutaka kutembea; na usitembee mahali panapokutaka kukimbia "
Mali iliyopatikana kwa haraka itapunguka; Bali yeye achumaye kidogo kidogo atazidishiwa-Mithali 13 :11
There's a place for you at the top

Mtu Jasiri

MTU JASIRI
Katika ulimwengu wa sasa majasiri wengi hawajulikani. Dunia ya leo imewatukuza wasemaji ikaacha wakimya, imemdharau mtu mpole ikampa heshima mtu mkali. Katika vikao wasikilizaji wazuri hawatambuliwi kama majasiri wa kusema. Kusikiliza si jambo jepesi, hakuna mtu mgumu kumsikiliza kama mtu mkorofi na mtu asiyejua.
Si wengi wanauzoefu na uwezo wa kusikiliza kwa makini, wengi hupenda kusikilizwa si kusikiliza. Huwezi kusikiliza na huku unatazama televisheni au unasikiliza redio. Ni rahisi kuukusanya mwili lakini si akili ya usikivu. Huwezi kusikiliza ikiwa unataka kusema, unaweza kusikiliza ikiwa unataka kusikiliza. Alisema Winston Churchil, “Courage is not only what it takes to stand up and talk but courage is also what it takes to sit down and listen” kwa tafsiri “Inamhitaji mtu jasiri kusimama na kuzungumza, lakini inamhitaji mtu jasiri pia kukaa kimya na kusikiliza”.
Amenukuliwa mzee Kinana Katibu Mkuu CCM akisema, “kiongozi lazima asikilize wananchi”.  Kiongozi si lazima awe kwenye kampuni, kwenye taasisi ya umma au kwenye siasa, badala yake anaweza akawa kwenye familia baba wa familia, mama wa familia, kaka wa familia au dada wa familia.  Siku chache katika nafasi ya uongozi jambo kubwa nililojifunza ni kwamba, uongozi ni kusikiliza, It’s all about listening!
Ni raha kusikiliza, msikivu anaraha kwa kuwa anauelewa mpana. Je, ungependa kuitwa mwongeaji sana au msikivu sana. Je, ungependa mtu akitoka nyumbani kwako aseme hajawahi ona msemaji kama wewe au aseme hajawahi kukutana na mtu msikivu kama wewe.  Si vema mtu akushangae kwa kusema, “What a talker
Ni mtu jasiri peke yake anaweza kuwasikiliza waliotengwa, waliosetwa na wasio stahili katika jamii. Si rahisi kuwasikiliza wahalifu, mtu jasiri pekee anaweza kufanya hivyo.
Kwa kiongozi mpya wa nafasi na ngazi yoyote nasisitiza neno moja, sikiliza, sikiliza, sikiliza.
Tukutane kileleni wasikivu wanapopatikana.

Umeitwa kuongoza

UMEITWA KUONGOZA
Mtu hafanyiki kiongozi kwa cheo au nafasi aliyonayo katika Nyanja za siasa, taasisi, kanisa n.k; bali ni kusudi (purpose) linalozaa maono (vision) ndani yake. Sifa kuu ya kiongozi ni kuwa na maono chanya kwa mustakabali wa anachokiongoza. Mahali ambapo hakuna maono hakuwezi kuwa na uongozi, kunaweza kuwa na cheo lakini hakuna uongozi!.
Maono ndio hufanya kiongozi awe kiongozi. Siku zote watu hawafuati mtu, wanafuata maono yake. Mahali ambapo nguvu hutumika ili kufanya watu wafuate (follow) ni kwa sababu hakuna maono yanayoshawishi watu kufuata kwa utashi na hiari yao.
Ikiwa kila mtu ameumbwa kwa kusudi maalumu, basi ni ukweli uliowazi kuwa kila mtu ameitwa kuongoza katika eneo la kusudi lake; kumbuka maono ndio yanayotengeneza kiongozi na sio kinyume chake, na maono ni picha ya kusudi ndani ya mtu. Maono ndio yaliyotengeneza mtu anaitwa mama Theresa, Nelson Mandela, J. K. Nyerere, Martin Luther King Jr n.k. Maono ndio yanayotengeneza makampuni, mashirika, taasisi, ajira kwa watu, biashara, miradi (projects) na sio kinyume chake. 
Ninaposema kila mtu ameitwa kuongoza sina maana kila mtu ameitwa kuwa mwanasiasa (wapo waliokusudiwa hapa pia); na wala si swala la kuwa na cheo au kutokuwa nacho! Bali kwa kuwa umeumbwa kwa kusudi fulani, inatosha kujua mahali uongozi wako unahitajika. Uongozi wako unaweza hitajika kwenye eneo la biashara, eneo la tekinolojia, eneo la sanaa na michezo, eneo la siasa, jamii (social leader), afya, uchumi au madhabahu! (Your area of gifting and passions)
Kwanini nasema umeitwa kuongoza? Kwa sababu maono hutolewa kwa mtu mmoja kwanza kabla hayajapata wafuasi wengi; Na pia kila mtu ana eneo au nafasi yake kwa kadri ya kusudi la kuumbwa kwako sawasawa na maono aliyonayo; Ni kwa sababu ulichopewa si kwa ajili yako, ni kwa ajili ya wengine (japo na wewe utanufaika), mfano. Mwalimu hawi mwalimu kwa ajili yake, japo hupokea malipo ya kazi hio!  Kumbuka, hakuna mti unakula matunda yake wenyewe!!
There's a place for you at the top